Wednesday, April 25, 2012

Siku ya Malaria Duniani

Ugonjwa wa malaria ambao ni wakitropiki, unaendelea kuuwa watu wengi duniani na hasa barani Afrika hususani kusini mwa jangwa la Sahara. Ungonjwa huu ambao inasemekana umekuwa ukimsumbua binadamu kwa zaidi ya miaka 50'000 ni tishio kwa afya za Waafrika wengi.

Malaria huuwa zaidi kina mama na watoto
picha hii kwa hisani ya blogu hili
Asilimia 90% ya vifo vyote vya malaria hutokea barani mwetu, ambapo asilimia sitini ya vifo vyote huwa ni watoto wadogo chini ya miaka mitano. Mara nyingi malaria huambatanishwa na umasikini, na huenda ukawa moja ya vyanzo vya umasikini barani. Kuhusiswa huko na umasikini ni kutokana familia nyingi barani kushindwa kumudu manunuzi ya dawa za kuzuia maambukizi lakini pia mara nyingine kukosa uelewa wa namna ya kujikinga hususani vijijini na mijini kwenye familia zenye elimu na kipato cha kadri ama chini .
Chandarua chaweza kuzuia maambukizi
Ugonjwa huu unaweza kuzuiwa kwa kutumia chandarua kilichotiwa dawa ya kuua mbu na wadudu wengine, kusafisha vyema mazingira ya maeneo tunayoishi ili kuharibu mazalia ya mbu, kukausha na kuondoa maji yote yaliyotuama. na kadhalika.

Ugonjwa wa malaria unazuilika na inawezekana kufanya hivyo kama usemavyo ujumbe wa kataa Malaria. Na ukweli huu umedhihirika huko Zanzibar na Zambia ambapo katika ripoti za hivi karibuni, ugonjwa huo umedhibitiwa kwa asilimia zaidi ya hamsini.

Kwa kumbukumbu ya siku hii tujihadhari zaidi na kuhadharisha wenzetu wawe makini na ugonjwa huu unaoendelea kuuwa binadamu wengi zaidi mithiri ya vita.  

Taarifa za Malaria zaidi zinaweza kupatikana katika blogu hii pia. na katika blogu la unicef, who nk




Sunday, April 22, 2012

JE UMEANDIKA NINI?

Kipanya kikitoa huduma ya usafiri kwa umma. Picha toka blogu

















Hivi karibuni nilikuwa kwenye basi dogo la usafiri wa umma daladala; toka Mtwara kwenda Mikindani. Usafiri maarufu kwa daladala za Mtwara ni vipanya; vibasi vidogo vidogo ambavyo nadhani vingi ni mitumba toka Dar es Salaam. Vipanya vingi mjini hapa vimechoka na vinakwenda kwa mwendo wa kusuasua vinapokuwa barabarani. Hakuna mabasi makubwa mithili ya yale ya Mwenge Posta kwa Dar es Salaam, pamoja na hayo ule udaladala upo pale pale. Daladala ama vipanya hivi vinajaza kama ilivyo ada ya daladala sehemu nyingi Tanzania. Hapo juu nimegusia Mikindani; huu ni mji mkongwe, mji wa zamani ambao kwa bahati mbaya umesahaulika, hauendelezwi tena. Pengine kwa kuwa neema ya gesi mjini hapa imefunguliwa basi mambo huenda yakawa sawia  kwa mji huu wa kihistoria.Sasa nirejee kwenye mada ya makala hii.

Mikindani chakavu, picha na blobu ya wadau wa safari


















Katika kipanya nilichokuwa abiria, utakumbuka kuwa kwenye daladala huwa kuna mada nyingi, kondakta wetu alikuwa muongeaji kupindukia. Kodakta, konda ndivyo wanavyofahamika zaidi, huyu hatofautiani na wengi walio mikoa mingine; ni kijana aliyevalia sare chakavu ya kazi na ambapo kama walivyo wengi wao suruali yake ilikuwa ikining'inia zaiki kuliko kuvaliwa, namna hiyo ya kuvalia huitwa na vijana wa leo "kata k". Koda yule katika utani na abiria mmoja ndani ya daladala letu, ambaye nadhani ni shwahiba wake kwa jinsi walivyokuwa wameshibana kwa simulizi za kutosha bila shaka kwa lengo la kufupisha safari. Basi yule konda alimtupia rafiki yake swali ambalo hasa nd'o linabeba kichwa habari cha mada hii, hivi wewe toka umalize shule ya msingi umeandika chochote kweli?
Hivi wewe umeandika chochote kweli? Kwa hakika hili ni swali dogo sana na lategemea uzito ambao mtu ataamua kulitilia mkazo. Lakini ni jambo kubwa na muhimu sana pia. Mtu anayeandika kwa kawaida ni mtu anayesoma pia. Kwa hivi swali la konda lauliza pia, je, umesoma nini hivi karibuni? Sina hakika kama yeye mwenyewe ameandika ama amesoma chochote hivi karibuni. Tafiti na ripoti mbalimbali zinaonyesha kuwa moyo na tabia ya kujisomea kwa watu wengi imepotea ama inapotea kwa kasi kubwa . Hapo zamani ilikuwa ni lazima kuandika barua ili kujua nini kinaendelea nyumbani kwa wazazi wako walio mbali nawe, siku hizi inatosha kuweka salio katika simu ya mkoni, simu hizo karibu kila mmoja anayo yake; hii ni moja ya sekta ambazo Tanzania imepiga hatua kubwa sana, na kuanza kuongea. Anayejua kuandika ataongea kama asiyejua kuandika halikadhalika. Kukua kwa tekinolojia ya habari nako kwa kiasi kikubwa kinachangia kushuka kwa moyo wa kuandika na kusoma kama hapo awali. Hivi leo hata zile huduma za kibenki ambazo humlazimu mtumiaji kuandika japo sentensi mbili tatu zinafanywa kwa wepesi na urahisi kabisa kupitia simu ya mkononi hata na mtu asiyejua kusoma na kuandika ila tu masuala ya lazima hususani yahusuyo pesa. Maendeleo ya tekinolojia ya habari ni muhimu lakini tuendelee kujifunza kusoma na kuandika.

Hivi wewe umeandika chochote toka uhitimu elimu ya msingi, sekondari, chuo kikuu, toka upate udaktari wa falsafa?Swali hili la konda mhitimu wa darasa la saba lamgusa kila mmoja wetu toka wale wa shule ya msingi hadi madaktari wasiotimu watu ila falsafa. Nchini Tanzania pamoja na juhudi nyingi za wasomi wetu mahitaji ya vitabu vya mafunzo mbalimbali bado ni vichache; tunaendelea kutumia vitabu toka ng'ambo. Hili si jambo jema hata chembe.

Wito kwa kila mmoja wetu tuongeze muda wa kusoma vitabu zaidi na kufanya hivyo tutapata hamu na ujumbe wa kuandika chochote kitu kwa lengo la kuielimisha jamii, ambalo ni jukumu la kila mmoja wetu.

Monday, April 16, 2012

MANENO MAKALI HAYAVUNJI MFUPA

The image by the courtesy of Google
                                   
"The smallest deed is better than the greatest intention." John Burrough.
Maneno Makali hayavunji mfupa!

Wazo hili nimelipata katika mtandao wa advance Africa. Mtandao ambao siku zote hutoa kwa wahitaji fursa za masomo na kazi zaidi . Mtandao huu ni nyenzo nzuri wa vijana walio masomoni na wanaotarajia kumaliza masomo yao na kujiunga na ulimwengu wa kazi.

Mtandao huu huonyesha fursa za kazi kwenye nchi mabalimbali ikiwa ni pamoja na ughaibuni. Kwanza nieleweke vyema kuwa jambo muhimu kwa mwenye kuweza kulifanyia kazi, ni mtu binafsi kujiajiri ni vyema akafanya hivyo japokuwa si vibaya kama atafanya kazi sehemu nyingine kwanza ili apate mtaji wa kuanzisha shughuli zake binafsi. Kwa wale wanaopenda kufanya kazi za kuajiriwa, wanaweza pia kufikiria kazi za hapa nchini na pia zile za kimataifa. Vijana wetu wafahamu kuwa kazi hizo zipo pia kwaajili yao si tu kwa watu wa mataifa mengine. Hata hivyo ili kuweza kupata fursa hizo ni vyema kuzingatia masuala kadhaa yenye umuhimu usio kifani. Weledi, uaminifu, kujiamini na kujituma, ujuzi wa lugha za kigeni, utayari kuishi katika tamaduni mchanganyiko na kadhalika.

Weledi ni kigezo cha uhakika kwa mtu kufanya kazi popote apendapo. Weledi ni msamiati ulioibuka hivi karibuni ukimaanisha ujuzi na uwezo wa kufanya kazi. Wanachuo ama mtu yeyote anayetaka kufanya kazi ni vyema awe na ujuzi wa kile anachotaka kufanya hii ni muhimu hasa. Hapa linaibuka swali la mtu anapata vipi uwezo na ujuzi wa kazi ili hali ndo kwanza anatoka masoni? Swali hili lafaa kujibiwa na fursa za kujitolea; vijana wanafunzi, wanavyuo tujenge utamaduni wa kujitolea kufanya kazi katika makampuni, mashirika na hata kati taasisi za kidini ili mradi kuwe na fursa ya kujijenga katika utendaji kazi na hapo hakutakuwa na ukosefu wa ujuzi.

Uaminifu; ni moja ya mahitaji muhimu katika ulimwengu wa kazi na ujasiriamali. Katika ulimwengu wa mtaji jamii "social capital" uaminifu ni suala la lazima katika mafanikio, ili ufanikiwe ni lazima uwe na mtandao mkubwa na mpana, huwezi kupata mtandao mkubwa vile kama wewe si mwaminifu. Kwa hivi basi ni lazima kujifunza kuwa mwaminifu. Tunu ya uaminifu ni moja kati ya zawadi amabazo watu wengi hujifunza toka katika familia zetu; huwatazama wazazi wetu jinsi wanavyoishi na hii hurithi toka kwao. Hata hivyo kulingana na uwezo mkubwa wa ubongo wa binadamu; unaweza kujifunza kila kitu mradi tu upatiwe mazingira na kuwe na nia na ulazima wa kufanya hivyo.

Kujiamini na kujituma; hivi ni vigezo muhimu katika mafanikio. Ili uweze kufanya jambo fulani ni lazima kwanza wewe mwenyewe ujiamini kuwa unaweza kulifanya, lakini kujiamini peke yake haitoshi ni lazima kujituma katika kile unachonuia kukifanya. Tunu hivi mbili ukiziweka pamoja basi una uhakika wa kufanikiwa. Msemo wa Kiswahili Penye nia pana njia unafaa uwe kielelezo na mwongozo katika malengo yako maishani.

Ujuzi wa lugha za kigeni; hiki ni kitendea kazi muhimu hasa hususani katika zama zetu za utandawazi. Katika nyakati hizi watu wengi zaidi husafiri, kufanya hivyo kuna walazimu kujifunza lugha kadhaa. Wewe huna sababu ya kutojifunza lugha muhimu za maitaifa mengine hasa zile zenye ushawishi kwa mataifa mengi. Unaweza kujifunza na kutawala vyema zaidi Kiingereza, Kifaransa, Kispanyola, na sasa kwa sababu za kiuchumi, watu wanajifunza kichina. Ujuzi wa lugha nyingi utakufanya uwe mshindani mkubwa na kujitofautisha na hata wale waliofanya kazi siku nyingi.

Utayari kuishi katika tamaduni mchanganyiko; binadamu sisi ni wamoja kwa namna zote muhimu. Binadamu ana undwa kwa chembe hai ndogo ndogo ambazo ni sawa kwa kila binadamu, ana mifumo kadhaa ambayo hufanya kazi sawa sawa na kadhalika. Hata hivyo tamaduni, mazingira, makuzi n.k huleta tofauti tulizonazo katika jamii za binadamu zilizosambaa katika uso wa sayari ya dunia. Tofauti hizi muhimu ndo hutufanya tufanikiwe kwani hutujengea ushindani mioyoni mwetu. Sasa kama unataka kufanikiwa ni lazima ujifunze kuishi na watu wa jamii zingine; kupitia wao utajifunza taaluma na tekinolojia za watu wengine. Ukipata fursa hiyo; itumie vyema kwani unaweza kuibadilisha dunia toka duniani kote!

Kwa wanaotafuta nafasi za kazi na masomo nje ya nchi tafuta kwa kubonyeza hapa


Saturday, March 31, 2012

KIFO: UKAMILIFU WA UBINADAMU

Sehemu ya umati uliofika kumuaga mwanachuo aliyeaga dunia
















Kama ilivyo kwa mawiyo na macheyo ya jua, ndivyo ilivyo kwa kuzaliwa na kifo. Msemo mmoja wa kiafrika wasema: "Kamwe ardhi haichoki kutupokea" ama kama inavyojidhihiri katika vitabu vitakatifu; kuna muda wa kila jambo: kupanda na kuvuna, kuzaliwa na kufa... ama tena binadamu u mavumbi na mavumbini utarudi. Na zaidi na pengine muhimu kupindukia; mbegu isipoanguka ardhini na kufa hubaki kama ilivyo, lakini ikianguka na kufa huzaa zaidi na zaidi kuliko ilivyokuwa hapo kabla. Mbegu ya mmea wowote inaweza kufananishwa na maisha ya binadamu.

Inafaa kukumbushana kuwa mara tu binadamu anapotungwa kwenye tumbo la mamaye, tayari anakuwa na sifa za kuaga dunia, kufa. Hii inadhihirisha kwa maisha ya vichanga ambavyo hata kabla ya kuzaliwa, hufariki dunia. Vijana wengi hudhani ya kuwa kifo ni kwaajili ya wazee; watu walioishi kwa miongo kadhaa hapa duniani. Ni vyema tuambiane kuwa hii si kweli, kila binadamu yupo tayari, ameiva, amepevuka kwaajili ya kifo. Kama isemwavyo hivi leo kila mtu ni marehemu mtarajiwa. Kwa mantiki hiyo basi hatuna haja ya kuogopa. Kinyume chake inafaa tujiandae kwa tukio hilo la uhakika kama ilivyo kwa kuchomoza jua bila juhudi zetu kila asubuhi, kwa uzoefu tu twafahamu kuwa jua litachomoza. Pamoja na kujua ukweli huo bado hatuzoei suala hili.


Jeneza likiwa ndani ya ndege tayari kwa safari

Kamwe hatuzoei kifo kwa sababu kila kinapotokea, kinatokea kwa mtu ambaye hajawahi kufa. Najua hili si jambo geni lakini huo ndo ukweli wenyewe, je ni kwanini? Jambo hili li hivyo? Bila shaka ni kwa sababu kila mtu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kiimani twaelewa kuwa binadamu ameumbwa na Mungu na kuwa binadamu nd'o kazi nzuri kuliko kazi nyingine zote za Mungu na ni kwa sababu hiyo kila anapofariki dunia mwenzetu basi sisi hupatwa na simanzi lisiloelezeka, hata wale wenye mioyo migumu huguswa pia na kifo cha mpendwa ama mwanadamu ambaye walimfahamu, kuishi naye na kadhalika. Kifo ni sehemu ya ukamilifu wa binadamu.

Katika vitabu vitakatifu twaambiwa ya kuwa Mwenyezi alitufahamu hata kabla ya kuiumba dunia hii, kama nilivyoeleza hapo awali, binadamu kwa hakika ni kazi bora kabisa ya Mwenyezi Mungu. Twajua pia kuwa binadamu huanza kibaiolojia pale yai la mwanamke linaporutubishwa na mbegu ya mwanamume: kuanzia hapo safari ya binadamu fulani kibaiolojia huanza, na maisha yake huanza hapa duniani kwa kuzaliwa. Binadamu anazaliwa anaishi na hatimaye lazima afariki dunia. Kupitia kifo mzunguko wa binadamu unakamilika. Hivyo tukichukulie kifo kama ukamilifu wa ubinadamu wetu. Hata hivyo jambo la msingi hapa ni je, maisha hayo tunayaishi vipi hapa duniani?

Hivi leo wengi tunadhani kazi yetu katika sayari hii ya dunia ni kukusanya na kujilimbikizia mali nyingi iwezekanavyo. Tunajisahau, ukweli na wito wa binadamu ni kutoa mchango wa kuiboresha zaidi dunia kwaajili ya utukufu wa Mungu kama asemavyo Inyasi wa Loyola (1491-1556) . Tunaweza kuiboresha dunia kila mmoja kwa nafasi yake; mwalimu afanye kzi yake ya ualimu vyema, mwanasiasa afanye kazi yake vizuri, mwandishi, mkulima, mwanasayansi, mwanafalsafa, mwanafunzi na kila mmoja wetu afanye vyema kabisa kazi yake. Kushidwa kufanya vyema ama kutimiza wajibu wetu ni sawa na kushindwa kuitikia wito wa maisha yetu na tukishindwa kufanya hivyo basi maisha yetu yanakosa maana!

Tafakari hii imenijia baada ya kuona nyuso nyingi za huzuni wakati wa kumsindikiza mwanachuo wa stemmuco hivi karibuni baada ya kukamilisha safari yake hapa duniani.

Saturday, March 17, 2012

Mkanganyiko wa Maisha: Misitu ama Maisha?


Baiskeli hii TZ MKAA ikiwa imeengesha bidhaa kusubiri wahitaji mjini Mtwara
Kuishi kwenye jumuiya ya wasomi ni faida kubwa. Msomi, kwa tafsiri yangu ni mtu yeyote mwenye elimu kuanzia darasa la saba, ama kwa upana zaidi anayejua kusoma na kuandika, lakini mwenye moyo wa utafiti, kujisomea na kuwashirikisha wengine taarifa ya anachosoma ama anachotafiti.

Mwanachuo wa Stella Maris Mtwara University College (STEMMUCO), ambao kwa maelezo yangu ni wasomi, wapo katika harakati za kuandika taarifa, ripoti ya tafiti walizofanya sehemu mbalimbali hapa nchini. Kuna mada nyingi karibu kadri ya idadi ya watafiti hao. Kuna ripoti juu ya hali ya uchumi nchini, hali ya hisabati shuleni, nafasi ya sayansi katika elimu ya tanzania, hali ya elimu nchini, ushiriki wa wasichana katika elimu, jando na maendeleo, kwa ufupi nyanja zote muhimu zimeguswa, kuanzia siasa, uchumi, sayansi, na jamii. Zaidi tasnifu hizo za wasomi zimeangazia makundi mbalimbali katika jamii; wazee, wanawake, walemavu, vijana na kadhalika.

kwa ufupi, makala hii inagusia mkanganyiko unaowakuba vijana wanaofikia kundi la kujitegemea maishani. Hili ni kundi muhimu mno; hii ndio nguvu kazi hitajika ya ujenzi wa taifa letu. Tafiti zinaonyesha kuwa kundi kubwa la vijana karibu ya vijana milioni mbili na laki tatu (2.3), takwimu rasmi za serikali ya Tanzania 2005, hawana ajira zinazoeleweka. Kumbuka hii ni idadi ya makadirio tu, kuna idadi kubwa sana ambayo mara nyingi haijumuishwi kwenye taarifa rasmi, kwa hivi basi, vijana wengi hawana kazi. na wanakumbana na mkanganyiko wa maisha.

Baadhi ya sera zinakataza ama zinapiga vita shughuli ambazo vijana huzitegemea kuendesha maisha yao. Bishara ya mkaa ni moja ya biashara zinazopigwa vita kwa vile watayarishaji mkaa wengi huvuna miti kwaajili ya kuni bila mpangilio maalumu. Ni kweli zao la mkaa linaharibu mazingira na kuhatarisha dhana ya maendeleo endelevu. Wakati zao hili linapigwa vita, mahitaji na matumizi yake ndo kwanza yanazidi kuongezeka kila uchao. Na hii ni dhahiri kuwa mkaa ni bidhaa ambayo itaendelea kutumika kwa miaka mingi ijayo; kama wasemavyo vijana wa Bongo Flava; mkaa bado tutakuwa nao kwa muda mrefu sana. kumbe tufanye nini sasa.

1. Mosi, maafisa misitu, ama wataalamu wa maliasili waweke utaratibu wa kupanda miti kuwe na maeneo maalumu ya kupanda miti na vijana wavuna miti kwaajili ya mkaa wapewe maeneo ya kupanda miti na kuitunza ili hali waonyeshwe eneo maalumu la kuvuna miti ya kazi yao hiyo.

2. Pili, mamlaka husika zenye kujihusisha na gesi ya kupikia majumbani waangalie uwezekano wa kupunguza kwa kiasi kikubwa kodi za chanzo hicho mahususi cha nishati hitajika ili wananchi wengi ikiwa ni pamoja na mashambani waweze kuitumia pia.

3. Tatu, tafiti zifanyike kuangalia upunguzaji wa bei ya umeme ili walio na fursa ya kutumia nishati toka shirika la taifa la umeme watumie pia kwa kupikia; kwa sasa bei yake ni kubwa mno kwa mwananchi mwenye kipato cha wastani kumudu gharama hizo.

Mpanda baiskeli akitafuta wahitaji wa biadhaa yake manispaa ya Mtwara-Mikindani
Nchini Tanzania hali halisi ndivyo ilivyo vijana wengi wamejiajiri kuuza mazao ya miti

Tukifanya haya kuna uwezekano wa kufikia ndoto tuliyonayo ya kuwa na Watanzania wa daraja la kati ifikapo 2025 kama inavyoelezwa kwenye mpango wa maendeleo wa taifa. Kinyume na hivyo vijana wetu wataendelea kuwa kwenye mkanganyiko mkubwa wa misitu ama maisha ya leo; je nikate miti ili nichome mkaa ama nisikate na kufa njaa? 

Wednesday, March 14, 2012

Siku ya Wanawake STEMMUCO - MTWARA


Sehemu ya wanawake wakifuatilia matukio

Wajumbe wakifuatialia mtiririko wa matukio
Akina mama wakifanya utambulisho siku ya kimataifa ya wanawake duniani



http://www.stemmuco.ac.tz/index.php

Sunday, March 11, 2012

Mashindano ya PRO-LIFE - MTWARA

Picha kwa hisani ya google
Mashindano ya Pro life, ambayo yanaanza kujenga mizizi mjini Mtwara, kwa mwaka huu 2012 yamefunguliwa rasmi hapo jana. Mashindano hayo yanajumuisha taasisi kadhaa za elimu mjini Mtwara.

Moja ya malengo la mashindano haya ni kujenga uhusiano baina ya wanavyuo katika manispaa ya mji huu wa kusini mashariki mwa Tanzania. Yanatumika pia kama sehemu ya matumizi sahihi ya nguvu za vijana; kundi la watu wenye nguvu kubwa za mwili. Mashindano ni sehemu ya mazoezi muhimu yanayohitajika kwaajili ya kujenga na kuulinda mwili.

 Pamoja na malengo mengine mahususi na mazuri mno yaliyotajwa; Jina la mashindano haya lengo lake hasa ni kutetea na kulinda uhai kama jinsi ilivyo kwa malengo halisi ya "Pro-life". Pro life ni vuguvugu lenye lengo mahususi la kutetea na  kulinda uhai wa binadamu. Binadamu huanzia kwenye muungano wa yai la mama na mbegu ya baba, na hapo safari ya mwanadamu mpya huanza. Kwa hiyo binadamu anaanzia tumboni mwa mama hata kabla ya kuzaliwa. Kutokana na maelezo hayo basi utaona kuwa Prolife hutetea uhai wa mtoto anayekuwa tumboni mwa mama na kwa hivi hupinga utoaji mimba kwa lengo la kutetea na kulinda uhai.

Kwa hiyo basi vijana wa kike na wa kiume wanaalikwa kuheshimu uhai wa mwanadamu kwa kujizuia kabisa kushiriki katika utoaji mimba. Kunaweza kuwa na sababu lukuki za kuhalalisha utoaji mimba lakini ukweli ni ule ule kwamba utoaji mimba ni uuaji ni uharibifu wa maisha. Vijana hivi leo wanashindwa kujizuia kushawishiwa kutoa mimba; njia rahisi ya kuepuka kujiingiza kwenye kosa hilo ni kuwa na mahusiano yenye heshima. Mvulana na msichana wawe marafiki ili kusaidiana kukua kikamilifu katika ubinadamu (mwanaume hujifunza toka kwa mwanamke na kinyume chake pia) mahusiano ya kimwili yasubiri vijana watakapofunga ndoa na kutambulika mbele ya jamii na mwenyezi kuwa wao ni bwana na bibi fulani. Kufanya hivyo kutasaidia kuondoa utoaji mimba-uuaji!

Katika tafsiri ya leo ya kutetea na kulinda uhai vijana tunaalikwa kuacha mambo yote ambayo yanapunguza maana ya maisha yetu. Vijana tupunguze ama kuacha kabisa unywaji wa pombe, tuache uvutaji wa sigara kwa kuwa hasara na matatizo yanayosababishwa na uvutaji ni makubwa kuliko furaha ya uvutaji. Kwa wale tunaotumia dawa za kulevya tuache na tuwashawishi rafiki zetu waache ushiriki na utumiaji wa vitu hivi vinavyopingana na maisha. Tukifanikiwa katika hayo amani, upendo na mafanikio vitatamalaki kote duniani, lakini vianzie kwa kila mmoja wetu.

Kwa hivi basi mashindano ya "STEMMUCO Pro-life 2012" yanalenga kutetea na kulinda uhai wa binadamu. Vijana wote walio mashindanoni wanapaswa kufahamu hilo na kwamba wao tayari wanakuwa ni mabalozi wa uhai-ni watetezi na walinzi wa uhai. Mashindano mema!!!

Thursday, March 8, 2012

Siku ya Wanawake duniani katika matukio Mtwara

Vazi rasmi siku hiyo ilikuwa kitenge - Naam kina mama wanapendeza
na kuongeza staha sana kwa mwanamke pale wanapovalia mavazi ya heshima




























Hii ni siku mahususi kwa wanawake duniani. Hutumika kuwakumbusha wanawake wenyewe, watunga sera, na jamii yote kwa ujumla juu ya haki na nafasi ya mwanamke katika nyanja zote za maisha.































Tafiti nyingi hapa Tanzania zinaonyesha kuwa mwanamke hususani yule wa kijijini anafanya kazi nyingi kuliko mwananchi mwingine yeyote. Pamoja na mchango huo mkubwa wa wanawake, mara nyingi juhudi zao hazitambuliki vya kutosha na wala hawathaminiwi na jamii kwa kiasi stahiki. Hivyo kwa siku ya leo ni fursa kuikumbusha jamii na wanawake wenyewe hasa wale wa mashambani. Ni dhahiri kuwa wanawake wengi vijijini wanafanya kazi nyingi kwa kuwa tamaduni nyingi, zenye mfumo dume, zinawalazimu kufanya hivyo.





























Tunawaomba na kuwapa changamoto wanawake wa mijini, kulihamasisha kundi hili lenye mchango mkubwa kwa uchumi wa nchi yetu. Mwaka huu, kwa kutambua nafasi ya elimu kuleta mabadiliko kwa jamii, wito umeelekezwa kwa ushiriki wa mtoto wa kike katika elimu kama kichocheo kikubwa kuleta maendeleo ya jamii.

Saturday, March 3, 2012

Duh angurumapo simba mcheza nani?


Hii toka kwa kaka michuzi
Hakuna ubishi kuwa watu wengi tunapenda mchezo wa soka hapa Tanzania.

kupitia huu upenzi wa mpira kwanini tusibuni njia ya kuhamasishana kwenye elimu kupita soka ili kiwango na ubora wa elimu yetu vikue pamoja na soka hasa la kina mama; soka la kina mama Tanzania ni bora zaidi kuliko la kina baba, kwa kigezo cha matokeo. Taifa Stars imewahi kuifunga timu nyingine mabao matano?


Hii ni keki tuliyokula siku ya ufunguzi wa Simba TV. Hata hivyo TV hiyo inayorusha vipindi vyake kupitia clouds tv inaishia tu mikocheni, haifiki walipo watazamaji wa mdenga, Mtwara, Lindi, Mazoo, Shytown, Ta etc fikisheni mapema basi! 

Harakati za Ubunifu wa vazi la Taifa?




Picha zote kwa hisani ya blogu la UDADISI

Thursday, March 1, 2012

Mtazamo Chanya Humjenga Binadamu!

Maneno haya ya kiingereza juu ya rais huyu wa Marekani ni fundisho la aina yake
tujifunze kupenda tunachofanya na tukifanye kwa moyo wote matokeo yake ni furaha na amani
Ujumbe huu nimeupata toka kwenye e-mail niliyotumiwa na Edward Ezekiel, kwa hakika ni ujumbe mzuri na wa maana mno.

Huu unawafaa vijana wote ambao ni wepesi wa kukatishwa tamaa na watu wengine. Kumbuka hakuna mtu mwenye mamlaka ya kukufanya ukose furaha, ili ukose furaha, ukasirike ama uwe kwenye aina yote ya hisia ni lazima wewe mwenyewe uamue; Lincoln ni mfano mzuri mno. Maneno ya watu wengine si yenye kutubomoa.

Fundisho la pili ni kufanya kazi zetu kwa uadilifu, ubunifu, umakini na zaidi ya yote upendo. Mambo hayo husaidia kuvumbua mbinu mpya za kurahisisha maisha na kuleta maendeleo kwa watu haraka. Ndugu huyu japo si Mwafrika na atukumbushe kutenda mema!

Je Afrika imejididimiza yenyewe?

Ndugu zangu salam,
Kigoda cha Taaluma cha Mwalimu Nyerere kinawakaribisha wote kwenye , Malumbano ya Hoja baina ya Wanafunzi wa Sekondari na Chuo Kikuu, mada ni " Handira hii inaamini kwamba Afrika imejididimiza yenyewe" ikifuatiwa na filamu ya "The Last Days of Walter Rodney" hapa UDSM-katika ukumbi wa Nkrumah, tarehe 03.03.2012 siku ya Jumamosi kuanzia saa 4:00 asubuhi mpaka 8:15 mchana. Malumbano haya ya hoja yatakuwa katika lugha ya Kiswahili. Nawaombeni tusambaze tangazo hili kwenye mitandao yetu ya jamii. Karibuni sana.
Nimeambatanisha ratiba na bango bonyeza hapa.

Walter Rodney Luanda
Mwalimu Nyerere Chair-Senior Administrative Officer

Tuesday, February 28, 2012

Kumbe wabunge wetu ni maskini vile !

Jengo la kisasa la Bunge la Tanzania huko Dodoma
Mbunge ni mwakilishi wa moja kwa moja wa wananchi wengine kwenye chombo rasmi cha kuwasilishia mawazo na maoni ya wakaazi wa nchi wenzake. Kwa hivi ni mtu muhimu katika jamii, japokuwa anabaki kuwa mtumishi wa wananchi, kwani wao ndio hasa wanaompatia ridhaa ya kuwaongoza.

Sasa ili mtu huyu aweze kufanya kazi yake vizuri ni vyema kwa hakika kuwa na mazingira stahiki ya kufanya kazi zake kwa weledi na hasa kwa uzalendo unaojidhihirisha kabisa.

Ili kuwa mbuge kwa Tanzania, tunahitaji mtu mwenye kuwa na sura na mfano wa watu anaowawakilisha ndio maana enzi zile wakaitwa 'ndugu' hivi leo ni waheshimiwa. Pamoja na kufanana na waajiri wake kwa maana ya kuyafahamu vyema mazingira yao na inafaa zaidi akiishi huko huko na wala si mjini tu, inafaa awe na nafasi kiasi ya kiuchumi kiasi ili mambo mengine yanayohusu kazi yake aweze kuyamudu kwa pesa zake mwenyewe. Si saw kila kazi ihitaji kodi za watanzania, hapo ndio has inafaa ajiulize anaifanyia nini Tanzania?

Makala hii imechochewa na taarifa niliyoiona kwene televisheni hivi karibuni na hatimaye kuingia kwenye mtandao wa youtube ikielezea japo kwa kifupi tu hali ngumu kiuchumi ya ndugu zetu wabunge. Hayo yamedhihirishwa na kiongozi wa bunge hilo la Tanzania alipoongea na wananchi wa jimbo lake huko Njombe. Kwa habari zaidi tazama hapa

Kwa hakika jambo hili nimeniacha na maswali mengi kuliko majibu. Kwanini watangaza nia hutumia nguvu na wakati wao mwingi vile kujinadi mbele ya wapiga kura ili wapate nafasi hii yenye umasikini wa kutupa?

Je, wengi wao huenda bungeni bila kujua kuwa kuna umasikini wa kiwango hicho?

Uwezekano mwingine wa suala hili ni kuwa watangaza nia na hatimaye wabunge wetu ni watanzania wenye uzalendo sana na  hakika maslahi ya taifa letu yamo mioyoni mwao kiasi kwamba pamoja na umasikini ulio bungeni, ambao nadhani watakuwa wakiufahamu kwani kwa hali ya kawaida mtu hufanya kwanza utafiti wa kile anachokitatuta, bado huamua kwenda bungeni kwenye umasikini wa kutupa.

Wabunge ni wawakilishi wa moja kwa moja wa watanzania. Na hivi wanabeba sura ya nchi yetu; bunge pale Dodoma likiwa kazini inamaanisha kuwa Tanzania yote kupitia majimbo ipo pale katikati ya nchi hii tukufu, na hivyo wawakilishi hawa lazima kuwajali vilivyo. Sasa kwa kuwa kiongozi wa moja ya nguzo kuu za uongozi wa taifa letu amesema kuwa kuna umasikini katika chombo hicho, itakuwa vigumu kwa hawa watumishi wetu kufanya kazi vizuri. Inafaa tutatue tatizo hili kwa kuwawekea wazalendo na watanzania wenzetu hawa mazingira mazuri ya kufanya kazi. Kwa kuwa tuna uzoefu wa kutatua matatizo yetu wenyewe basi natulitatue njia mojawapo ni kuunda tume kwaajili ya kuchunguza ukata unaowakabili waheshimiwa wetu.

Kupitia uchunguzi huo tupate mwongozo wa nini cha kufanya...
Picha zote kwa hisani ya google!

Wednesday, February 22, 2012

Uelewa kwa vitendo!

Wanachuo wakionyesha uelewa kwa vitendo chuoni STEMMUCO
Hapa kaka akifanya kweli
Wanachuo wakionyesha uelewa kwa vitendo chuoni STEMMUCO
Dada hakubaki nyuma katu!

Monday, February 20, 2012

Elimu ya Majanga - Zima Moto!

Ndugu Ibrahim Badiri - Mtaalamu wa kikosi
Cha zima moto Manispaa Mtwara-Mikindani
akitoa mafunzo juu ya majanga hususani moto
Baadhi ya wanachuo wa Stella Maris Mtwara University College (STEMMUCO) walipata mafunzo juu ya majanga na hasa juu ya moto.

Katika mhadhara huo uliofanyika chuoni hapo, ndugu Badiri alisema watanzania wengi hawana elimu ya kujiokoa toka kwenye majanga na hivyo basi tatizo kama la moto linapotokea inakuwa vigumu kujiokoa.

Mtaalamu huyo alichanganua aina za moto: moto utokanao na mada za kioganiki, moto utokanao na hitilafu ya umeme, moto utokanao na gesi na moto utokanao na madini na vyuma mbalimbali. Kupambana na moto alisema kila aina ya moto huzimwa kwa kizima moto mahususi.

Moto wa vifaa vya kioganiki huweza kuzimwa kwa maji, poda / unga mkavu maalumu, mchanga
Moto wa umeme huzimwa kwa poda/unga mkavu maalum,
Moto wa gesi, kama ule wa kituo cha mafuta huzimwa kwa mchanga, poda / unga mkavu maalum
Moto wa madini huzimwa kwa poda/ unga mkavu maalumu.

Baadhi ya wana STEMMUCO wakifuatilia mafunzo hayo
Hata hivyo mtaalamu huyo alisema njia hizi hufanyika zaidi kama huduma ya kwanza na pia kwa moto ambao bado haujawa mkubwa, hulenga zaidi moto ambao ndo kwanza unaanza.

Sunday, February 19, 2012

Binadamu hujiumba

A man, as a general rule, owes very little to what he is born with - a man is what he makes of himself.










































Kanuni ya maisha ni kwamba, binadamu hutegemea kwa kiasi kidogo mno kile anachozaliwa nacho, kimsingi binadamu anaamua yeye mwenyewe kuwa anavyotaka yeye mwenyewe.

Alexander Graham Bell.

Mwenyezi Mungu anatuumba mara moja na kutupatia pumzi ya uhai. Pumzi hiyo ya uhai nd'o has maisha yenyewe; hiyo ndo hasa sayansi bado haiwezi kuelezea ni nini hasa. Tunapozaliwa tunakuwa tumekamilika idara zote za miili yetu. Hata hivyo maamuzi ya binadamu awe nani ni suala na maamuzi binafsi lakini muhimu hasa kama tunapenda maisha yetu yawe na maana na kuleta furaha na maana kwa maisha ya watu wengine.
 
Kuvumbua, kuibua, kuja na wazo jipya na kadhalika ndo hasa mambo amabayo tunatakiwa tuyafanye ili kweli maisha yetu yawe na maana kabisa. Kutafuta na kukusanya mali kwa bidii zote (hili ndilo jambo ambalo wengi wetu hulifanya) ni muhimu na vyema kabisa ili kuupiga vita umaskini na uhohehahe lakini pesa isiwe ndio lengo letu kuu; pesa itumike tu kuboresha maisha ya jamii ya wanadamu kote duniani.
 
Hivi leo vijana wengi hapa Tanzania hatufahamu hasa nini maana ya maisha yetu tunadhani lengo la maisha ni kusaka pesa tu "mkwanja" hasa tukikutana na maneno na ushawishi wa vijana wa Marekani ama bara Ulaya, "Jitahidi kupata mali maishani ama kufani". Kamwe hili si lengo la maisha, jambo muhimu tukumbuke kila mwanadamu ana nafasi ya kujiumba na kuwa anavyotaka awe! 

Friday, February 3, 2012

Maneno ya kujenga na kuimarisha zaidi

Maneno ya kujenga na kutia moyo kwa vijana na wengine wote wenye nia ya kujiendeleza yanapatikana katika mtandao wa Advance Africa ambao hutoa taarifa ya nafasi nyingi za masomo ya juu zaidi. Kwa wanaopenda kujifunza juu ya nafasi hizo wasome hapa


If you think you are beaten, you are.
If you think you dare not, you don't.
If you like to win but think you can't,
It's almost a cinch you won't.

If you think you'll lose, you're lost.
For out in the world we find

Success begins with a fellow's will.
It's all in the state of mind.

If you think you are out classed, you are.
You've got to think high to rise.
You've got to be sure of your-self before
You can ever win the prize.

Life's battles don't always go
To the stronger or faster man.

But sooner or later, the man who wins
Is the man who thinks he can.

C. W. Longenecker.


        "When one door closes another door opens; but we so often look so long and so regretfully upon the
                                      closed door, that we do not see the ones which open for us."

 Alexander Graham Bell.






Tuesday, January 31, 2012

Mgomo wa madaktari Tanzania

Baadhi ya matabibu na wauguzi wa hospitali ya
Muhimbili wakijadiliana mambo kadhaa picha kwa
hisani ya rfi Kiswahili

















Tunawapa pole wote wanaoathiriwa na mgomo huu!

Binadamu, kulingana na biolojia tunayoifahamu sisi wanadamu hivi leo, ndio mnyama mwenye ubongo mkubwa na wenye kufanya kazi vyema zaidi kuliko wanyama wengine. Bila shaka ukweli huu upo kwa lengo mahususi na si kwa bahati mbaya.

Binadamu mara tu anapozaliwa ana jukumu muhimu kwa dunia hii, hiyo ni moja kati ya sababu nyeti za uwepo wake hapa duniani - la raison d'être. Hali hiyo ni lazima kwa kila kilicho!

Hivyo basi, lazima tujiulize hivi nini hasa sababu ya uwepo na wajibu wa serikali kwa wananchi wake, ikiwa ni pamoja na madaktari? Nini sababu ya uwepo na wajibu wa madaktari hapa duniani?

Bila shaka kwa kutumia ubongo wenye uwezo mkubwa wa kupambanua magumu, tunaweza kupata suluhu ya tatizo hili...  

Sunday, January 29, 2012

KUSOMA VITABU KWAJENGA SANA


Hatimaye nimemaliza kusoma  "The Innocent Man"  cha John Grisham

Kitabu hiki kinajadili mambo mengi ya msingi mno kwa maisha ya binadamu. Mawili kati ya hayo ni; mosi jinsi ambavyo mfumo wa sheria, niruhusu kusema duniani, unavyoweza kuwa na mapungufu ya kutoa haki kwa binadamu, pili jinsi ambavyo watoa huduma wengine walivyo makini kuona haki inadhihirika na binadamu anatendewa haki katika mfumo wa sheria. Jambo la pili limenifurahisha sana!

Ni kitabu kizuri mno ambacho kinaweza kuamsha na kujenga moyo na usawasha wa kutenda mema katika jamii. Moyo wa kuona ukweli ukipatikana unaweza kuwa katika nyanja anuwai ama zote za maisha ya binadamu. Asante ndugu Grisham kwa kutushirikisha mawazo mazuri kabisa, huu ndo uzuri wa ubinadamu! 

Tuesday, January 17, 2012

DAWA BANDIA ZA MALARIA NI KIFO KWA AFRIKA...

Tabibu akitoa huduma kwa Mtoto mgonjwa wa malaria













Hivi karibuni kumekuwa na wimbi la bidhaa nyingi bandia... karibu kila kitu unachonunua ni kama kuna mbadala wake ambao ni bandia. Hali hii imeonekana kuwa ni kitu cha kawaida na hali inayokubalika kimaisha. Hali hii la hasha haijakubalika kisheria, ambapo kuna nyaraka rasmi kwamba kuanzia sasa tuwe na bidhaa bandia, lakini kulingana na jinsi mambo yanavyokwenda basi tunaweza kusema ni hali iliyokubalika. Bidhaa bandia nyingi zinasemekana kutoka nchi za mashariki zinazoendelea kiuchumi.

Inasemekana kuwa katika nchi hizo za mashariki hususani Uchina; unaweza kutengenezewa bidhaa ya aina yoyote kulingana na uwezo wako wa kifedha. Tatizo hili linasababishwa na wafanyabiashara wenye uchu wa kujitajirisha haraka... utajiri si jambo baya ila utajiri kwa njia isiyo sahihi ni makosa. Lazima mambo haya ya bidhaa BANDIA TUYAKEMEE, na katika afya ni hatari zaidi.

Dawa bandia kwa hakika ni kifo kwa bara la Afrika, takwimu za shirika la afya duniani WHO linaonyesha kuwa Malaria ndo ugonjwa unaoongoza vifo vya watu wengi zaidi barani humo, bara linawekwa kwenye orodha za umasikini duniani. Kuzuka kwa wimbi la dawa bandia za ugonjwa huo unaoongoza kwa vifo barani ni sawa na kutoa hukumu ya kifo kwa waafrika hususani wale wenye kipato duni; sehemu kubwa ya Waafrika. Jambo la kusikitisha hapa ni kuwa hukumu hii inatolewa na ndugu zetu wa barani humu.

Wanaoingiza nchi dawa bandia za Malaria ni ndugu zetu waafrika, kwa hili tusimame pamoja tuwaambie acheni kuua ndugu zetu- wafanyabiashara wanaoingiza, wanaoagiza dawa bandia hawana utu na ni wauaji - waache kufanya hivyo!

Taarifa hizi zinapatikana pia kwenye wavuti wa Bbc Kiswahili

MZEE JANGALA AONGELEA SANAA

  Na Mwandishi wa BASATA
 Msanii Nguli wa sanaa za maonesho, Bakari Kassim
Mbelemba (Mzee Jangala) aikizungumza na
wadau wa sanaa kwenye Jukwaa la Sanaa


Msanii nguli wa Sanaa za Maonesho, Bakari Kassim Mbelemba (Mzee Jangala) amesema kuwa programu ya Jukwaa la Sanaa inayoendeshwa na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) ni chuo tosha kwa wasanii katika kuwapa elimu na ufahamu wa masuala mbalimbali ya sekta ya Sanaa.

Akizungumza wiki hii, kwenye programu hiyo katika ukumbi wa BASATA, Ilala Sharif Shamba, Jangala alisema kuwa, Jukwaa la Sanaa ni jambo la kujivunia na ni chachu ya kukua kwa Sanaa.

“Jukwaa la Sanaa ni programu inayonifanya nithubutu kusema, sasa Sanaa ni kazi, maana kazi yoyote ili ifanywe kwa ufanisi inahitaji elimu, uratibu na mwongozo, hivyo wasanii tuitumie fursa hii adimu” Jangala alisema.

Aliongeza kuwa, programu hii imekuwa ikiwaleta wataalam na wadau mbalimbali wenye uzoefu katika sekta ya Sanaa hivyo, kwa wasanii ambao wamekuwa wakihudhuria toka mwanzo wamepata mambo mengi ambayo yatawasaidia katika kukuza na kuendeleza vipaji vyao.

Alisisitiza kuwa, Sanaa inabadilika na kumezwa na teknolojia mpya zinazokuwa zinajitokeza hivyo, ni lazima wasanii wajenge utamaduni wa kutafuta maarifa mapya na kuwa wabunifu huku wakizingatia maadili ya kitanzania.

Kuhusu wasanii kulewa umaarufu na sifa, alishauri kuwa ni vema wakabadilika na kufanya kazi zao kwa bidii na ubunifu zaidi kwani, sifa ya msanii inakuja yenyewe kutokana na kazi anazozalisha na kupeleka kwa jamii inayomzunguka.

“Sifa ya mpishi hutolewa na mlaji, kwa hiyo wasanii wanapotengeneza kazi zao wasijisifu wenyewe bali wasubili kusifiwa na msikilizaji au mtazamaji” alishauri Mzee Jangala.

Alizungumzia pia suala la wasanii kutegemea vipaji tu pasipo kuingia darasani na kusema kuwa hilo haliwezi kukuza sekta ya sanaa na badala yake tutakuwa na kazi zinazoandaliwa kwa msukumo wa soko na si taaluma ya Sanaa

“Wasanii ni lazima watambue kuwa, mbolea ya kipaji chochote kile ni elimu. Ni vigumu sana kutegemea kipaji tu pasipo kukipalilia kwa taaluma ya sanaa husika”

Kwa upande wake, kaimu mwenyekiti wa Jukwaa la Sanaa, Vivian Nsao Shalua alishauri wasanii kulitumia Jukwaa la Sanaa ili kuzijua sheria, taratibu na mbinu mbalimbali zitakazo waongoza katika shughuli zao za Sanaa.

Wednesday, January 11, 2012

MAVAZI YA AIBU YALALAMIKIWA

Picha toka mtandaoni
imepakuliwa hapa https://www.youtube.com/watch?v=wxBwsU9u6vw
Picha kwa hisani ya google
                                                                                                                                                          
Wafaransa wana msemo wao, "L'habit ne fait pas le moine" unaotafsiriwa kwa kiingereza "Clothes don't make the man" ama kwa tafsiri ya Kiswahili isiyo rasmi, "si mavazi yanayofanya mtu kuwa mtu".



Hapo kale tumesoma katika historia ya kuwa wazazi wetu wa kale walijisitiri tu sehemu zao za utupu na kuwa hiyo ilikuwa ni namna yao ya maisha na hakukuwa na shida yoyote. Unaweza pia kuona katika filamu ya "the gods must be crazy " Mavazi ni kwaajili ya binadamu na si vinginevyo.

Hivi karibuni jamii zetu zimekuwa na muingiliano na jamii zingine na zimepiga hatua kubwa katika nyanja anuwai ikiwa ni pamoja na kwenye suala la mavazi. Binadamu ameona ni vyema akajivika mavazi yenye heshima na yenye kumpendeza.






Picha hii kwa hisani ya
blogu la haki za binadamu
Lakini muingiliano huo haukuishia tu kwenye mambo mazuri ya kujifunza kumekuwa na mambo yasiyo ya kupendeza kwa jamii. Kuna aina ya mavazi ambayo humuacha kiumbe akiwa karibu nusu uchi, ni kweli kwamba si mavazi yanayomfanya mtu kuwa mtu, lakini ni vyema kukubaliana na kile jamii inachotaka. Jamii ya leo Tanzania inahitaji mavazi yenye kusitiri vyema maungo, basi natufanye hivyo.

Kutoka Dodoma Mwandishi wa Tanzania Daima anaandika zaidi

BAADHI ya wakazi wa mji wa Dodoma wamesema kuwa wanakerwa na tabia ya baadhi ya wanafunzi wa kike wa vyuo vikuu wanaovalia mavazi ambayo yanaonyesha maungo yao na hivyo kuleta aibu kwa jamii.

Wakizungumza na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti, walisema kuwa tabia za wasomi hao haziendani na jinsi jamii inavyowachukulia kwani badala ya wao kuwa kioo kwa jamii wamegeuka kuwa chukizo.

Mmoja wa wakazi hao, Twaha Kivale, alisema kuwa kwa sasa mavazi ambayo yanavaliwa na wanavyuo hususan wa kike katika mkoa wa Dodoma ni ya aibu na yanaleta picha mbaya kwa wadogo wao wa elimu ya chini kama vile shule za msingi na sekondari.

“Tunategemea kuwaona wasomi wakiwa na tabia njema lakini cha kushangaza wasomi hao wanavaa nguo mbaya ambazo zinaonyesha maumbile yao ya ndani, hii ni sawa na kutembea uchi bila aibu tena mchana.

Tunashindwa kutofautisha wasomi na makahaba kutokana na mambo ambayo yanafanyika, kama kweli wasomi ambao tunawategemea kuongoza nchi wanavaa hivi kinyume kabisa na maadili yetu kuna maana gani ya kuelimika,” alihoji Kivalle.

Naye, mchungaji Evance Lucas wa Kanisa la EAGT, Siloam Ipagala, akizungumzia suala hilo alisema kuwa kitendo cha baadhi ya wanafunzi wa kike kuvaa nguo hizo ni mpango kamili wa shetani.

Alisema kuwa kwa sasa shetani anawatumia sana watu ambao wanaonekana kuwa wasomi na wasipoweza kujitambua ni wazi kuwa watajikuta wakishindwa kufikia malengo ambayo wameyakusidia.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi, katika hilo alisema kuwa hata yeye anakerwa na tabia hiyo ambayo kimsingi inadhalilisha utu wa mwanamke.

Dk. Nchimbi alisema pamoja na kuwa mji wa Dodoma una vyuo vikuu vingi na kuonekana kama sehemu ya maendeleo lakini kwa sasa hali ni mbaya kwani zimekuwepo tabia ambazo zinatia aibu katika jamii.

Hata hivyo alisema ili kuondokana na tabia hiyo kunatakiwa kuwepo kwa ushirikiano mkubwa kati ya viongozi wa dini na serikali ili kuhakikisha tabia ya namna hiyo inakomeshwa.

Naye mwanachuo mmoja wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) ambaye hakutaka kutaja jina lake, alipoulizwa alisema kuwa mavazi ni hiari ya mtu na kuongeza kuwa licha ya wananchi kulalamika bado wataona mambo mengi kwani kila mtu ana uhuru wa kuvaa atakavyo.

Kwa sasa katika mkoa wa Dodoma kuna vyuo vya elimu ya juu vya Udom, St.Johns, Chuo cha Mipango na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE).










Tuesday, January 10, 2012

BASATA YAONYA MAPROMOTA WABABAISHAJI

Na Mwandishi wa BASATA
Mkurugenzi Idara ya Ukuzaji Sanaa BASATA, Vivian Nsao Shalua
   akizungumza na wadau wa Sanaa katika Jukwa la Sanaa linalofanyika
kila wiki makao makuu ya Baraza hilo. Kulia ni Afisa Habari wa
BASATA Aristide Kwizela.


Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewaonya wakuzaji sanaa nchini kuacha mara moja ubabaishaji wanapokuwa wanaendesha matukio na matamasha mbalimbali ya Sanaa.

Onyo hilo limetolewa mapema wiki hii na Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Sanaa wa Baraza hilo, Vivian Nsao Shalua wakati akiongea na wadau wa Sanaa kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa inayofanyika kwenye ukumbi wa BASATA uliopo Ilala Sharifu Shamba.

Shalua alisema kuwa, Mapromota wamekuwa wakiwarubuni wasanii kwa kuwafanyisha kazi zisizo na mikataba huku wao wakinufaika na kuwaacha wasanii wakishindwa kujikwamua kimaisha.

“Utaratibu uliopo sasa kila mdau yeyote anapoandaa tamasha au tukio lolote linalohusisha wasanii lazima aje na mikataba na wasanii hao, aoneshe uwezo wake kifedha katika kuendesha tukio lakini pia awe na kamati inayoeleweka ya uendeshaji” alisisitiza Shalua.

Aidha, aliongeza kuwa, kumekuwa na ukiukwaji kanuni na taratibu za uendeshaji matukio hayo ambapo Baraza limekuwa likiwapa onyo na kuwafungia wahusika lakini akasisitiza kuwa, njia pekee ya kuepuka hali hii ni kwa mapromota kufuata taratibu zilizopo.

Akizungumzia kuhusu suala la mikataba, aliwataka Wasanii kuhakikisha hawashiriki tukio au onyesho bila kuwa na mkataba na waandaaji kwani hali hiyo inawafanya wadhulumiwe na kushindwa kudai haki zao kwa mujibu wa makubaliano.

“Ni lazima sasa wasanii wadai mikataba. Sisi tunawabana wakuzaji sanaa (mapromota) kuambatanisha mikataba yao kabla hatujawapa kibali lakini lazima na wasanii waoneshe wajibu wao kwa kudai mikataba na kutoshiriki maonyesho bila makubaliano ya maandishi” alionya Shalua.

Alisisitiza kuwa, Baraza litakuwa makini katika kufuatilia wadau wanaopewa vibali vya kuendesha matamasha na matukio mbalimbali ya Sanaa na mara taratibu na kanuni zitakapokiukwa halitasita kuchukua hatua za makusudi.

Wednesday, January 4, 2012

Masomo Zaidi...?

Elimu haina mwisho ndivyo usemavyo mmoja wa semi za wahenga wetu.
Kujiendeleza kielimu ni muhimu kabisa kwa wale wenye kupenda kufanya hivyo.

Mtandao wa Advance Africa lengo lao kuu ni kufanya hivyo; hebu sasa wale wenye moyo na nia ya kufanya hivyo wasome zaidi hapa. Bonyeza hapa

Mbinu za kazi tofauti malengo yaleyale - safi sana!


    

Sunday, January 1, 2012

MAISHA NI MALENGO

Leo ni mwanzo wa juma jipya, mwezi mpya, mwanzo wa miezi mipya kumi na mbili ama maarufu zaidi mwaka mpya.

Mwanzoni mwa mwaka ni kipindi kizuri kufanya tathmini ya kile tulichokuwa tukikifanya kama hatukufanya hivyo mwishoni mwa mwaka. Ama yaweza kuwa fursa ya kuweka malengo mapya ama kuyapitia yaliyotangulia kwaajili ya muda mpya unaoanza mbele yetu.

Kufanya tathmini ama kujiwekea malengo katika maisha ni suala la msingi mno kama tunataka kuishi katika namna inayoeleweka na yenye tija na mchango katika dunia yetu. Lengo la maisha kwa kila binadamu awe anafahamu ama la ni kuwa na furaha maishani. Aristotle, mwanafalsafa wa kale anasema hivyo pia; ili mtu awe na furaha basi hana budi kujiwekea malengo. Malengo huwekwa na watu wa kila kada.

Mwalimu shuleni hujiwekea malengo yake, mwanafunzi, mwanasiasa, mwanamichezo, mwanasanaa, mwanauchumi, msomi, mwanazuoni, mwanasheria, mkufunzi, mfanyabiashara, mkulima, mchungaji kanisani, shehe msikitini, imamu sinagogini, na kadhalika…watu wote makini wa kada zote hujiwekea malengo maishani. Kutokuwa na malengo maishani ni mithili ya muuza duka bila daftari, ambapo twajua mali bila daftari hupotea bila habari. Maisha bila malengo hupotea bila taarifa.

Kujiwekea malengo ni utamaduni ambao inafaa watu wote tuwe nao. Kwa kusema hivyo nafahamu fika kuwa kuna ndugu wasio na mazoea ya kufanya hivyo; watu hao mara nyingine hufananishwa na bendera fuata upepo hufuata chochote kitakachokuwa mbele yao. Bila ubishi si utaratibu mzuri wa maisha. Kwa wasio na utaratibu huo ni wakati sawia kuuanzisha.

Dini nyingi hutueleza kuwa hapa duniani ni sehemu tu ya mpito - twapita tu na kwamba makao yetu halisi yapo kwa muumba wetu. Hivyo wakati tukiandika malengo yetu ya maisha ni vyema tukamshirikisha huyo muumbaji kwa kuwa sisi hatujui siku wala saa ya kuyahama makazi ya hapa duniani, japokuwa hatutakiwi kuogopa kifo.

Unapoandaa malengo fanya hivi:

Kwa wanandoa, ama watarajiwa, wawashirikishe wenzi wao. Malengo haya si yako peke yako. Kwa hiyo nafsi ya kwanza ni Mwenyezi Mungu na pili ni mwenzi wako wa maisha; mkeo, mumeo ama mchumba wako. Muombe(ni) Mungu ili awaangazie kufanya malengo ya kweli.

Hatua ya pili ni kuwa mkweli na hali yako halisi; weka malengo ambayo yana uhalisia wa maisha yako. Mfano haina maana kwako mwanafunzi wa Tanzania kuwa na lengo la kuwa rais wa Pakstani miaka mitano ijayo. Weka malengo ambayo kwa kiasi fulani una nafasi ya kuyatekeleza. Mfano kusoma kozi ya Kifaransa kwa undani mara baada ya kumaliza masomo yako mwezi wa Juni.

Weka malengo yenye kukujenga na yatakayohitaji juhudi zako kuyatimiza.

Usiogope kuwa na malengo mengi bora tu ni muhimu katika makuzi na utu wako, mwisho wa muda wa kuyatimiza utakapowadia utakuwa na wasaa wa kujitathmini na kujua wapi ulihitaji ama utahitaji juhudi zaidi. Mara nyingine tukiwa na malengo mengi na yenye kudai juhudi zetu zaidi ndipo ambapo huwa na mafanikio zaidi maishani.

Usiwe mtu wa kujihurumia; kuona kuwa malengo haya ni mengi na magumu mno siwezi kuyatimiza. Usishindwe kujaribu, jaribu kutenda na ukishindwa wakati ukitenda ni tofauti kabisa na ukishindwa kujaribu kufanya chochote.

Jiamini na usijilaumu. Fanya utakachoweza kwa juhudi zako na mambo yakienda kombo, bila shaka utapata fursa nyingine ya kutenda tena!



Kila la heri na Mungu akubariki!

Mandalu
01/01/2012