Friday, November 11, 2011

Vazi la kitaifa na miaka 50 ya Uhuru Tanzania

 Mwanamitindo maarufu nchini Tanzania, Asia Idarous akipita jukwaani na mwanamitindo kuonyesha ubunifu wake katika ufunguzi wa Swahili Fashion week.

Picha kwa hisani ya blogu la michuzi








Umri wa miaka hamsini kwa binadamu si umri haba. Katika umri huo kwa hakika binadamu anaanza kuhesabu mengi aliyoyafanya; lugha yake inaanza kuwa ya wakati uliopita. Utamsikia nilipokuwa fulani, nilipokuwa na kina fulani, nilipokuwa sehemu fulani, nilifanya hivi, nilikuwa hivi... hata hivyo hiyo ni lugha hiyo ni watu tu wa sehemu fulani tu. Kuna wengine ambao husema miaka hamsini ndo kwanza maisha yanaanza na hivyo lugha zao ni zile za wakati ujao, nitafanya hiki, nitakuwa fulani... nita... nita... nita...

 Hata hivyo muhimu zaidi kwa Tanzani hivi sasa ni kuwa baada ya miaka 50 ya Uhuru wa taifa hili ambalo ni nyumbani kwa Serengeti,mlima Kilimanjarokreta ya Ngorongoro, nyumba kwa visiwa vya karafuu Zanzibar bado haina VAZI RASMI la kitaifa. Huu ni wakati kwa wanamitindo na wanasanaa kutumia ujuzi wao kutoa kinachoweza kuwa vazi la taifa na hivyo kuwasaidia watanzania kuwa na vazi lao la kujivunia lenye kubeba na kuheshimu tamaduni zetu. 




Thursday, November 3, 2011

KUMBE KWELI SISI SHAMBA LA BIBI...

Picha kwa hisani ya google
Moja ya makala za HabariLeo katika chapisho lake la leo, imetoa habari inayotufanya nchi yetu kuonekana kama shamba la bibi lisilo na mmiliki...

Bibi ni mama mzazi wa baba ama mama; ni mtu muhimu kwani, huyu pamoja na mumewe ama mwanaume flani ambaye tutamuita babu, ameshiriki moja kwa moja kuwaleta duniani wazazi wetu. Mtu huyu ki-umri amekula chumvi nyingi, na kitamaduni sehemu nyingi barani ni mahiri katika mambo mengi. Ujuzi na busara ya mambo ipo katika uzoefu wa siku nyingi.

Bibi ndiye aliyewalea baba na mama (kila mmoja na mzazi wake - wote waitwa bibi ); hivi basi kwa jinsi wazazi wetu walivyo na nidhamu na utaratibu wa maisha, sehemu flani wamevipata toka kwa bibi. Ni yeye hasa ndio aliyewalea na kupata watoto wenye maadili mema na staha kama tuwajuavyo wazazi wetu. Ni kweli kuwa hupata ujuzi mwingine kwenye mazingira waliokulia, mafunzo sehemu mbalimbali lakini nafasi ya bibi kwa maana ya mzazi na mlezi ni kubwa hasa. Hata hivyo kuna jambo jingine ambalo hushangaza sana toka kwa bibi.

Kina bibi wengi wanaelezewa kama watu wenye kuwadekeza kupindukia watoto wa watoto wao; wajukuu. Kiasi cha kuwadekeza huko, huwashangaza watoto wao yaani baba na mama zetu, ambao mara nyingine hulazimika hutoa simulizi za namna ambavyo bibi alivyokuwa mkali enzi za malezi yake kwao. Kuna sababu kadhaa zinazoeleza kwanini bibi anakuwa mpole na rafiki mno kwa wajukuu zake. Moja ya sababu hizo ni uzee, uchovu na upweke wa utu uzima. Bibi anawahitaji watoto wa watoto wake ambao kwake ni marafiki; ili kuwapata mara nyingi huweza kutumia rasilimali alizonazo kuwaweka kwenye himaya yake. Ni kupitia mwanya huo basi mali za bibi huweza kutumika vibaya; kuharibiwa, kuhujumiwa, kila mmoja akachukua anachotaka na tena kwa nafasi yake. Katika hili bibi hajali mali yake inaharibiwa kiasi gani, muhimu kwake ni kujenga mahusiano na wajukuu wake wakiharibu ama wasiharibu hilo si muhimu kwake muhimu ni kwamba uhusiano wa kirafiki na wajukuu unakuwa bora zaidi na zaidi. Ni kutokana na masuala hayo ndo analojia ya shamba la bibi ikazuka.

Habari Leo hivi leo wametoa taarifa yenye kufanana na analojia ya shamba la bibi. Hapa nchini, katikati ya kitovu cha uchumi wa nchi, Dar es Salaam kumekuwa na shule ikiendeshwa kinyume na sheria kwa miaka kumi na miwili. Hii inaweza kuwa kipande cha pande kubwa la “jabari” la barafu baharini. Si ajabu kuna mengi ambayo hayajagunduliwa na tena yenye madhara makubwa kwa taifa.  Nchi ina mali asili nyingi tena za kila namna; je ni namna gani rasilimali hizo zinaendeshwa katika namna inayowanufaisha wananchi walio wengi na taifa kwa ujumla wake.

Tanzania ina mbuga lukuki za wanyama pori, je shughuli za kiuchumi za wanyama pori zinafanyika kwa jinsi inayotakikana? Je, taifa linapata pato stahiki? Tanzania ina bahari, maziwa, mito na mabonde yenye uwezo wa kunufaisha taifa kwa namna anuwai; je watu waliokabidhiwa madaraka kuendesha vyanzo hivyo vya mapato wanaitendea haki jamii na taifa kwa ujumla? Je, shughuli hizo zinaendeshwa katika namna endelevu? Ili kwamba wajukukuu wa wajukuu wetu wakute mali hizo ama faida zake na wao pia wamudu kuendesha maisha yao kwa furaha? Tunaweza kuorodhesha utajiri na zawadi nyingi zilizopo nchini  hata hivyo si nia yangu kufanya hivyo lengo ni kukumbushana juu ya taifa letu na mustakabali wake.

Kuhitimisha tunasema kuwa kila mmoja wetu awajibike kizalendo ili kulinda na kutetea maslahi ya taifa letu la Tanzania, na kuboresha maisha ya jamii ya wanadamu wanaoishi sasa na wale watakao kuja baadaye kwa taratibu na sheria zinazokubalika.

Monday, October 31, 2011

KIBANGA AMPIGA MKOLONI

Na. Maisha na Mafanikio
Zamani za ukoloni, palitokea Mzungu mmoja. Mzungu huyo hakuwa mtu mwema. Alikuwa mkali na mkatili sana. Kwa ajili ya ukatili wake watu walimwita mkoloni. Wanancgi wote walimchukia sana popote pale alipokwenda.


Mzungu huyo alikuwa Bwana Shamba. Alikuwa na bakora iliyokuwa imetengenezwa kwa mkwaju. Kila alipokwenda kukagua mashamba, alikuwa na bakora hiyo mkononi. Alipendelea sana kuitwa "Bwana Mkubwa". Mkolono huyo alifurahia sana kupiga watu. Aliwapiga watu waliposhindwa kupalilia mashamba. Aliwapiga pamba yao ilipokuwa chafu. Aliwapa taabu sana.

Friday, October 28, 2011

Mtwara by Night

Mmoja wa mitaa ya mji wa Mtwara ukiwa ndani ya giza licha ya umeme wa uhakika mkoani humo- mipango miji wako wapi?

















Mkoa wa Mtwara ni moja kati ya mikoa michache nchini Tanzania isiyofahamu kadhia ya mgawo wa umeme. Mkoa haujaunganishwa kwenye mfumo mmoja wa taifa, hapa ni kwa faida ya wakazi wa Mtwara. Kwani hakuna maana kuwa chanzo cha umeme na usiupate umeme huo. Kwa Mtwara ni tofauti na maeneo yenye utajiri mkubwa ilihali watu wake hohehahe wa kutupwa.

Mkoani Mtwara kuna umeme utokanao na gesi asilia; gesi hii asilia inapatikana mkoni humu na hii inajidhihirisha kwa wakazi wa mkoani humo kwani hakuna mgao. Nafahamu kuwa hii ni hali ambayo wakazi wa mikoa mingi wangependa kuiishi. Na katika hali ya kawaida, ungetarajia kukutana na mitaa yenye kumulikwa vyema na taa nzuri za barabarani nyakati za usiku, lakini hali si hiyo. Nyakati za usiku mjini Mtwara kuna giza kubwa sawa sawa na mikoa yenye mgao wa nishati hiyo muhimu kwa maendeleo ya binadamu. Wazo kwa wahusika wakuu hususani wapanga maendeleo ya mji, wajipange na kuweka taa za barabarani katika mitaa ya mji huo wa kusini mwa nchi yetu ili kuupendezesha mji huo, kuongeza usalama wa mji na hivyo kuvutia wawekezaji wengi zaidi mjini humo.

Elimu kwa Maendeleo

Wanafunzi wa Stella Maris Mtwara University Collegge wakijisomea katika maktaba mpya ya chuo hicho.

Tuesday, October 18, 2011

WASANII WATOA ELIMU

Msanii wa Kundi la Orijino Komedi, Lucas Mhavile ‘Joti’ akisisitza jambo wakati akizungumzia Changamoto anazokumbana nazo kwenye Sanaa ya Vichekesho anayoifanya.


 
 
Picha na maelezo kwa hisani ya BASATA

BASATA NA HAKI ZA WASANII

Meneja Mzalishaji wa Kundi la Vichekesho la Orijino Komedi, Sekion David ‘Seki’ (aliyesimama) akiongea na wadau wa Jukwaa la Sanaa wiki kwenye Ukumbi wa BASATA.Wengine kutoka kulia ni Kaimu Mratibu wa Jukwaa hilo, Aristide Kwizela, Msanii Lucas Mhavile ‘Joti’ na Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari, BASATA Godfrey Mungereza.

Picha zote na maelezo kwa hisani ya mwandishi wa BASATA

BASATA YAWATAKA WASANII KUJITAMBUA

Na Mwandishi  BASATA
Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewataka wasanii kujitambua kwa kuwa na mipango ya muda mfupi na mrefu katika kazi zao na kutambua thamani yao.

Akizungumza wiki hii kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika makao makuu ya BASATA, Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari, Godfrey Mungereza alisema kuwa, kujitambua kwa msanii ni mwanzo wa kuipa kazi yake thamani kubwa kuliko ilivyo sasa ambapo wasanii wamekuwa wakikubali kulipwa malipo kidogo.

“Sanaa ni kazi, sanaa inalipa, ni lazima wasanii wawe na mipango ya muda mfupi na mrefu. Muhimu ni kwa wasanii kutambua thamani yao na kazi wanazozifanya. Ifike mahali wasanii watambue thamani yao ni nini” alieleza Mungereza...

Friday, October 14, 2011

Julius Kambarage NYERERE (1922-1999)







Huko Tanzania, Oktoba 14 ya kila mwaka imetangazwa kuwa siku mahususi ya kumkumbuka na kumuenzi Julius Kambarage Nyerere, maarufu zaidi, Mwalimu Nyerere, ni siku aliyofariki huko Uingereza mwaka 1999. Rais wa kwanza wa nchi hiyo, MwanaAfrika na mjengadunia halisi; mpigania uhuru wa nchi nyingi barani humo, mwanafalsafa, mwandishi, mzalendo, mcha Mungu na binadamu mwadilifu.

Mwalimu ni mmoja kati ya viongozi wachache wa kiafrika aliyekuwa kwenye mamlaka kwa muda mrefu. Alikuwa waziri mkuu wa kwanza wa Tanganyika mara tu baada ya kupata uhuru 1961  (1962 -1985) bila kujilimbikizia mali kama wafanyavyo viongozi wengi barani humo, mwalimu hakuwa mbinafsi. Alijitahidi kuishi vyema na kufuata misingi ya fikra za ujamaa na kujitegemea alizoziasisi.




Mwalimu pamoja na wenzake aliasisi Azimio la Arusha ambalo lilitoa maelekezo ya kuliongoza taifa ikiwa ni pamoja na maadili ya viongozi. Hii ilisaidia kuongoza nchi kwa uadilifu na ubadhilifu ulidhibitiwa kwa umakini, “Awamu ya kwanza rushwa ilikuwepo, lakini mtoa na mpokea rushwa wote walitiwa msukosuko mkubwa,… aliyebainika kupokea rushwa alicharazwa viboko 24, kumi na viwili kabla ya kwenda gerezani na kumi na viwili akimaliza kifungo chake ili akamwonyeshe mke wake…”

Julius Nyerere alikuwa na fikra binafsi ambazo aliziasisi, moja ya fikra hizo ni ile ya Ujamaa na kujitegemea. Katika nadharia hii Mwalimu alilenga kujenga taifa lenye uwezo wa kujipatia mahitaji yake lenyewe bila kutegemea sana mataifa ya ng’ambo. Mwalimu alijaribu kusimamia nadharia hiyo kwa mfano hata kama haikufanikiwa kama ambavyo angependa.

Zaidi Mwalimu aliwaunganisha watanzania wenye makabila zaidi ya miamoja na ishirini; wakati Tanganyika ikipata uhuru, kulikuwa na vijitaifa vingi, hivyo kazi aliyoifanya Mwalimu na viongozi wenzake ilikuwa ni kuunganisha mataifa hayo madogo madogo kuwa taifa moja kubwa. Kazi hiyo nzuri ilisaidia kuliepusha taifa hili la Tanganyika, na kisha muungano wa Tanganyika na Zanzibar 26. 04. 1964, Tanzania, toka kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe ambazo zimesambaa kote barani Afrika.

J.K Nyerere aliasisi mbio za Mwenge kwa tukio lenye hisia, kumbukumbu, na ujumbe mzuri hasa. Mwenge huo wa uhuru ulisimikwa kileleni mwa mlima mrefu kuliko yote barani Afrika; Kilimanjaro. Ni kapteni Alex Nyirenda wa jeshi la wananchi wa Tanganyika ndiye aliyefanya kazi hiyo nzuri. Akihutubia mjumuiko wa Umoja wa mataifa Mwalimu Nyerere alisema sisi tumeamua kuuwasha mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro ili umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete tumaini pale walipokata tama, heshima palipojaa dharau (si maneno halisi)…………Ni dhahiri kuwa makala hii ni fupi mno kumuelezea mmoja wa waasisi wa taifa tukufu la Tanzania. Hata hivyo jambo la msingi ni je, tunamuenzi  kwa kiasi gani Mwalimu Julius Nyerere?

Miaka kadhaa baada ya kifo cha Mwalimu, Tanzania inaendelea kumuenzi mzee huyu aliyefanya mambo mengi makubwa kwa taifa hili la Afrika Mashariki, lenye utajiri mkubwa japokuwa utajiri wake hauwafikii wote kwa usawa. Taifa linaendelea kumuenzi sana Mwalimu kwa sifa na sherehe zenye mbwembwe nyingi kote nchini. Lakini hatumuenzi Mwalimu kwa mambo ambayo yeye mwenyewe aliyataja kama muhimu kufikia maendeleo ya kweli ya watu. Kwani lengo kuu la kuongoza nchi ni kuleta maendeleo kwa wananchi; mwalimu alisema ili tuendelee tunahitaji mambo manne;

1. Watu,

2. Ardhi,

3. Siasa safi na

4. Uongozi bora

Ili nchi zetu ziweze kuendelea tunawahitaji watu wenye elimu nzuri, afya njema, chakula cha kutosha na mahitaji yao muhimu ya kila siku ili kushiriki katika ujenzi wa taifa lao, jamii ya wanadamu na dunia kwa ujumla wake. Lakini hivi leo watu wengi wa nchi hiyo bado hawana huduma za lazima kufikia wanapotaka kufika.
















Ardhi, ni chanzo cha vyakula vingi anavyotumia binadamu na ni sehemu ambapo shughuli za kijamii na kimaendeleo za binadamu hufanyikia. Hii leo hiyo yenye utajiri, rutuba na mengine muhimu wanapatiwa wananchi wachache wenye pesa nyingi na wageni wenye mapesa na ushawishi mkubwa.

Siasa safi na uongozi bora ni tunu muhimu na za lazima kwa maendeleo ya watu…tunu hizo zimepiga hatua kubwa kwa malengo nia ile ile ya kuleta maendeleo kwa watanzania. Hata hivyo bado kuna mapungufu katika nyanja hiyo ya siasa safi na uongozi bora; kwa hivi kuna haja ya kuendelea kufanya marekebisho kwenye suala hili la uongozi. Hivi leo huko Tanzania, siasa inaonekana kama ni ajira yenye kuleta kipato kikubwa kwa haraka, matokeo yake watu wengi wenye kutaka utajiri wa haraka haraka, ikiwa ni wasomi, wafanyabiashara, wakulima hukimbilia siasa hata kama hawana wito huo. Viongozi wengi hivi leo hawana maadili sahihi ya uongozi, wameingia siasa kwa malengo mbalimbali; wengine wameingia kulinda biashara zao, wengine kujiongezea heshima tu na kulinda malengo yao binafsi. Azimio la Arusha lilitoa mwongozo namna gani kiongozi aongoze watu wake. Siasa safi na uongozi bora ni muhimu mno kwa maendeleo ya kweli ya WATANZANIA WOTE! Hivyo lazima kuwe na namna flani ya Azimio la Kujenga maadili ya viongozi nchini!

Picha kwa hisani ya tovuti ya nyerere.info

Thursday, October 13, 2011

MUDA WA KUSAKA FIKRA ZAIDI


Mtaalamu wa burudani za mafunzo akiburudisha na kuelimisha wageni waalikwa siku ya hiyo ya ufunguzi wa mwaka wa masomo.

         MJ wa Mtwara hakukosa kwenye orodha ya waelimisha jamii wa siku                                      
   



                                                                                                                                                                
Burudani hii murua ilitufunza namna ya kupokea tofauti na vipaji vyetu na kuendelea kuishi kati jumuiya moja kwa upendo na mafanikio. Burudani nyingi zilitolewa na kundi hili maarufu la SAUT TRAVELLING GROUP (STG)




MUDA WA KUSAKA FIKRA ZAIDI

Picha kwa hisani ya blogu ya mdau Muliriye

Jumatatu ya 10.10.2011 ilitumika kufungua mwaka wa masomo Chuo Kikuu Cha Mtakatifu Agostino – Mtwara. Masomo ni njia ya kumwezesha mtu kugundua vipawa vyake na kuvitumia kwa malengo yale yale ya kuweza kuitawala dunia na vilivyomo humo ilikuboresha maisha ya jamii ya wanadamu.

Elimu ya Chuo Kikuu, kwa kutumia maneno ya Mwalimu Nyerere, ni elimu hasa yenye malengo ya kumfunza mtu kuwa na fikra bayana, kuwa na uhuru wa fikra, kuchanganua, na kutatua matatizo kwa kiwango cha juu kabisa, haya ni mawazo ya Mwalimu kwa maneno yangu. Kwa hivi basi elimu ya Chuo Kikuu imjenge kijana kuwa na fikra binafsi na tena zenye nia ya kuiendeleza jamii ya wanadamu.

Kumbe elimu hiyo ya juu haina lengo la kumfanya mwanafunzi akariri, lengo kuu ni kumfanya awe na uwezo wa kujenga fikra binafsi, zenye kuweza kuijenga jamii na awe na uwezo wa kuyatetea na kuyasimamia mawazo yake, kwa kufanya hivyo ndio tunaweza kupata wagunduzi (wavumbuzi), wanasayansi na watu waliotayari kuijenga dunia.

Huko SAUT Mtwara, shughuli za kuanza mwaka wa kuendeleza ujenzi wa fikra mpya ulianza kwa kuomba msaada wa Mwenyezi Mungu na kisha kufuatiwa na shughuli mbalimbali za kijamii.



Baadhi ya wageni mashuhuri wakielekea eneo la tukio


Wageni Maarufu na mashuhuri mno walikuwepo, hapa Profesa kijana akiwa na wadau wengine wakielekea eneo la tukio katika viwanja mahususi kwa tukio la siku

Hapo chini wadau wakiimba wimbo wa Taifa kabla ya kuanza shughuli yenyewe

Tuesday, October 11, 2011

Falsafa - kiwanda cha fikra!















Muhula wa mwaka mpya wa masomo wa vyuo vikuu nchini Tanzania kwa kawaida huwa ni miezi ya Septemba na Oktoba. Hii ni kwa sababu wanaojiunga na vyuo humaliza masomo yao ya elimu ya sekondari mwezi Februari, na kisha matokeo yao kutoka hufuata utaratibu maalumu kuomba nafasi ya kujiunga na vyuo vikuu nchini ambavyo idadi yake yazidi kuongezeka. Pamoja na vyuo vikuu nchini kuongezeka, bado vyuo hivyo haviwezi kuchukua idadi ya wanafunzi wote nchini wenye sifa za kujiunga na elimu hiyo ya kiwango cha juu. Vyuo kadhaa binafsi vinasaidia kwa kiasi kikubwa kutatua tatizo hili kwa kuanzisha matawi ya vyuo hivyo sehemu mbali mbali nchini. Kwa kiasi kikubwa hii inasaidia sana kuwapatia wanafunzi wengi fursa za kuendelea na masomo katika elimu ya juu.

Katika makala hii naangazia japo kwa ufupi tu tawi la Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino kilichopo mjini Mtwara. Chuo hiki ambacho kilianza kama kituo cha masomo cha "Saint Augustine University of Tanzania" (SAUT) kimepiga hatua sasa na kuwa "University College" hatua ya juu kuelekea kuwa na mamlaka binafsi. Chuo hiki kinafundisha programu ambazo hakuna sehemu nyingine hapa nchini. Moja ya programu hizo ni ile ya falsafa na elimu. Falsafa ni somo geni kwa wanafunzi wengi wa nchi zinazotumia kiingereza kama moja ya lugha zake rasmi, hususani za Afrika Mashariki, kwa nchi zinazotumia kifaransa, somo hili hufunzwa hata katika elimu ya sekondari.

Falsafa ni chimbuko kuu la mawazo; humjengea mtu nafasi ya kuwa na fikra binafsi ambazo anaweza kuzisimamia na kuzielezea bayana. Kwa mtazamo wangu binafsi, nchi zetu za Afrika, kupitia viongozi wake, zina haja ya kubuni mikakati na fikra binafsi za kiafrika ili kutatua matatizo yanayotusibu hapa barani. Falsafa inawapatia wanafunzi fursa ya kukutana na mawazo ya watu mbalimbali toka bara ulaya, bara Asia, Marekani, na pia barani Afrika; inafanya hivyo kwa lengo la kumpatia kijana fursa ya kujenga fikra zake binafsi. Wakati kijana anapata fursa ya kujenga mawazo binafsi, anafaidika pia na kwa kujifunza masuala ya maadili, jambo ambalo lazitatiza nchini nyingi barani Afrika, hususani tatizo la rushwa.

Wakati vijana wanaanza safari yao ya kujenga na kunoa bongo zao ni vyema wakajipanga kwa kusoma mambo ambayo yatainufaisha jamii nzima ya wanadamu na hivyo kuwa kweli wajenzi wa dunia; kila mmoja wetu ana nafasi ya kuwa mjenzi wa dunia hii kwa namna yake mwenyewe kulingana na vipaji alivyojaaliwa; akiongeza na kipawa cha falsafa mambo yatakuwa mazuri zaidi.


Picha kwa hisani ya google

Wednesday, October 5, 2011

Siku ya Walimu duniani












Picha zote katika makala hii ni kwa hisani ya google
Oktoba, 5 ni siku ya walimu duniani. Siku hii ambayo kimataifa imeanza kusheherekewa 1994, ina malengo hasa ya kuikumbusha jamii ya wanadamu kuwa walimu ni muhimu kwa maendeleo ya jamii zetu na kwa dunia kwa ujumla. Ni fursa nzuri kuwakumbuka walimu ambao wamechangia sisi wote kuwa hapa tulipo.

Walimu ndio chanzo cha mafanikio katika kila sekta, kila mtaalamu, katika hali ya kawaida, huhitaji mwalimu wa aina yoyote ile ili kujifunza, kuboresha alichonacho ama kujifunza zaidi na kuwa imara zaidi. Kwa hivi hata wale wenye vipawa maalumu bado ni lazima wapate maongozo ya namna flani. Kwahiyo kimantiki, mwalimu inatakiwa awe ni mtu mwenye uwezo mkubwa sana kiakili, uwezo mkubwa wa kuwafundisha wengine na si kinyume chake. Na zaidi tunahitaji walimu wengi ili kutoa ujuzi kwa watu wengi zaidi. Vigezo hivi muhimu vyatulazimisha watanzania kutafakari kwa kina mahitaji yetu ya walimu na ubora wao.















Kwa Tanzania, tunaungana na jamii ya kimataifa kusheherekea siku hii adhimu kwa jamii ya wanadamu. Ni muhimu kwa kuwa kila mmoja wetu ana mwalimu ama walimu wake ambao kamwe hawezi kuwasahau kwa jinsi walivyomsaidia na kumjenga kitaaluma, kiutu, kijamii na kadhalika.

Kama tulivyoona hapo juu, mwalimu ni mtu mwenye (anayepaswa kuwa na) mafunzo ama ujuzi maalumu kwaajili ya kuwafunza na kuwasaidia wengine. Mtu mwenye kufanya hizo inafaa awe na uwezo mkubwa wa kuelewa na kuwasilisha ujuzi huo kwa watu wengine. Ujuzi na uwezo wa mtu, kwa bahati mbaya sana, mpaka hivi sasa hupimwa kutumia vyeti alivyonazo. Vyeti hivyo huonesha matokeo ya mitihani mbalimbali ambayo mtu huyo alifanya; binafsi siamini njia hii ya namna ya kupima uwezo wa mtu, nakumbuka HakiElimu waliwahi kusema elimu sio cheti bali uwezo. Kurejea kwenye mada yetu, swali hapa ni je, walimu wetu Tanzania wana sifa zipi na ni namna gani huwapata?

Sina rejea sahihi kuhusiana na uwezo wa Mwalimu Julius Nyerere, ila simulizi za walimu wangu shuleni zinaonesha(hapa ni uvivu wa kufanya utafiti) kuwa alikuwa mwanafunzi hodari ndio maana akasomea ualimu. Mwalimu wangu darasani aliniambia kuwa huo ulikuwa ni utaratibu wa kikoloni kuwa wanafunzi wenye uwezo mkubwa darasani wanakwenda kusomeshwa ualimu ili wafundishe wengine. Utaratibu huu ulikuwa na mantiki na maana kubwa sana. Mtu anataka kuwa mwalimu awe ni yule aliyefaulu vyema sana katika masomo yake, kwa kutumia vyeti, tuchukue wanafunzi wenye daraja la kwanza na la pili.

Na kwa taaluma zingine, ambazo pia ni muhimu kama vile utabibu, uhandishi, sheria, wanasaikolojia n.k kuwe na utaratibu utakaofaa; wanafunzi wote wakifundishwa vyema na walimu wenye uwezo mkubwa basi madaraja yoyote kuanzia la kwanza hadi la tatu yanaweza kutoa wataalamu wenye sifa takikana kabisa. Kwa hali ilivyo hivi sasa baadhi ya watu hapa Tanzania waidharau taaluma ya ualimu, kiasi cha kushauri mwanafunzi aliyefanya vibaya mitihani kusomea ualimu. Sasa hii, si sawa, kwa kuwa mwanafunzi ambaye hana uwezo wa kutosha kuelewa inawezekana kabisa akawa na uwezo mdogo wa kuelewesha wengine. Kwa hivi basi kuna haja ya kuangalia kwa makini namna tunavyowapata walimu wetu wa baadaye ili kupata  kuwa na uhakika wa kupata wanataalamu wa fani zingine waliofunzwa na walimu wenye ujuzi na uwezo wa kufaa kuwapatia elimu hitajika. Kinyume na hapo tutapata wataalamu wasioiva sawasawa ni muhimu sana.

Ili wanafunzi wanaofanya vyema waweze kwenda kusomea ualimu na kufunza ni muhimu wakapatiwa motisha ili kuwahamasisha. Ni muhimu kufanya hivyo kuwa kila binadamu ana uhuru wa kufanya aonavyo muhimu ili mradi tu hadhuru ama haathiri haki za wengine. Kuwe na utaratibu na sheria ya namna ya kuwafanya wanafunzi waliofanya vyema zaidi kwenda kusomea ualimu. Hiyo inaweza kuwa moja ya malengo ya kimaendeleo ya taifa hasa wakati huu ambapo hapa nchini kuna shule nyingi kama zilivyo kata. Ili kuepuka kuendelea kuwa na takwimu kubwa ya shule bila ubora stahiki basi hilo tuliangalie.
Shule ya Tusiime Picha na google












Sifa stahiki za walimu zinatupeleka kwenye sifa stahiki pia kwa shule zetu. Serikali ya Tanzania imepiga hatua kubwa kwenye sekta ya elimu, japokuwa, bado kuna mengi yanatakiwa kufanyika. Kuwa na shule kila kata ni hatua nzuri mno ya kimaendeleo, lakini aina gani ya shule ni muhimu zaidi kwa kuwa shule inaweza kuwa ni ukombozi ama utumwa. Mwanafunzi aliyefunzwa vyema yeye na jamii yote ya wanadamu itakuwa imekombolewa ilhali yule asiyefunzwa barabara atakuwa mzigo mkubwa kwa jamii; kwa vile atatazamwa kama aliyekombolewa na elimu. Mtu aliepata elimu katika mazingira duni ya kitaaluma ni mtu aliyeelimika nusunusu, mtu mwenye elimu nusunusu ni hatari kweli katika jamii kwani anaweza kuutumia, ashalkumu si matusi, umbumbumbu wake kuleta madhara akidhani kuwa anatoa msaada kwa jamii. Kwa hiyo wito hapa ni kuboresha walimu na mazingira yao ili wafanye kazi kwa uzuri na hivyo kuwa chachu kwa maendeleo ya taifa lote.

Thursday, September 29, 2011

Vijana wa CCM na CHADEMA


Picha kwa hisani ya mmiliki-Mtwara















Hawa ni vijana na wanafunzi; wataalamu wa leo na baadaye. Wana uwezo na nguvu nyingi zinazo hitaji kuelekwezwa sehemu sahihi kinyume na hapo ni maafa. Vijana kwa asili yao ni watu motomoto. Wana nguvu na hazina nyingi miilini na akilini mwao ambayo wanahitaji kuvifanyia kazi ili nguvu hizo ziwe na manufaa kwa jamii ya wanadamu.

Ili waweze kufanikiwa kuzitumia nguvu zao vyema ni lazima wapatiwe mafunzo ili watambue namna ya kuzigundua na kuzitumia vyema nguvu hizo; leo hii kuna AZAKI nyingi zinazotoa STADI ZA MAISHA kwa vijana.


Hilo ni jambo jema kwani bila kufanya hivyo huweza kuzitumia nguvu hizo vibaya. Wakitokea waharibifu wachache wenye kutambua vyema nguvu nyingi walizonazo vijana, huweza kuwaharibia kabisa  malengo yao ya maisha bila huruma. Hivi leo hapa Tanzania kwa sababu kadha wa kadha, baadhi ya vijana wanaingia kwenye Siasa kwa malengo ya kusaka ajira; siasa kwao ni ajira. Siasa, na hasa Siasa Safi (JK.Nyerere) ni muhimu na lazima kwa maendeleo ya watu. Lakini siasa isipokuwa safi ndipo hapo utasikia vijana wamefanya vurugu zilizohamasishwa na itikadi za kisiasa. Bila kuvurugwa na makundi ya wabinafsi wachache wenye kulenga kujinufaisha kupitia nguvu kazi na akili ya vijana, kundi la vijana ni hazina kuu kwa taifa lolote duniani, na halina haja ya fujo.Hayo yamedhihirishwa na makala hii ya Habari Leo: Vijana Chadema, CCM hawataki vurugu Igunga


MWANAFUNZI BORA


                                          Imepakuliwa hapa :https://www.youtube.com/watch?v=Y1JhL9FTA8Y                
Hapo juu wanafunzi wa moja ya shule za msingi hapa Tanzania. Mwanzo kabisa wa safari ndefu ya miaka kadhaa... wana mahitaji mengi kufanikisha ndoto zao.

Mwanzoni mwa mwaka huu shirika binafsi la HakiElimu lilitoa shindano la kuandika sifa za mwanafunzi bora. Shindano lilimtaka mshiriki aandike insha ama achore picha juu ya mada hiyo. Hatimaye hivi leo mshindi amepatika; unaweza kusoma mada hiyo kwenye Habari Leo Hapa  chini ni moja ya insha zilizoshiriki shindano hilo:

Mada hii ni muhimu kwa kuwa ni mwanzo wa maendeleo ya nchi yoyote duniani. Mwanafunzi mwenye sifa bora hufanya vyema katika masomo yake na kupata ujuzi wa aina fulani wenye manufaa kwa nchi. Mwanafunzi mwenye sifa bora hufaulu vyema masomo yake na kufaulu kwake ni lulu kwa nchi kwani kupitia ujuzi na weledi wake katifa fani aliyonayo huchangia katika maendeleo ya taifa lake.

Mwanafunzi ni mtu anayetafuta elimu ama maarifa fulani . Kwa kawaida mtu huanza kupata elimu toka utotoni. Ni vyema ikawa hivyo kwa kuwa mtoto anapokuwa mdogo ana uwezo mkubwa kwa maana ya wepesi wa kujifunza na kuelewa mambo mengi mapya kwa urahisi zaidi. Wakati wa umri mdogo mtoto anahitaji uangalizi wa karibu kabisa wa mzazi/ mlezi wake. Uangalizi huo ni vyema ukaangalia pia suala kujifunza kwa mtoto. Hivyo kujifunza kwa mwanafunzi wakati angali na umri mdogo ina maana kuwa huwahusisha pamoja naye mwenyewe, mwalimu, mzazi/mlezi, na familia yote kwa ujumla wake. Pamoja na hayo yote kuna vigezo na mazingira ambayo ni muhimu kwa mwanafunzi kuweza kutafuta maarifa kwa usahihi zaidi.

Ili mwanafunzi aweze kufanya vyema katika masomo yake na hivyo kuweza kuchangia katika maendeleo ya taifa lake na ya jamii yote ya wanadamu kwa ujumla wake, mara baada ya kupata ujuzi, ni lazima awe na sifa kadhaa. Sifa za mwanafunzi bora ndio hasa mada ya insha hii. Mwanafunzi bora anatakiwa awe na aina mbili ya sifa. Awe na sifa za ndani na za nje; nitazielezea kwa unagaubaga hapa chini.

Sifa za ndani ni za kimaumbile, hizi ni zile ambazo binadamu anazaliwa nazo. Hafanyi chochote kuzipata ni zawadi ya uumbaji na ni sifa za lazima kabisa; nazo ni akili na utashi. Akili ni ule uwezo wa kupokea, kuzisoma na kuzitafsiri taarifa zote toka nje ya mwili wa binadamu. Utashi ni ule uwezo wa binadamu kuamua kufanya jambo moja ama jingine baada ya utashi huo kupewa na akili taarifa zote zihusianazo na jambo fulani kabla ya kulifanyia maamuzi. Akili inampatia mwanafunzi uwezo wa kujifunza mambo mapya na kuyatunza kama ujuzi; hivyo ni jukumu la mwanafunzi, kupitia utashi, kuamua kujifunza. Sifa hiyo inatufikisha kwenye utashi; kazi ya utashi ni kuamua kufanya hili ama lile kisha kupewa taarifa zote muhimu. Hivyo basi, kwa sifa hii, mwanafunzi ana hiari ya ama kujifunza ama kutojifunza.

Sifa za nje za mwanafunzi bora ni usikivu, udadisi, heshima na matumizi sahihi ya ujuzi alioupata. Kijana wa kike ama wa kiume ili aweze kujifunza vyema hana budi kuwa msikivu. Asikilize kwa makini maagizo ya mzazi/mlezi nyumbani, mafunzo ya mwalimu shuleni na ni vyema pia milango yake yote ya fahamu ikawa na usikivu ili maarifa mapya yapatikane. Picha ya mtu mwenye masikio makubwa inaweza kuwakilisha twasira ya mwanafunzi mwenye usikivu.

Udadisi; hali ya kutafuta jambo kwa kuulizauliza . Kwa hakika hii ni sifa muhimu kwa mwanafunzi bora. Pamoja na kufundishwa na mzazi/mlezi nyumbani na mwalimu darasani, mwanafunzi mwenyewe inamlazimu ajifunze kutafuta elimu, mambo mbalimbali juu ya mafunzo yake bila ya kuwa tegemezi kwa mwalimu tu. Mwanafunzi mdadisi anaweza kuomba na kujiunga uanachama katika maktaba mahalia kwa lengo la kusaka mambo mbalimbali kwa kina zaidi.

Heshima, thamani ya utu, adabu ; hii ni sifa nyingine muhimu kwa mwanafunzi bora. Sifa hii humfanya mwanafunzi awe mwenye mahusiano mazuri na wazazi /walezi na walimu wake. Mahusiano mazuri ni kigezo na kichocheo cha muhimu cha udadisi na kujifunza. Mwanafunzi mwenye mahusiano mema na mwalimu wake hana hofu kuuuliza ama kutoa maoni yake juu ya mada fulani darasani.

Matumizi sahihi ya ujuzi alioupata. Mwanafunzi bora, si yule mwenyekukariri kila afundishwacho na kwa kurudia aliyoweka kichwani hupata alama nzuri katika mitihani, bali ni yule mwenye uwezo wa kutafsiri nadharia na masomo yake kwenda kwenye vitendo halisi. Mfano, kwenye somo la Sayansi kimu, mwanafunzi anajifunza juu ya utunzaji wa vyakula; swala hilo anaweza kulifanya kuwa kitendo halisi kwa kuwashirikisha wazazi wake kama simulizi inayoweza kufanyiwa kazi na hivyo kuipatia familia mbinu ya kuhifadhi chakula.

Kuhitimisha insha hii; wazazi/walezi na walimu wao pia wana majukumu makubwa juu ya wanafunzi wao. Kubwa na muhimu zaidi ni kuwajengea mazingira ya kujifunza na kuwatia shime ili wawe na hamu ya kuzitumikisha sifa zote za ndani na za nje. Akili, utashi wa kujifunza, usikivu, udadisi, heshima na matumizi sahihi ya ujuzi mpya ni sifa za mwanafunzi bora. Sifa hizi huleta matokeo mazuri mno pale zinapopatiwa mazingira na fursa sahihi na hiyo huweza kudhihirisha uwezo wa mwanafunzi bora.

Thursday, September 15, 2011

Chanzo cha Mapato kwa Wananchi

Hii ni sehemu ya soko la Samaki mkoani Mtwara.
Hapa ni sehemu samaki wanapochuuzwa mara  baada ya kuvuliwa.



Biashara ya samaki ni moja kati ya maeno yenye kutoa ajira kwa wananchi wengi wa kawaida hususan kina mama. Hii ni shughuli ambayo huwapatia wananchi wengi pesa za kuweza kuendesha maisha yao na pia huweza kuchangia pato la taifa kwa kulipa kodi hata kama ni kiasi kidogo.

Hivi karibuni nilitembelea soko hilo kujionea jinsi lilivyo na kuangalia uwezekano wa kujipatia kitowewo. Hali niliyoikuta sokoni hapo si ya kuridhisha sana. Soko la bidhaa hiyo muhimu kwa afya ya binadamu si nzuri kiafya. Hata hivyo nilipouliza kidogo wachuuzi sokoni hapo niliambiwa kuwa kuna mikakati na ujenzi wa soko la kisasa tayari umekwishaanza. Hivyo kuna matumaini ya kupata sehemu nzuri zaidi siku za usoni.

Hii ni sehemu ya muendelezo wa soko letu la samaki mjini Mtwara, wahusika wameliona na hivyo wanaendelea kuliboresha...



Bila shaka mazingira safi ni muhimu kwa akili safi... ni muhimu marekebisho yafanyike haraka... bila shaka tutahitaji soko la kisasa kama pale Magogoni...

Wednesday, September 14, 2011

Clouds Fm hongereni lakini...


Hiki ni kivuko kinachotoka Mtwara kwenda Msanga Mkuu.
Picha inaonekana kwa mbali kiasi; vitu unavyoona vya rangi ya pinki vikipepea ni maboya ya kuokoa maisha. Unaonaje yavaliwe wakati gani?

Kituo cha redio (Mawingu) Clouds Fm cha jijini Dar es Salaam, kimeanzisha mkakati wa kuchangia ununuzi wa maboya ya kuoa maisha-mkakati huo umepewa jina la "OKOA MAISHA"  Maboya hayo "life jackets" hutumika kuokoa maisha ya abiria endapo ajali ya majini itatokea. Maboya hayo huvaliwa na abiria kwenye ndege-ili kwamba chombo hicho kikiangukia majini, husaidia kuoa maisha ya abiria, vazi hilo hutakiwa kuwepo pia kwa chombo chenye kusafirisha abiria majini. Clounds wanapiga la mgambo ili kusaidia wasafiri majini. Kwa hili binafsi nawapongeza sana. Hata hivyo kuna mambo mawili hapa ya kutafakari si tu wa mpiga mwano huu bali ni kwa watanzania wote.

Mosi, binafsi natambua kuwa kwenye ndege maboya hayo, kwa kawaida, huwatosha abiria wote; kila abiria anakuwa na life jacket chini ya kitivchake. Na hivyo kikitokea kile ambacho katu hakitamaniki, bali kila abiria hupata kutumia boya lake. Nimesafiri mara mbili kwa maji toka Dar es Salaam kwenda Zanzibar, binafsi sikumbuki “boya langu” lilikuwa wapi. Kwa kusema hivi sina uhakika je, kila abiria kwenye vyombo vya maji hapa Tanzania, ana uhakika wa kupata boya lake ama, je idadi ya maboya inalingana na idadi ya abiria chomboni?

Swala la pili ni juu ya muda wa kuvaa boya hilo. Nilipokuwa mwanafunzi kule Uganda, nilipata nafasi ya kutembelea wafungwa kwenye gereza lililo kisiwani katika mji wa Jinja. Kwenda gerezani, chuo nilichosoma kiliweka utaratibu wa kila mwanafunzi kuvaa boya lake pale anapokuwa chomboni. Hi ili wanafunzi wasafiri kwa usalama na uhakika zaidi. Tunaweza kuanzisha utaratibu kama huo pia, kila abiria avae boya “life jacket” pale tu anapoingia chomboni. Najua utaratibu huu utazua hofu kwa abiria na wamiliki wa chombo.

Abiria, akivaa boya la kuokoa maisha, atajihisi kama anaingia kwenye ajali moja kwa moja na ataona kama anajiombea dua baya kwa kufanya hivyo. Mmiliki wa chombo atahisi kuwa abiria wataondoka ya maboya yake na safari inayofuata hakutakuwa na boya hata moja. Tukitaka kufanikiwa lazima tubadilishe tamaduni zinazobadilika.

Tuvae maboya mara tunapoanza safari majini; kwa kufanya hivyo ndo tutakuwa tunajali maisha hofu za kimazingaombwe kamwe haziwezi kutusaidia. Mmiliki wa chombo majini, aweke utaratibu wa kukusanya maboya mwisho wa safari; kila aingiaye chomboni apate boya na kila anapotelemka akabidhi, kama hana alipe gharama ya boya hilo hata kama hakuvaa. Kuokoa maisha ni lazima tuwe wabunifu, makini lakini pia wakali kwenye utekelezaji. Utaratibu huu kwa kiasi fulani unafanyika pale kituo cha mabasi, Ubungo, Dar es Salaam.(Kukagua abiria kama wamefunga mikanda)

Mandalu

Uzembe ukipungua ajali pia zitapungua !

Google Image
                                          Inapakiwa hapa https://www.youtube.com/watch?v=MpzE7flW9_A
Wakati tukiendelea na tafakari juu ya ajali ya meli kule Nungwi ni wasaa mwafaka kwa watanzania na wanadamu wote kwa ujumla na hasa wenye kutumia vyombo mbalimbali kusafirisha binadamu wennzao, iwe ni vya ardhini, majini ama angani, kuwa waangalifu zaidi. Ajali ya meli ya abiria LCT Spice Islanders, iliyokuwa ikitoka Unguja kwenda Pemba, imesababisha vifo vya ndugu zetu wengi. Ni msiba mkubwa kuona watu wengi wenye afya njema na ambao ni  nguvu kazi muhimu kwa ujenzi wa Taifa, wakiaga dunia.Tunamwomba Mwenyezi Mungu kwa huruma yake awapokee ndugu hawa kwenye makazi ya kudumu, na wafiwa na wajeruhi wote wapate faraja na kupona haraka! Kutokana na tukio hili serikali na wananchi wote kwa ujumla wetu tunapenda kuona wamiliki vyombo vya kusafirishia abiria, mamlaka za kudhibiti vyombo vya usafiri na wasafiri wenyewe wakiongeza umakini...

Tuesday, September 13, 2011

Vijana na Mabadiliko

Makala ya Mwandishi Ahmed Rajab; Vijana wa Afrika wanawaperemba tu viongozi... imejaa mambo anuai ambayo yana manufaa mengi kwa kijana mwenye malengo ya kuchangia katika jamii yake.

Mwandishi anaongelea mwamko mpya wa vijana barani Afrika katika kudai haki za jamii zao, aidha anatoa picha ya jinsi viongozi wabadhilifu wanavyo tumia vibaya mali za umma kwa manufaa binafsi.

Monday, September 12, 2011

Tandahimba Pia


















Sekondari ya Milongodi ilikuwa na walimu wetu pia. Hapa mkuu msaidizi wa shule hiyo akitushirikisha jambo kuhusu sekondari hiyo ambayo ingali ikikuwa kabisa.

Katika shule hii kidato kimoja kina wanafunzi wa kiume tu bila binti hata mmoja, Zaidi ya hayo walimu, kama ilivyo katika shule nyingine nyingi, ni wachache mno. Kwahiyo, walimu mafunzoni ilikuwa ni ukombozi mkubwa kwa shule nyingi za wilayani Newaala na Tandahimba, mkoani Mtwara. Pengine muda wa mazoezi uongezwe, ili huduma hiyo iendelee kwa muda mrefu zaidi? Tutawauliza walimu hawa mafunzoni.

Walimu mafunzoni

Nilipata fursa ya kukutana na walimu-mafunzo
sekondari ya kutwa Newala mjini

Alaa kumbe ni NEWALA !














Hapa nikijiandaa kuanza safari asubuhi na mapema- mjini Newala! Picha na Eric Wamalwa

Nipo wilayani Newala. Hii ndo wilaya ya kwanza kuandikishwa hapa Tanzania, ni moja ya wilaya tano za mkoa wa Mtwara. Wilaya hii, kama jinsi ilivyo kwa maeneo mengine, ina mahitaji ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kuna makundi yote ya lazima katika jamii; watu wazima, vijana, na watoto.

Kijamii; maji ni shida (jamii imejenga utamaduni wa kuvuna maji ya mvua: karibu kila familia ina mikingio maji kwaajili hiyo – huu ni utamaduni wa kuigwa hasa na sehemu zenye mvua za kutosha. Maji hayo ya akiba yaweza kuwa na matumizi kedekede. Mfano kumwagilia bustani za mboga mboga, kuanzisha mabwawa ya samaki n.k )

Elimu: wilaya ina shule kadha wa kadha; karibu kila kata ina shule yake. Hili ni moja ya mambo mazuri ya serikali iliyopo madarakani. Ni vyema kuwa na shule za kuweza kuandikisha wanafunzi wengi iwezekanavyo. Vijana wengi wakiandikishwa shule za sekondari ndo hasa mwanzo mzuri na wa uhakika wa kupiga vita umasikini kwa vitendo. Hata hivyo mtaala wa elimu uzingatie mfumo wenye vitendo zaidi kuliko nadharia kama ilivyo hivi sasa. Vijana wetu wengi wakimalima masomo yao, kwa mfumo tulio nao hivi sasa, hulazimika kusubiri ajira. Mfumo unaofaa ni ule wa kumuandaa kijana ili aweze kujiajiri; hilo hasa ndo liwe lengo la elimu yetu. Tukirejea mada yetu; shule nyingi huko Newala zina watenda kazi wachache sana.

Shule kadhaa zina walimu wawili, watano, sita, nyingi zina idadi isiyozidi walimu kumi. Hii ni changamoto kuu na kubwa mno katika sekta ya elimu. Wanafunzi wanapokuwa na walimu wa kutosha ndo inawarahisishia kujifunza kwa ufanisi zaidi. Kwa walimu wakiwa na wanafunzi kiasi, kwao inakuwa ni vyema zaidi katika utendaji kazi wao.

Ukosefu nyumba za walimu; shule nyingi za kata zipo vijijini hasa, ni sawa kwani huko ndiko wanapoishi wananchi na watanzania wengi zaidi. na vijiji vyetu vingi havina huduma kwa wageni hususani nyumba za kulala wageni. Ukosefu nyumba za kulala wageni vijijini unakwamisha hata wakaguzi na wataalamu wa kada zingine kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi. Shule nyingi hizi za kata ama hazina nyumba za kutosha kwa walimu ama hazina kabisa nyumba hizo. Ni kweli walimu waliopo katika shule hizo ni wachache pengine inajieleza sawa pia kutokuwa na nyumba kwa walimu. Kuwa na nyumba za ziada kwa walimu inaweza kuwa ni fursa ya kuwavutia walimu wageni, ambao wengi wafikapo kujitambulisha na kuona mazingira ya shule hugoma kurejea shuleni huko.

Kisiasa: Newala ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hivyo huko pia kuna mfumo wa vyama vingi vya kisiasa lakini wakazi wa huko wanaishi kwa amani na undugu. Hata hivyo hii ni tathmini yangu ya juma moja tu.

Kiuchumi: zao la korosho ni uti wa mgogo wa uchumi wa wilaya hiyo; wakazi wengi hujihusisha na kilimo cha zao hilo la msimu na lenye kuhitaji matunzo ya karibu hasa. Kwa wananchi wanaoweza kufuata vyema maelekezo ya wataalamu wa kilimo hujipatia mavuno na pesa nzuri kutokana na kilimo cha zao hilo. Hata hivyo mkulima siku zote huchukua tu bei inayopangwa sokoni na watu wengine; yeye hufanya kazi ngumu ya kutunza shamba na kufuatilia ukuazi wa korosho hadi kuwa tayari na kisha hapo watu wengine wenye “utu” zaidi ya mkulima hukaa meza na kupanga bei ya zao hilo kama ilivyo kwa mazao mengine ya wakulima wetu maskini hapa Tanzania na sehemu nyingi nyingine barani Afrika. Siku moja tufikie hatua ya kupanga bei ya mazao yetu wenye kwenye hilo soko la dunia; hii ni mantiki zaidi kwa kuwa wakulima wetu ndio wanafahamu haswa gharama za kilimo.

Ajira za vijana: Vijana kundi lenye nguvu na msukumo mkubwa wa maendeleo ya wakati uliopo na ujao katika jamii. Nikiongea na vijana kadhaa wa mjini Newala niligundua kuwa kuna idadi kubwa ya vijana wa kitanzania wanofanya shughuli za kiuchumi, hususan biashara nchini Msumbiji. Newala ni wilaya ya mpakani kabisa na Msumbiji. Upande wa kaskazini ya Msumbiji haujapiga hatua kubwa kimaendeleo na hivyo kutoa fursa nyingi kwa watafuta mali: hivyo vijana wetu hupitia huko na kufanya biashara za bidhaa anuwai. Vijana niliongea nao, wanijuza kuwa vijana hao wa kitanzania huko, hususani wale wenye bidii ya shughuli zao, ni wenye mafanikio makubwa.

Nyumba za kulala wageni chache: wilaya hii ina nyumba chache za kulala wageni. Upungufu huo hivyo unatoa fursa za kiuchumi kwa wananchi kujiimarisha kiuchumi na hivyo kujiongezea pato na pia kuongeza pato la taifa kwa ujumla.Kuna changamoto lakini pia fursa anuwi za kujiimarisha kiuchumi, kujiondoa kwenye umasikini na kuchangia kwa pato jumla la taifa.



Tuesday, August 23, 2011


Baadhi ya wadau wa Vijana tukisimama kwa picha ya pamoja

Wadu wa Vijana

Hapa ni Moro nikiwa na wadau wa vijana.
Hawa ni wadau toka mikoa mbalimbali waliokutana kujadili masuala ya afya ya uzazi na maendeleo ya vijana kwa ujumla.

Picha kwa hisani ya kiongozi wa mradi wa masuala ya vijana wa fhi









Saturday, August 20, 2011

Vijana Maji Moto

Picha kwa Hisani ya mtandao
Hivi karibuni tumeshuhudia harakati kubwa za vijana sehemu mbalimbali duniani. Harakati hizo zimekuwa na dhima na vyanzo tofauti tofauti. Harakati za vijana mashariki ya kati na Afrika kaskazini zilisababishwa na kukosa mahitaji yao muhimu hususani kukosa nafasi za kazi na kutokuwa na uhakika wa mustakabali wa maisha yao. Giza hilo kwa mustakabali wa maisha ya vijana ulisababishwa na ubinafsi wa viongozi wa nchi hizo. Kiongozi wa Tunisia, Ben Ali amekuwa madarakani kwa muda mrefu na amejikusanyia mali nyingi mno na hivyo kuharibu matumaini ya vijana na wananchi wake kwa ujumla. Hali kadhalika, Misri, Libya, Yemen na kwingineko mashariki ya kati.

Vijana wa Uingereza wao nao walisababisha fujo ama varangati (Kiswahili cha kizamani) lakini wao sababu ilikuwa tofauti. Makala ya mwandishi kutoka London Macha, inatoa sababu ambazo zinawapambanua vijana wa Uingereza na wale wa Mashariki ya kati. Wachambuzi wengine husema kuwa vijana wa dola hiyo kuu zamani, wanafundishwa tu/ ama zaidi juu ya haki zao, hawafahamu kuhusu wajibu wao kwa jamii. Hili ni tatizo kubwa. Vijana wanapokua ni vyema tukawajuza haki zao, lakini muhimu kabisa watambue pia namna ya kuwajibika kwa jamii zao. Hili ni jambo la kila mahali Tanzania na nchi nyingine zote duniani, na tena muhimu kwa wananchi na pia serikali kutoa mchango wo kwa maendeleo ya vijana.

Tanzania kuna asasi zisizo za kiserikali (AZAKI) lukuki zinazojihusisha na masuala ya vijana. AZAKI hizo zimeanzishwa na wananchi kwa malengo lukuki, ikiwa ni pamoja na kuwahudumia vijana. Hili ni jambo jema kwani vijana ni moja ya makundi yaliyo muhimu kwa maendeleo ya jamii ya wanadamu. Hata hivyo katika siku za nyuma kidogo kulizuka AZAKI nyingi ambazo hazikujali masilahi ya walengwa husika bali waanzilishi kujijaza mapesa.

Serikali yetu Tanzania, imepiga hatua kubwa hasa kwa kuwa na utashi muhimu wa kisiasa na kuazisha shule za sekondari kila kata. Bila ubishi hii ni hatua kubwa sana ya kuelekea maendeleo ya kweli. Elimu mwanzo wa ustaarabu wote duniani; elimu kwa upana wake si tu ile ya darasani. Hata hivyo changamoto kubwa kwa serikali ya Tanzania na wananchi wake kwa ujumla wao ni kuziboresha shule hizo lukuki za kata. Ni muhimu kufanya hivyo kinyume na hapo tunapata taifa la watu walioelimika nusu nusu. Hii elimu nusu ni hatari sana, pengine afadhali asiyeipata kabisa; mwenye elimu nusu hatokubalika katika kundi la wajinga kabisa kwani ana maarifa kiasi na hivyo kuwa tofauti na wasiosoma kabisa, lakini hawezi changamana pia na walioiva vilivyo kielimu kwake itakuwa ni kujinyanyapaa – “kujichora” (maarufu kwa vijana) mbele ya wasomi. Ni hatari kama nusu wasomi hawa watakuwa wengi; watadai haki kwa njia zisizokubalika kwani elimu yao yawatuma hivyo.

Hivyo AZAKI zilenge kuwasaidia vijana wapate stahili yao. Wananchi wote kwa ujumla na serikali kwa maana ya dola tujipange kuziboresha shule hizi haraka iwezekanavyo kama inavyoelezewa kwenye MKUKUTA II ili kuepukana na nusu wasomi na matatizo mengi toka kwa vijana wetu siku zijazo.

Wednesday, August 3, 2011

Familia Inafaa - Families Matter Program! FMP

Hapa nikiwa na mratibu wa Mradi wa Familia Inafaa huko mkoa wa Ruvuma. Wanakikundi ni wadau wa Familia Inafaa katika mkoa wa mashujaa wa kingoni, nyumbani kwa simba wa vita 



Hapa nikiwa na raia wa siku nyingi hapa Tanzania. Mzee huyu ananipatia somo juu ya malezi kulingana na uzoefu wake wa siku nyingi duniani hapa- asante mzee! 



      
                                                                                                                                                               Hapa nikiwa na wadau wa Familia Inafaa mkoani Mtwara; hapa ni kijiji cha Nanguruwe Mtwara Vijijini!


Familia Inafaa – Families Matter Program! (FMP)













Huu ni mradi unaongozwa na Kampuni ya T-MARC. Mradi huu unawalenga wazazi, walezi na wadau wa malezi ya watoto ambao bado hawajabalehe kwa wavulana na hawajavunja ungo kwa mabinti. Familia Inafaa! Ni mradi ambao tayari umeshaanza kutoa huduma kwa wazazi na walezi wa mikoa ya Mtwara na Ruvuma.
• Lengo la msingi kabisa la FMP ni kuwatia shime wazazi katika juhudi zao za kuwalea watoto wao ili wakue katika afya njema.

• FMP ni program mahususi kwa ajili ya wazazi. Imeandaliwa katika namna ambayo inawasaidia wazazi kutumia mbinu ambazo zinaweza kuwalinda watoto wao dhidi ya tabia hatarishi za afya ya jinsia, hivi sasa na wakati ujao pia.

• FMP inaamini kuwa wazazi wana nafasi yenye ushawishi mkubwa wa kujenga, katika namna chanya tabia za kiafya za watoto wao.

• Lakini hata hivyo ushawishi huo ni lazima ushindane na ujumbe wanaoupata watoto wao toka kwenye vyombo vya habari, vijana wenzao, na jamii yote kwa ujumla.

• Mawasiliano ya wazazi yanaweza kuwalinda watoto, kujenga uwezo wa kufanya maamuzi yafaayo, na kufikisha ujumbe sahihi.

• FMP inataka kuwasaidia wazazi “kuongeza ujuzi wao” kwa kuwapatia vifaa na mbinu mahususi kabisa ili waweze kuwa na mtindo bora wa afya katika familia zao.