Thursday, February 7, 2013

AFRIKA SIMAMA MWENYEWE


Bonde la Olduvai - Picha kwa hisani ya blogu husika

Waziri mkuu wa kwanza wa Kongo
Picha kwa hisani ya blogu husika

Bara letu tukufu la Afrika, kwa mara nyingine limo tena katika migogoro baina yetu wenyewe. Bara Afrika lenye nchi zaidi ya hamsini lilianza kujipatia uhuru wake zaidi ya miaka hamsini iliyopita. Ghana ilikuwa nchi ya mwanzo kabisa, yenye waafrika weusi wengi zaidi, kujipatia uhuru wake chini ya ndugu Kwame Nkurumah. Na mara ya mwisho nchi ya Afrika kujipatia uhuru wake ilikuwa ni Namibia? tarehe 21 Marchi 1990. Ukiacha Sudani Kusini iliyopata uhuru wake toka kwa ndugu yake Sudani tarehe 9 Julai 2011. Afrika Kusini; iliyopata uhuru wa watu weusi walio wengi mwaka 1994  ilikuwa na hali ya kipekee sana; ilivamiwa na wazungu walioifanya nchi hiyo kuwa nyumbani kwao. Nguvu ya Umma haikuzuilika tena na ilikuwa lazima wananchi walio wengi wapate haki yao. Kwa utangulizi huu, ingawa mfupi mno kwa bara lenye kila aina ya utajiri, binafsi nadhani bara hili, japokuwa ni changa kwa umri wa mataifa ya kisasa lakini kongwe kihistoria kwakuwa ndo nyumbani kwa binadamu wa kwanza; tazama Olduvai Gorge, ilitakiwa tuwe na uwezo wa kujitawala na kujisimama wenyewe. 

Afrika ina utajiri anuwai na wenye kupatikana katika nchi nyingi za barani mwetu. Pamoja na utajiri tulionao tunaendelea kuonekana kama masikini wa kutupwa. Wayuropa na Wamarekani na hata Waasia wanatufanya sisi (ama sisi wenyewe )  kama binadamu wa daraja la pili. Matokeo yake ni kubweteka, kukosa fikra zetu wenyewe, kuwa tegemezi na kusubiria misaada toka kwa hao wajomba wasiozaliwa tumbo moja na mama zetu.

Utegemezi upo kwenye nyanja nyingi sana za maisha yetu; toka kwenye mipango ya maendeleo hadi kwenye masuala ya vyakula vyetu wenyewe. Nchi zetu (kupitia viongozi tulionao) ni kama hazijui tunahitaji kitu gani na tunataka kwenda wapi. Utasikia mpango wa maendeleo tunanakili toka Ulaya na Marekani kama ilivyo ili hali tukibadilisha majina na mahitaji yetu mahususi tu. Jambo hili linadumaza hata fikra za vijana wetu shuleni na vyuoni; kwanini kuwa mbunifu ili hali mawazo yangu hayatumika popote, anajiuliza mwanafunzi. Badala ta kutumia muda mwingi kujenga fikra binafsi sahihi ni afadhali kufuatisha mawazo ya watu wengine. Utegemezi unatufanya tushindwe kujenga mambo yetu wenyewe. Mathalani kwenye elimu fursa za kimasomo zinazotolewa nje ya nchi; bila shaka ni kwa lengo zuri tu la kusaidia kujenga wataalamu toka katika nchi zinazokuwa. Hata hivyo ni vyema kutazama misaada ya aina hiyo kwa jicho la kichunguzi; inawezekana kabisa nyuma yake kuna fursa ama bidhaa zinazohitajika toka nchi zetu hivyo unazilainisha nchi hizi zinazoendelea kwa misaada midogo kama hiyo. Nasema midogo kwa sababu nchi zetu za kiafrika zina wajibu wa kujenga shule na vyuo vikuu vyenye sifa na hadhi kubwa kidunia kwa sababu vinavyohitajika kufanya hivyo vipo hapa barani. Tutazame mifano wa nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya watu wa Kongo. Kwenye makala hii nitatumia zaidi jina KONGO 

KONGO - Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo; Kongo ni "JITU" lililolala. Nchi hii ina utajiri asilia wa kila namna. Nchi Kongo kuna misitu asilia, madini ya kila namna, watu wenye nguvu na akili, ardhi/ wenye rutuba, mito, nguvu ya umeme, bahari, tamaduni nyingi nzuri na kadhalika. Pamoja na utajiri mkubwa usiodikika, wananchi wengi nchini Kongo hushindia mlo mmoja tena mara nyingi usio kamili. Wafanyakazi  wengi nchi humo hupitisha miezi bila malipo, bidhaa nyingi zinazopatikana huko hutoka nchi jirani. Kongo ilipopata uhuru wake toka mikononi mwa Ubelgiji (kinchi kidogo kikilitawala jitu kubwa vile) tarehe 30 Juni 1960 chini ya uongozi wa rais wa kwanza Joseph Kasa vubu na waziri mkuu wa kwanza Patrice Lumumba  ambaye alikuwa na mawazo mengi mazuri juu ya bara zima la Afrika, Siku ya uhuru wa nchi yake, kama ilivyokuwa huko Ghana kwa Kwame Nkurumah, aliyesema kuwa Ghana sana u huru milele, Lumumba yeye alisema Kongo itakuwa muhimili wa mambo mengi makubwa Afrika na duniani (si maneno yake moja kwa moja - mengi ni tafsiri na vionjo vyangu zaidi). Leo miaka zaidi ya hamsini kisha uhuru hakuna kiongozi wa jitu hilo kubwa aliyeweza kufikia mawazo ya mwana Afrika huyu halisi. Toka kifo chake nchi hii imekuwa itawaliwa kwa namna isiyokubalika, hususani kipindi cha rais aliyeiongoza nchi hiyo kwa muda mrefu Mobutu Sese Seko. Ndugu huyu aliifanya nchi kuwa mali yake binafsi na kufanya alivyotaka. Msemo wa Kiswahili; "Mungu si Athumani" bwana huyu aliondolewa madarakani na vikosi vya Laurent Kabila mwaka 1997. Laurent Kabila, kama ilivyo kwa historia za wapigania uhuru wengi wa Afrika, alishiriki shughuli za kisiasa toka ujana wake kwenye kikosi cha vijana cha Patrice Lumumba. Ndugu huyu alikuwa na matamanio na nia njema sana ya kuleta uhuru wa kweli kwa watu wa Kongo, lakini alishindwa kwa kuwa alikuwa amefungamana na makundi yaliyokuwa na uchu mkubwa wa mali za nchi hiyo. Hivyo miaka minne baadaye aliuwawa. Toka kuuwawa kwake bado hakujawa na uimara thabiti japokuwa Joseph Kabila, mtoto wa rais kabila, anajitahidi kuongoza nchi hiyo kubwa. Hata hivyo kuna waasi wanaoibuka na madai mbalimbali juu ya Kongo.

Hivi karibuni kumezuka kikundi kingine cha waasi maarufu kwa jina M23. Hili ni moja kati ya makundi mengi ambayo tayari yamekwishaibuka ili kudai wanachoita kuwa haki zao. Yamewahi kuibuka makundi mengine kadhaa wa kadhaa "Banyabulenge" na mengine.  Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, mashirika ya kikanda na mashirika mengine mbalimbali duniani yamejaribu kuleta amani ya kudumu bila mafanikio ya kweli kwa muda mrefu sasa. Binafsi nadhani suluhu kwa machafuko ya Kongo imo mikononi mwetu Waafrika na nadhani tunaweza kujilinda na kujiletea maendeleo ya kweli. Kongo ina utajiri mkubwa mno kiasi kwamba wengi wanaokwenda kupatanisha wanaingia kwenye mtego wa kujichukulia utajiri huo japokuwa kidogo- ni vigumu kupata ushahidi wa kuandikwa katika haya lakini kuna mambo mengi yanaendelea. Umoja wa Afrika kwa makubaliano ya Kongo unaweza kujenga jeshi imara na kulinda amani itakayoleta maendeleo ya kweli kwa nchi hiyo. Naamini kuwa uchumi wa Kongo ukiwa imara uchumi wa bara zima utanufaika na kukua vyema zaidi.  Afrika tuna uwezo na wa kufanya mambo yetu wenyewe shida ni huko kupumbazwa na Wayuropa na Wamarekani - matokeo yake tunajihisi kuwa hatuwezi. Afrika simama mwenyewe imara unaweza!

Sunday, January 13, 2013

TUTOE ELIMU SAHIHI YA BIDHAA KWA MLAJI


Saruji ya Rhino/  Kifaru - Picha na wadau



Saruji ya Simba- Picha wadau husika

Tanzania ni moja kati ya nchi zinazoendelea, uchumi wake kwa mujibu wa taarifa rasmi, japokuwa bado haujatafsiriwi kwenye maisha ya mwananchi wa kawaida, unaendelea kukua kwa kasi ya zaidi ya asilimia 6. Kasi ya asilimia sita, hii maana yake nini kwa mkulima wa Sangamwalugesha, Chibe, Kinyanambo n.k. Pamoja na uchumi wa Tanzania kukua kwa kiasi kilichoelezwa bado nchi hii haizalishi bidhaa nyingi zinazotumiwa na wananchi wake. Kumbe mawazo yale yale ambayo Mwalimu Julius Nyerere, Mzalendo Thomas Sankara na kanuni za kimaendeleo zinayapinga, waTanzania na waAfrika wengi hutumia bidhaa na huduma wasizozalisha wenyewe. Mfano magari mengi yenye kuleta foleni ndefu katika miji yetu hususani majiji, simu za mkononi ambazo kulingana na tafiti za hivi karibuni zimeleta mapinduzi makubwa na chanya ya mawasiliano hapa nchini na sehemu nyingi barani Afrika; pamoja na umuhimu wa bidhaa na huduma hizi hakuna ambazo tunazalisha wenyewe; karibu kila kitu kinatoka nje ya mipaka yetu. Sisi tunaendelea kuwa mabingwa katika matumizi ya bidhaa hizo toka nje na tena hushiriki kupata matoleo mapya zaidi, bila kuumia rohoni na akilini kuwa tunatumia tu walivyozalisha wengine na kwamba sisi pia tuna jukumu la kuzalisha.

Coca Coala - Picha wadau husika
Hatusemi kuwa Tanzania haijapiga hatua za kimaendeleo, la hasha! Maendeleo makubwa yamefikiwa nchini Tanzania toka nchi hii ipate uhuru, hatua hizo za kimaendeleo kwa hakika zaoneka vyema hata kwa asiye na macho ila tu kwamba mwendo kasi bado ni wa taratibu mithili ya ule wa kobe. Na kwa upande wa fikra sehemu nyingi za bara letu bado hatujajikomboa kwenye fikra yakinifu. Watu wetu wengi wanaendelea kuwa tegemezi wa nadharia na fikra za waYuropa na waMarekani na hivi punde tutahamia Beijing. Kufanya hivi kwa lengo la kujifunza si mbaya, lakini hatuna mikakati mahususi ya kufundisha na kuwaonyesha ukweli huo watu wetu ili kwamba waAfrika wengi zaidi tuweze kuwa na ujuzi wa kiteknolojia unaotokana na tamaduni zetu wenyewe. Ili watu wengi zaidi tuweze kukomaa kifikra na kuwa na uwezo wa kuchambua masuala ya msingi maishani na kujenga hoja zenye mashiko na katika misingi inayokubalika, basi ni vyema watu wetu wapate kusoma falsafa, na tena waisome kwa lugha zao wenyewe. Suala hili tunaweza kuliongelea siku nyingine, sasa natuingie mada ya leo. Elimu ya mlaji juu ya bidhaa anuwai zilizopo kwenye maduka na sehemu mbalimbali za kutolea huduma kwa wananchi.

Hapa nchini na nchi nyingi Afrika, tuna bidhaa nyingi zinazotoka nje ya bara letu, zipo pia zinazotengenezwa katika nchi zetu. Kuna bidhaa anuwai katika maduka ya bidhaa; baadhi ya mahitaji hayo yapo toka viwanda, nchi, tamaduni na ustaarabu tofauti na wa nchi mbalimbali. Chukua mfano wa dawa ya meno. Madukani zipo za kila aina; Whitedent, Colgate, Rungu, nini dent na kadhalika.., Sabuni za kipande; Jogoo, Mbuni, Magwanji, Dobi...Sabuni za kuogea; Malaika, Ayu, Geisha, Protex, Familia...Sigara; Nyota, Baridi, SM, Aspen, Portsman n.k. Baadhi ya bidhaa nilizozitaja huwa na maelezo ya matumizi na faida kwa mlaji / mtumiaji. Hata hivyo tuna bidhaa nyingine nyingi ambazo hazitoi maelezo yoyote ya matumizi, faida na hata hasara kwa mtumiaji lakini bidhaa hizo zipo madukani na sehemu nyingine za kujipatia mahitaji. Ni jambo muhimu na lazima kwa  bidhaa kuwa na maelezo kwa mtumiaji. Vyombo husika nchini vina jukumu la kufanya hivyo ili kunusuru afya za wananchi na kuwawezesha kufika inapotakiwa.

Nchini kuna mafanikio yaliyofikiwa; watengeneza sigara walitakiwa kuweka alama ama tangazo linaloonyesha madhara ya bidhaa hiyo na kwamba atakayeamua kuitumia afanye hivyo kwa hiari yake mwenyewe na si kwa kukosa elimu. Nadhani halikuwa jambo jepesi, pamoja na kwamba maandishi yale ni madogo, lakini walau jambo hilo limefanyika. Hata hivyo kuna bidhaa nyingine nyingi zinahitaji kuelezewa ili kufanya mambo yaende sawa sawa. Natumia mifano miwili tu hapa. Mmoja ni mfano wa bidhaa inayoingia mwilini mwa binadamu na mwingine ni wa bidhaa tunayoitumia kujenga nyumba zetu; vinywaji baridi na saruji.

Kinywaji Pepsi - Picha wadau husika
Vinywaji baridi  al maarufu zaidi SODA; havionyeshi vilivyotumika kutayarisha bidhaa hiyo.  Faida wala hasara yake mwilini haijulikani kwa watu wengi. Binafsi naamini kuwa bidhaa hizi zina faida na hasara mwilini kama ilivyo kwa bidhaa nyingi, sasa kama ni hivyo kwanini mimi mtumiaji sipatiwi hiyo elimu? Je nini lengo la kutotoa elimu hiyo kwa mtumiaji? Je, tunaangalia faida za kiuchumi tu kuliko afya ya mlaji? Ni muhimu kwa vyombo husika kuwasimamia waandaa bidhaa hiyo ili watoe hayo maelezo muhimu. Na serikali kwa ujumla wake inalazimika kusimamia hilo, ni vyema kufanya hivyo bila kuogopa tu kupungua kwa kodi toka makampuni husika pindi wananchi watakapofahamu kilichomo ndani ya vinywaji hivyo na kusitisha ama kupunguza matumizi yake. Najua yamekuwa ni mapokeo kwa baadhi ya bidhaa, toka nchi fulani zenye nguvu kiuchumi, kutotaja vilivyomo kuepuka mbinu zao za biashara kuibwa na washindani wao, lakini sisi tunasema afya za watu wetu walio wengi ni muhimu zaidi kuliko faida za wachache wanaonufaika kupitia ujinga wetu juu ya bidhaa zao.

Saruji Twiga - Picha na wadau husika
SARUJI: hii ni bidhaa muhimu katika nchi nyingi zinazoendelea; nimeona hata kauli mbiu ya moja ya makampuni hayo kuwa ni kulijenga bara Afrika. Nchini Tanzania, hivi sasa kuna makampuni kadhaa yanayozalisha bidhaa hii muhimu. Kwa hakika hili ni jambo la msingi na la kimaendeleo kabisa kupitia bidhaa hii wananchi wengi zaidi wanaweza kujijengea nyumba zao za kisasa na za kudumu kwa muda mrefu zaidi kuliko za tope na nyasi. Mjini Mtwara; kwenye maduka mengi ya vifaa vya ujenzi utakutana na saruji / simenti ya Simba, Twiga, Rufiji, Rhino na kadhalika. Bidhaa hizi huwa na bei tofauti tofauti; tofauti hii ya bei bila shaka inasababishwa na mambo kadhaa; huenda ikawa ni gharama za uzalishaji, ubora, ama tu tamaa ya pesa nyingi. Hata hivyo tatizo langu hapa, kama ilivyo kwa SODA ni lile lile la kutopata elimu ya mtumiaji. Sikumbuki kuona mfuko wa simenti aina yoyote, hata mara moja, ukiwa na maelezo juu ya bidhaa na utumike sehemu ipi ya nchi; kwa maana ya aina ya udongo ama ardhi, ama aina fulani ya saruji itumike katika hatua ipi ya ujenzi; msingi, kujenga boma na kadhalika. Nafahamu kuwa baadhi ya makampuni ya ujenzi hufanya upembuzi yakinifu juu ya hilo na kujua pengine aina ipi ya saruji itumike, hata hivyo inanitia mashaka kwa kuwa hakuna kilichoandikwa popote pale. Makampuni, na wananchi wenye uwezo mkubwa zaidi kiuchumi wanaweza kufuata maelekezo na taratibu za kihandisi kwa uaminifu na si wananchi wa kawaida. Mwananchi anayejenga wa kiwango cha kati atatumia saruji ya bei ya juu kwa imani kuwa hiyo nd’o yenye ubora takikana ama atatumia uzoefu wa fundi mahalia, ambaye mara nyingi hana hata hiyo elimu husika.


Saruji Tembo - Picha na wadau husika
Wito kwa wadau wa saruji, najua kuwa sisi sote ni wadau, lakini moja kwa wenye makampuni ya kutengeneza saruji; wahakikishe wanaweka maelekezo yatakayoheshimu thamani ya pesa na kumpatia mtumiaji/mlaji kile anachohitaji na kustahili kupata. Kwa vyombo husika vya serikali; wasimamie kuwekwa kwa maelekezo hayo ili wananchi wanufaike vilivyo na kujenga taifa la watu wa kima cha kati kama usemavyo mkakati wa maendeleo wa taifa wa 2025 na si hohehahe. Wananchi mmoja mmoja tusaidiane kudai haki zetu kwa njia ya amani na kwa utaratibu unaokubalika kisheria.


Hitimisho la jumla ni kwamba wazalishaji wote nchini na barani Afrika wazalishe bidhaa zenye ubora, maelekezo ya matumizi kwa walaji / watumiaji ili kujenga afya njema kwa wananchi na kusaidia kusukuma mbele zaidi hatua za kimaendeleo kwa wananchi mmoja mmoja, Tanzania na bara Afrika zima kwa ujumla wake.

Monday, December 24, 2012

HERI YA NOELI NA MWAKA MPYA


Picha kwa hisani ya blogu wadau

Saa chache zijazo sherehe ya Noeli ama maarufu zaidi kama "krismas" itaanza kwa Misa, ibada na karamu mbalibali kusheherekea kuzaliwa kwa Yesu Kristo miaka zaidi ya elfu mbili iliyopita.
Sherehe za siku kuu hii huwa ni kubwa pengine kuliko sherehe nyingine katika nchi zinazotumia kalenda ya Kigregory inayosoma mwaka huu kuwa ni 2012. Sherehe hizi huwa kubwa kwa sababu kadhaa; chache kati ya hizo ni sherehe ya kiimani kuzaliwa kwa mkombozi; yeye ambaye alikubali kujitoa kwa hiari ili kusaidia wengine, shughuli kubwa za kibiashara zafanyika wakati huu, na tatu inaungana na zingine ni mwisho wa mwaka.
Mwisho wa mwaka ni kipindi mwafaka kwa karibu binadamu wote; ni kipindi cha kufanya mahesabu, je, mambo yamekwenda kama tulivyotarajia katika shughuli zetu?, wapi tuboreshe, ama turekebishe? Wapi tumefanikiwa na tuna haja na haki ya kujipongeza? Tukifanya sherehe hizi tunawajibika kulinda afya na usalama wetu.
Kuwa na afya njema ni jukumu letu la kwanza kabisa. Kupitia afya njema ndo mengine yaliyo mengi ama karibu yote hufanyika. Hivyo wakati tukisheherekea tunalazimika kufanya sherehe zetu kwa kadri, tusifuje kila akiba tuliyonayo kwenye sherehe hii, tufurahie ili hali tukiwa na akili zetu timamu; wanywaji tufanye hivyo kwa kiasi sana. Wote twale; tule kwa kiasi tule kwa afya. Tunaosafiri; madereva wote waendeshe kwa umakini zaidi kuliko pengine vipindi vingine vya mwaka. Kamwe dereva usinywe kinywaji chenye kilevi na kuendesha. Tukifanikisha haya yote kwa hakika tutakuwa tunajipanga vyema zaidi kuuanza mwaka mwingine kwa mafanikio.

                                 Kila la heri ya Noel, Merry Christmas na Joyeux Noël

Tuesday, December 11, 2012

SACCOS suluhisho la Mitaji kwa Wasanii


Picha kwa hisani ya mtandao Mkurugenzi wa Basata ndugu Ghonche Materegho na Mbunifu mahiri wa sanaa ya mitindo ya mavazi nchini Tanzania ndugu Mustafa Hassanal  
Picha kwa hisani ya Tanzaniatoday 
Na Mwandishi wa BASATA

Wasanii nchini wametakiwa kutumia vyama vya kuweka na kukopa (Saccos) ili kujiwekea akiba itakayowawezesha kukopa ili kuendeleza kazi zao za Sanaa.

Akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa Jumatatu iliyopita, Mwenyekiti wa SAA Saccos ambayo inamilikiwa na washereheshaji (Mc’s) na wachezeshaji muziki (Dj’s), Emmanuel Urembo, amesema saccos ni suluhisho la mitaji kwa kazi za wasanii ambao wengi wao wameshindwa kukamilisha kazi zao kutokana na ukosefu wa fedha za kutosha.

Saccos zinaweza kuwasaidia kupata mitaji na kujikwamua kiuchumi kwa kupata mikopo yenye riba nafuu ili kuendeleza ubunifu walionao, kwa kuwa wasanii wamekuwa hawana sifa za kukopesheka na benki mbalimbali kutokana na kutokuwa na fedha na dhamana za zinazowezesha mkopaji kupewa mikopo, lakini kwa kupitia saccos zao wenyewe wanaweza kujikopesha na kujiendeleza zaidi.

Aidha Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa nchini, Ghonche Materegho, aliwasisitiza wasanii kuanza kujizoesha kujiwekea akiba. Aliwahimiza wasanii kujifunza kwa SAA ambao wameshaanza katika mfumo huu wenye kuleta maendeleo na tija katika sekta ya sanaa, “kuendelea kulia juu ya ukosefu wa mitaji ya kufanyia kazi zetu na miradi ya sanaa hakutusaidii kusonga mbele, bali tunapaswa kujikwamua wenyewe kwa kuanzisha vyama hivi vya kuweka na kukopa kwa maendeleo yetu wenyewe” alitilia mkazo zaidi.



12.12.12

December, 12, 2012 or 12-12-12 was the last date of its kind - when all three numericals in a date are the same - for the next 88 years. The next time this will happen is on January 1, 2101, or 01-01-01.
Illustration image
12-12-12 was a special date.
©iStockphoto.com/Serdarbayraktar

Counting down the seconds

According to popular belief, 12-12-12 is a lucky date that will bring good fortune. Many engaged couples plan to hold their weddings on December 12, 2012, while some expectant parents hope to deliver their baby on that date.
For people attaching special significance to numbers, the highlight of this auspicious day will occur at twelve minutes and twelve seconds past noon. At that moment, the numerical pattern will consist of no less than six repetitions: 12-12-12 12:12:12

What will happen on December 12, 2012?

The rare numerical pattern may make some people believe that something extraordinary will occur at this very moment. However, the global significance of 12-12-12 12:12:12 is undermined by the fact that it occurs at different times in every time zone around the world. So, while Kiribatiexperiences the auspicious second at 22:12:12 on December 11, 2012 (UTC), clocks around the world will still show a very different time, and about half the planet will not even have entered December 12 yet. In countries that use the 12-hour time format, there will even be two instances of 12:12:12 per time zone: first just after midnight (12:12:12 a.m.), then just after midday (12:12:12 p.m.).
Countless internet sources also claim that the end of the World, as prophecised by the Mayans, will occur on this date. However, the Mayan Calendar ends on December 21, 2012 and not on December, 12, 2012.
For most people, 12-12-12 12:12:12 is nothing but a fun fact, and December 12, 2012 will be a day like any other.

The significance of 12

The number 12 has a great significance in many cultures. In western tradition, it is commonly associated with completeness and seen as a perfect and harmonious unit. As such, it has found its way into religion (e.g. the 12 apostles), mythology (e.g. the 12 gods of Olympus), and every day life (e.g. 12 hours on a modern clock face).
The practical and numerological significance of the number 12 is attributed not least to its mathematical properties. There are few small numbers that can be evenly divided by so many subsets. 12 is evenly divisible by 1, 2, 3, 4, and 6.

Saturday, November 17, 2012

MAZOEZI YA UFUNZAJI STEMMUCO 2012



Mwalimu wa hesabu akionyesha moja ya matumizi ya hesabu nyumbani

Kama ilivyo ada kwa waalimu wanafunzi wa mwaka wa tatu chuoni STEMMUCO hupata fursa ya kufunza darasa dogo kila mwaka. Mwaka huu wa taalumu zoezi hilo limeanza Jumamosi ya tarehe 10 Novemba 2012. Vipaji, kujituma na uwezo wa walimu wanafunzi wa chuo hapo vimeendelea kudhihirika. Hapa ni sehemu kidogo ya kilichojiri katika moja ya Jumamosi hizo. 




Mwalimu wa Jiografia na mabadiliko ya hali ya hewa
















Mwalimu wa Kiingereza kazini
Mwalimu wa Historia kazini - Vita ya Majimaji

































  

TAMASHA LA MaKuYa

Tamasha la Ngoma za asili la makabila ya mkoa wa Mtwara Maarufu kama Tamasha la MaKuYa limeanza rasmi, huku vikundi mbalimbali vya sanaa vikionyesha umahiri mkubwa katika kucheza ngoma za asili za makabila yao.

Tamasha hilo ambalo mwaka huu lilianza kwa maandamano kutoka katika viwanja vya mashujaa kwenda Uwanja wa Nangwanda maarufu kama uwanja wa Umoja mjini Mtwara limevuta hisia za wakazi wengi wa mji huo na vitongoji vyake ambapo licha kuwepo kwa jua kali, watu waliendelea kumiminika uwanjani, mithiri ya maji mtoni, kushuhudia wasanii wakisakata ngoma mbalimbali.

Thursday, November 15, 2012

MHADHARA WA NJIA YA UFUNZAJI VYUO VIKUU - SAUT MTWARA (STEMMUCO)

Sehemu ya Chuo Kikuu Aalborg
Chuo Kikuu Kishiriki Cha Stella Maris Mtwara (Cha Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino Tanzania) kilikuwa mwenyeji wa wanazuoni toka chuo kikuu cha Aalborg cha nchini Denmark.

Pamoja na kubadilishana mawazo wanazuoni wawili toka chuo hicho kikuu Profesa Jens Muller(PhD) na Profesa Mona Dahms waliotoa mada ambazo zilijadiliwa na wanazuoni wa Stemmuco ndugu Festo Gabriel na Profesa Eginald Mihanjo(PhD). Kisha mada hizo zilijadiliwa na wanachuo na wanataaluma waliohudhuria mhadhara huo.
Sehemu ya Chuo Kikuu Kishiriki Stella Maris Mtwara
Jens Muller, amebobea katika sayansi ya uhandisi, katika mada yake aliongelea suala la teknolojia mahalia na ulazima wa kuikuza teknolojia hiyo ili iwe na mchango kwa teknolojia ya dunia.

Gabriel Festo, akijadili mada hiyo alisisitiza kuwa jamii zetu nyingi za kale zimekuwa na teknolojia yake na wajibu wetu leo ni kuziendeleza na kujichochea jamii hizo kuziibua zaidi teknolojia hizo ili ziinufaishe jamii kubwa zaidi.

Mona Dahms aliongelea juu ya namna ya ufundishaji katika vyuo vikuu; alieza kuwa chuo chake kimekuwa kikifuata mfumo wa utatuzi wa matatizo katika ufundishaji. Alisema, tafiti zinaonyesha kuwa vijana wanaofundishwa kwa utaratibu huo wanaonekana kufanya vyema wanapokuwa kazi.

Eginald Mihanjo, mtaalam wa historia, aliwapongeza wanazuoni wa Aalborg kwa njia yao hiyo ya ufundishaji. Aliongeza kuwa huo ni mfumo mzuri ambao Tanzania iliutumia kupitia falsafa ya elimu ya Julius K.Nyerere aliyefuata na kusisitiza kuwa elimu iwe kwaajili ya kujitegemea. Mfumo huo haupo tena na hii ni hatari kwani vyuo vyetu vinaweza kutoa wahitimu wasio na ujuzi hitajika katika jamii.

Wednesday, November 14, 2012

TANZANIA NA KISWAHILI


Picha kwa hisani ya blogu ya udadisi
Kila nchi duniani hutambulika kwa mambo kadha wa kadha; Japan wanatambulika kwa ubobeaji wao kwenye teknolojia, Marekani wanatabulika katika kwa nguvu zao za kiuchumi, kisiasa, nk. Tanzania, pamoja na kutambulika kupitia mlima Kilimanjaro, mbuga nzuri za wanyama kama Serengeti, historia nzuri na kuvutia kupitia visiwa vya Zanzibar hutambulika pia kupitia Kiswahili.


Mlima Kilimanjaro  Picha hisani ya wwf
Nchi nyingi duniani huongea Kiswahili, hata hivyo Tanzania inaendelea kutambulika kuwa kiranja wa lugha hii adhimu. lakini je, lugha hii ina fursa zozote? Na je, watanzania wanazitumia vipi fursa hizo na ni kwa kiasi gani nchi ina nufaikanazo? Na jamii ya wanazuoni wana mchango upi katika ukuzaji wa lugha hii? Hebu tupitie sehemu ya hotuba ya waziri mkuu ndugu Mizengo Peter Pinda kama ilivyoandaliwa na blogu ya udadisi:  

IV UENDELEZAJI WA LUGHA YA KISWAHILI
22. Mheshimiwa Spika, katika Mkutano huu wa Bunge, Waheshimiwa Wabunge walipokea na kujadili pamoja na mambo mengine Maazimio mbalimbali. Niruhusu nirejee Azimio lililonigusa sana kuhusu Uanzishaji wa Kamisheni ya Lugha ya Kiswahili. Awali, Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA), Chama cha Kiswahili Tanzania (CHAKITA) na Wawakilishi kutoka Uganda walianzisha wazo la kuwa na Mpango wa Kuundwa kwa Baraza la Kiswahili la Afrika Mashariki. Hata hivyo, Baraza hilo halikuanzishwa, badala yake ikapendekezwa kuanzisha Kamisheni ya Lugha ya Kiswahili. Azimio la Kuanzishwa kwa Kamisheni hiyo ya Lugha ya Kiswahili tumelipitisha katika Bunge hili. Nitumie fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri sana mliyoitoa.....

Tuesday, November 13, 2012

KONGAMANO LA KIMATAIFA KUZUIA UHALIFU KWA VIJANA


Baadhi ya washiriki wa mhadhara wa kimataifa wa kuzuia uhalifu wa vijana katika jamii
White Sands Dsm 6-8 Nov 2012
Hivi karibuni Tanzania ilipewa uenyeji na taasisi ya haki na uzuiaji wa uhalifu ya Afrika Kusini (CJCP), kuendesha mhadhara (kongamano) wa kuzuia uhalifu kwa vijana. Mhadhara huo ilijumuisha wadau wa kada kadhaa: wanawake, vijana, watoto na yote ambayo yanalenga kuzuia uhalifu katika jamii. Mkutano huu ulifanyika hoteli ya White Sands (tarehe 6 - 8 Novemba 2012), Dar es Salaam.

Ndugu Msangi akitoa mada juu ya sera za jeshi la Polisi Tz















Mhadhara huu ulikuwa na mada anuwai zilizofanyiwa kazi. Malezi mema kwa watoto wangali wadogo kabisa, Njia mbadala za kuzuia uhalifu katika jamii, Polisi jamaa na vijana, Njia mbadala na fursa za kazi kwa vijana na kadhalika.

Ndugu Mandalu akitoa mada juu ya njia mbadala kupunguza
uhalifu miongoni mwa vijana















Wanamhadhara walitoka zaidi ya nchi ishirini na tano za mabara karibu yote ya dunia. Kwa hakika ilikuwa ni fursa nzuri kusikia wadau wa haki na amani wanavyofanya kazi kufanya dunia kuwa sehemu njema na ya kufaa kuishi sisi sote. Wanataaluma hawakuachwa kando pia, waliwasilisha tafiti zao zenye kutoa maelekezo na mwongozo wa namna ya kupunguza uhalifu katika jamii, wakati huo huo vijana, ambao ni wahanga wa fujo na wanawezeshwa kuondokana na adha hiyo. Inafahamika vyema kuwa wadau wakuu wa ujenzi wa dunia ni vijana, kwa kuwa ni kundi la watu wenye uwezo na nguvu kazi kubwa; kwahiyo basi ni muhimu kuwalea vyema wadau hao.   
Ndugu Muchunguzi akiwasilisha mada juu ya malezi

Monday, October 29, 2012

Mhadhara wa Katiba CHUONI STEMMUCO

Nchi ya Tanzania,  inaendelea na mchakato wake wa kuandika katiba mpya yenye mguso wa moja kwa moja toka kwa WaTanzania walio wengi. Katika juhudi hizo wadau mabalimbali ikiwa ni pamoja na taasisi, watu binafsi na kadhalika wanafanya juhudi kuwaelimisha wananchi walio wengi na wasio na ujuzi na uelewa wa katiba inayotumika nchini hivi sasa. STEMMUCO kwa nafasi yake imefanya kazi hiyo ya kuwaelimisha wanachuo juu ya katiba inayoiongoza Tanzania kwa sasa. Idara ya sheria, chuoni hapo imeongoza mhadhara wa wazi kwa wote waliopenda ili kuielezea katiba hiyo.








Thursday, October 25, 2012

MCHWA NA MAENDELEO MTWARA

Nguzo yenye kusambaza nishati ya umeme ikisaidiwa kazi hiyo na mti jirani
Manispaa ya Mtwara - Mikindani ina utajiri mkubwa wa kila namna. Kwa uchache utajiri huo unajumuisha, ujuzi wa uchongaji vinyago, ngoma za aina yake, mazao ya kibiashara; korosho, karanga na kadhalika, mali asili lukuki, kina bandari asilia, gesia asilia na kadhalika na kadhalika.





Mchwa ni moja ya utajiri mkubwa wa Mtwara, wataalamu wa masuala ya viumbe hai tunawaomba wafanye tafiti zinazowalenga mchwa kuona ni namna gani Mtwara -Mikindani na taifa kwa ujumla linaweza kunufaika na viumbe hawa. Wapo karibu kila sehemu na hushamiri zaidi kipindi cha ukame, huvamia karibu kila kitu kikavu kilicho mbele yao.





Sehemu ya nguzo iliyooza kwa karibu inavyoonekana


Hii nd'o nguzo iliyooza vibaya kwenye picha ndogo hapo juu

Katika pitapita zangu nimekuta mji kati kabisa wakiwa wamekula nguzo zisambazazo nishati ya umeme na sikuona juhudi za maana zikichukuliwa kunusuru linaweza kuwa tishio la maisha mjini humo.

Thursday, September 27, 2012

SIKU YA UTALII TANZANIA NA DUNIANI

Kazi ya Sanaa Mji mkongwe MIKINDANI
Wanayama wakivuka mto huko Serengeti - Tanzania



Sanaa MIKINDANI - MTWARA

Faru weusi huko Ngorongoro - Tanzania





















Leo ni siku ya UTALII TANZANIA NA DUNIANI: Utalii ni moja kati ya vyanzo vikubwa vya uchumi duniani. Kuna nchi kadhaa ambazo hutegemea tu uchumi kujiendesha na kuendelea kuwepo. Kikubwa ni uwekezaji wa makusudi na lazima katika sekta hiyo yenye uwezo wa kuzalisha ajira lukuki. Tanzania ina mali asili nyingi mno ambazo ni vivutio tosha vya utalii; moja ya mambo yanayoturudisha nyuma katika hili ni uwekezaji hafifu kwa watu wetu.

 Uwekezaji huu utazame kwa makini hasa aina ya elimu tuitoayo kwa wanafunzi wetu; kwa kuwa tuna vivutio vingi vya utalii basi tuwe na mitaala yenye kulenga utalii toka shule ya msingi. Shule zetu ziwe na michepuo yenye kuendana na mahitaji ya karne ya ishirini na moja. Kuwe na shule zenye kuangazia masomo ya sayansi na teknolojia yenye kujibu mahitaji ya moja kwa moja ya watu wetu. Tukirudi kwenye utaliii, shule na mitaala yenye kufunza huo utalii zianze mapema kufunza yaliyo ya lazima; uaminifu, ukarimu, lugha za kigeni, na mengine muhimu hiyo itasaidia kutumia vyema rasilimali na utajiri mkubwa tuliopatiwa na Mwenyezi Mungu, kinyume na hivyo tutaendelea kuwalaumu majirani waliojipanga kunufaisha jamii zao na hiyo nd'o hasa jukumu la serikali.    


Friday, September 21, 2012

Mashindano ya Hisabati, kemia, Fizikia, Jiografia n.k

Msaani Akitoa burudani kwa umma- Mashindano ya mavazi, mavazi sahihi- picha kwa hisani ya google?
Hapa duniani kila jamii ina aina fulani ya burudani na hiyo muhimu kwa maisha ya binadamu. Hata hivyo maisha ya nchi na watu wake ili yaweze kwenda mbele na nchi kupiga hatua za kimaendeleo ni muhimu ikawekeza kwa kiasi kikubwa zaidi katika elimu. Elimu kama tuambiawavyo nd'o ufunguo wa maisha. Elimu ndio inaweza kuwaweka sawa, kwa kiasi fulani, watoto wa tajiri na wamasikini. Ni kupitia hiyo elimu ndo mambo mengi iwe ni burudani; muziki, mpira, urembo, sana ya mavazi, iwe ni mawasiliano, sheria, tiba, taja tasnia zote; zinahitaji elimu ili kufanya vyema zaidi.

Nchini Tanzania, nchi yangu hii, kwa maoni yangu naona elimu hatuipatii fursa ya kutosha; ni kweli Serikali na wadau wengine wengi wanajitahidi kwa kiasi kikubwa kutoa huduma hiyo muhimu kwa jamii. Hata hivyo juhudi mara dufu bado yahitajika. Kuna njia na mbinu nyingi elimu inaweza kuiga toka kwenye kada nyingine hapa nchini.

Kwenye Muziki, filamu na sekta nyingine, wadau kadhaa wameanzisha tamasha maalumu kutafuta vijana wenye vipaji, na tamasha hizo zinafanywa kwa mbwembwe,ubunifu na bila shaka udhamini mkubwa na wenye gharama kubwa tu. Jambo hili ni jema sana kwani shughuli hizi zinachangia kuwakwamua vijana toka kwenye kukosa ajira na kuweza kupata kipato ambacho bila shughuli hizo wasingekipata.  Hata hivyo wazo na wito wangu: kuibuke wadau wengine watakao fanya mashindano ya vijana kwenye hisabati, fizikia, baiolojia, jiografia, kiswahili... wazunguke mkoa mmoja hadi mwingine kupata wataalamu wa hisabati, na kadhalika. Kufanya hivyo kutatuwezesha kupata teknolojia na kujenga hamu ya kubobea na kujikita zaidi  katika ulimwengu wa sayansi na teknolojia.   

Monday, August 27, 2012

Wasanii watakiwa kujiendeleza kitaaluma


Na Mwandishi BASATA

Mkufunzi wa masuala ya uandaaji wa Filamu Ngalimecha
 Ngahyoma akizumza jambo na wadau wa sanaa
ukumbi wa Basata

Wasanii wa nchini wametakiwa kujiimarisha katika masuala ya taaaluma ili waweze kufanya kazi zenye ubora na zinazokidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchini.

Akizungumza katika Jukwaa la Sanaa jana, mkufunzi wa masuala ya uandaaji wa filamu hapa nchini Ngalimecha Ngahyoma amesema kumekuwa na matatizo mengi katika uandaaji wa kazi za filamu hapa nchini kutokana na wasanii kutokuelewa misingi ya uandaaji wa filamu.

“Kuna maeneo ya msingi ambayo yanahitaji watu kubobea ili kuyafanya kwa utimilifu, na hakuna njia ya mkato ni lazima kuyapata shuleni kwa maana lazima mtu ufundishwe. Wasanii wengi wanatumia vipaji vyao, lakini matokeo ya kufanya mambo kwa vipaji ndiyo haya ambayo yanatupa filamu zenye matatizo katika maeneo mbalimbali,” alisema.

Tuesday, August 7, 2012

BASATA LAKERWA NA WASANII KUNG’ANG’ANIA FILAMU NA MUZIKI PEKEE

BASATA LAKERWA NA WASANII KUNG’ANG’ANIA FILAMU NA MUZIKI PEKEE


Na Mwandishi wa BASATA

Sehemu ya wadau waliohudhuria kwenye Jukwaa la Sanaa
wiki hii wakifuatilia kwa makini programu
Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limeeleza kusikitishwa na hali iliyopo sasa ya wasanii kuzipa kisogo Sanaa zingine na kung’ang’ania filamu na muziki pekee hali inayowafanya wengi wao kubaki wakihangaika na kulalama.

Akizungumza wiki hii kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa inayofanyika makao makuu ya Basata, Katibu Mtendaji wa BASATA Ghonche Materego alisema kuwa, ni jambo la kushangaza kuona wasanii wakifunga milango yote katika sekta ya Sanaa na kubaki wakihangaika na madirisha mawili tu ya filamu na muziki.

“Ndugu zangu hebu tujiulize tu, Sanaa ni pana sana na ina fursa nyingi katika kutupa ajira na kuzalisha kipato kwa vijana wengi lakini kwa nini wote tunang’ang’ana na filamu na muziki pekee? Fursa nyingine tunamwachia nani? Alihoji Materego.

Monday, August 6, 2012

Wabunge ‘wala’ rushwa marufuku kuingia China

Bunge la Tanzania Mjini Dodoma















Tumeambiwa na tunafahamu siku zote kuwa rushwa ni adui wa haki, na ni ya wananchi, ya binadamu, ama ya viumbe vilivyo hai walau kulingana  na miongozo na makubaliano yetu. Moja ya makubaliano hayo, kwa Tanzania ni kuwa rushwa ni adui wa haki, na kwenye kanuni/ ahadi za mwanaTANU (chama kilichopigania uhuru wa Tanganyika) kulikuwa na ahadi ya kutotoa na kutopokea rushwa kwani hupinga ama huzuia watu wengine kupata haki zao.

Katika nchi nyingi duniani, Tanzania ikiwa mojawapo, kuna utaratibu wa kuwa na chombo cha kutolea mawazo, kuihoji serikali iliyo madarakani, kutunga sheria n.k. Chombo hicho kinafanya kazi kwa uwakilishi; si rahisi kwa mwananchi mmoja mmoja kuingia katika chombo hiko kutetea, kudai haki yake ama/ na kufanya shughuli zingine za chombo hicho ambazo kwetu kinajulikana kwa jina la BUNGE. Kwa kuwa si rahisi wote kuingia basi tumelazimika kuwa na wawakilishi wachache ili wawe SAUTI zetu na waseme na kutenda kwa niaba yetu. Hivi karibuni tumesikia habari ya kushangaza juu ya hawa wawakilishi wetu. Tumesoma na kusikia vyombo vya habari vikielezea juu ya baadhi ya wawakilishi wetu hawa wakifanya kile tulichofundishwa kuwa ni adui wa haki, sio lengo la makala hii kuongelea suala hilo bali tu kuiwasilisha makala iliyo katika gazeti la MTANZANIA inayoeleza juu ya kicha habari.   

Mwalimu JKNyerere aliwahi kusema IKULU ni patakatifu nadhani BUGENI halikadhalika ni vivyo hivyo. Je, kama kweli kuna wabunge wameenda kinyume na utakatifu inafaa kweli waendelee kuwepo patakatifu?

Na Arodia Peter .

TUHUMA za rushwa zinazoendelea kuwaandama wabunge, zimechukua sura mpya, baada ya Serikali ya China kujiandaa kupiga marufuku wabunge wote wanaotuhumiwa kujihusisha na rushwa kuingia nchini humo.

Habari za uhakika ambazo MTANZANIA imezipata kutoka ubalozi wa China hapa nchini, zinasema umepokea taarifa rasmi kutoka kwa viongozi wakuu wa China, wafuatilie kwa karibu wabunge wote wanaotuhumiwa kwa rushwa, kisha watume taarifa ili wakibainika wasiingie kwenye nchi hiyo.
“Tumeletewa taarifa na viongozi wetu wa ngazi za juu, kuwa tufuatilie kwa kina wabunge wote ambao wanatuhumiwa na wakibainika majina yao yatumwe China, ili wazuiliwe kuingia kule,

…unajua taifa letu ni taifa ambao halina mchezo na mtu anayepokea rushwa ovyo ovyo na ni kosa la jina. kwa kiongozi kama hawa wabunge kujihusisha na siasa,

“Kwa kipindi chote hiki, kama wabunge hawa wangekuwa China leo hii, tungekuwa tunazungumza mambo mengine, wangekuwa wamechukuliwa hatua kali,

“Tunashangaa kuona kwa nini hapa kwenu, bado wanaendelea kuruhusiwa kuingia bungeni… au wanasubiri majibu ya kamati ndogo iliyoundwa kuchunguza tuhuma hizi,” kilihoji chanzo chetu.

Chanzo hicho, kilisema ubalozi wa China hapa nchini, umetuma maofisa wake mjini Dodoma kwa ajili ya kupata mwenendo wa wabunge wote wanatuhumiwa.

“Hivi sasa hapa Dodoma kuna maofisa wa ubalozi wa China, wanaendesha uchunguzi kuhusu tuhuma hizi, ikibainika ni za kweli baada ya majina ya wabunge ‘wala rushwa’ kutajwa, watachukua picha zao kwa ajili ya kuzituma China, ambako hawataruhusiwa kukanyaga kwa sababu kwao rushwa ni kosa la jinai,” kilisema chanzo chetu.

Naye Mratibu wa maombi yanayoendeshwa na Umoja wa Makanisa ya Kikristo Tanzania, mjini Dodoma Mchungaji William Mwamalanga alisema kwa kauli moja viongozi wa dini, wamesikitishwa na tuhuma hizo.

Alisema viongozi wa dini ambao wamepiga kambi mkoani Dodoma, kwa ajili ya kuliombea taifa, wamewataka wabunge wote waliotajwa wajiuzulu mara moja.

“Viongozi wa madhehebu mbalimbali tupo hapa Dodoma, kwa ajili ya kuliombea taifa, lakini moja ya jambo kubwa ambalo tumekubaliana kupita katika majimbo yao, kueleza waumini wetu matatizo haya ya rushwa… tunataka wajiuzulu kwa ajili ya kulinda heshima zao,  

Saturday, July 28, 2012

TAARIFA YA SERIKALI KUHUSU KUSUDIO LA WALIMU KUGOMA


SERIKALI kupitia Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi leo, Ijumaa, Julai 27, 2012 majira ya saa tisa alasiri, imepokea notisi ya saa arobaini na nane (48) ya kusudio la walimu wanachama wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kugoma kuanzia Jumatatu tarehe 30 Julai 2012 saa moja na nusu asubuhi.

Kabla ya notisi hii kutolewa, Serikali imekuwa ikifanya jitihada nyingi za kujadiliana na viongozi wa CWT kuhusu jinsi ya kuboresha maslahi ya walimu kwa nia ya kumaliza suala hili kwa maelewano kwa kutumia vyombo na ngazi mbali mbali za kisheria.

Kwa sasa, shauri hili liko Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na leo hii siku ya Ijumaa tarehe 27 Julai, 2012 majira ya saa sita mchana pande zote mbili zilifika Mahakamani, na Mahakama ikaamuru kwamba pande zote zikamilishe maelezo yao ifikapo siku ya Jumanne tarehe 31 Julai, 2012 saa sita mchana, ili kuiwezesha Mahakama kuendelea kusikiliza shauri hilo na hatimaye kutoa uamuzi.

Kwa hiyo, Mgomo huu siyo halali kwa sababu shauri hili bado liko Mahakamani.

Kwa msingi huo hatua ya CWT kutoa notisi ya kuanza kwa mgomo kabla ya kukamilika kwa shauri hili ni kukiuka taratibu halali za Kimahakama ambazo kila mmoja anawajibika kuziheshimu.

Serikali inapenda kuwafahamisha walimu wote kuwa kujihusisha na mgomo huu ni kwenda kinyume cha Sheria, Kanuni na Taratibu za kazi. Hivyo, walimu wanapaswa kupima madhara ya mgomo huu usiokuwa halali na Serikali inawataka walimu kupuuza mgomo huo na kutokujihusisha nao. Walimu wote wanatakiwa waendelee na kazi kama kawaida.



Peniel M. Lyimo
KAIMU KATIBU MKUU KIONGOZI
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
27 Julai, 2012

Tuesday, July 17, 2012

MKUTANO WA WAKUU AFRIKA WAMALIZIKA


Viongozi wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika Jijini Addis Ababa.
Viogozi wa Afrika wakimaliza mkutano wa 19 wa kawaida wa Umoja wa bara hilo makao makuu ya Umoja huo jijini Addis Ababa. Pamoja na kumchangua kiongozi mpya mtendaji bi Nkosazana Dlamini-Zuma, ambaye anakuwa mwanamke wakwanza kuuongoza umoja huo, viongozi hao wamekubaliana pia kuangalia na kuifanyia kazi migogoro mikubwa miwili inayoendelea barani humo. Mgogoro ule wa kaskazini mwa Mali na ule wa Mashariki wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Kiongozi mpya wa Umoja wa Afrika
bi Nkosazana Dlamini Zuma picha kwa hisani ya blogu wadau

Mama Nkosazana Dlamini Zuma akifurahia jambo. Picha na wadau