Wednesday, October 5, 2011

Siku ya Walimu duniani












Picha zote katika makala hii ni kwa hisani ya google
Oktoba, 5 ni siku ya walimu duniani. Siku hii ambayo kimataifa imeanza kusheherekewa 1994, ina malengo hasa ya kuikumbusha jamii ya wanadamu kuwa walimu ni muhimu kwa maendeleo ya jamii zetu na kwa dunia kwa ujumla. Ni fursa nzuri kuwakumbuka walimu ambao wamechangia sisi wote kuwa hapa tulipo.

Walimu ndio chanzo cha mafanikio katika kila sekta, kila mtaalamu, katika hali ya kawaida, huhitaji mwalimu wa aina yoyote ile ili kujifunza, kuboresha alichonacho ama kujifunza zaidi na kuwa imara zaidi. Kwa hivi hata wale wenye vipawa maalumu bado ni lazima wapate maongozo ya namna flani. Kwahiyo kimantiki, mwalimu inatakiwa awe ni mtu mwenye uwezo mkubwa sana kiakili, uwezo mkubwa wa kuwafundisha wengine na si kinyume chake. Na zaidi tunahitaji walimu wengi ili kutoa ujuzi kwa watu wengi zaidi. Vigezo hivi muhimu vyatulazimisha watanzania kutafakari kwa kina mahitaji yetu ya walimu na ubora wao.















Kwa Tanzania, tunaungana na jamii ya kimataifa kusheherekea siku hii adhimu kwa jamii ya wanadamu. Ni muhimu kwa kuwa kila mmoja wetu ana mwalimu ama walimu wake ambao kamwe hawezi kuwasahau kwa jinsi walivyomsaidia na kumjenga kitaaluma, kiutu, kijamii na kadhalika.

Kama tulivyoona hapo juu, mwalimu ni mtu mwenye (anayepaswa kuwa na) mafunzo ama ujuzi maalumu kwaajili ya kuwafunza na kuwasaidia wengine. Mtu mwenye kufanya hizo inafaa awe na uwezo mkubwa wa kuelewa na kuwasilisha ujuzi huo kwa watu wengine. Ujuzi na uwezo wa mtu, kwa bahati mbaya sana, mpaka hivi sasa hupimwa kutumia vyeti alivyonazo. Vyeti hivyo huonesha matokeo ya mitihani mbalimbali ambayo mtu huyo alifanya; binafsi siamini njia hii ya namna ya kupima uwezo wa mtu, nakumbuka HakiElimu waliwahi kusema elimu sio cheti bali uwezo. Kurejea kwenye mada yetu, swali hapa ni je, walimu wetu Tanzania wana sifa zipi na ni namna gani huwapata?

Sina rejea sahihi kuhusiana na uwezo wa Mwalimu Julius Nyerere, ila simulizi za walimu wangu shuleni zinaonesha(hapa ni uvivu wa kufanya utafiti) kuwa alikuwa mwanafunzi hodari ndio maana akasomea ualimu. Mwalimu wangu darasani aliniambia kuwa huo ulikuwa ni utaratibu wa kikoloni kuwa wanafunzi wenye uwezo mkubwa darasani wanakwenda kusomeshwa ualimu ili wafundishe wengine. Utaratibu huu ulikuwa na mantiki na maana kubwa sana. Mtu anataka kuwa mwalimu awe ni yule aliyefaulu vyema sana katika masomo yake, kwa kutumia vyeti, tuchukue wanafunzi wenye daraja la kwanza na la pili.

Na kwa taaluma zingine, ambazo pia ni muhimu kama vile utabibu, uhandishi, sheria, wanasaikolojia n.k kuwe na utaratibu utakaofaa; wanafunzi wote wakifundishwa vyema na walimu wenye uwezo mkubwa basi madaraja yoyote kuanzia la kwanza hadi la tatu yanaweza kutoa wataalamu wenye sifa takikana kabisa. Kwa hali ilivyo hivi sasa baadhi ya watu hapa Tanzania waidharau taaluma ya ualimu, kiasi cha kushauri mwanafunzi aliyefanya vibaya mitihani kusomea ualimu. Sasa hii, si sawa, kwa kuwa mwanafunzi ambaye hana uwezo wa kutosha kuelewa inawezekana kabisa akawa na uwezo mdogo wa kuelewesha wengine. Kwa hivi basi kuna haja ya kuangalia kwa makini namna tunavyowapata walimu wetu wa baadaye ili kupata  kuwa na uhakika wa kupata wanataalamu wa fani zingine waliofunzwa na walimu wenye ujuzi na uwezo wa kufaa kuwapatia elimu hitajika. Kinyume na hapo tutapata wataalamu wasioiva sawasawa ni muhimu sana.

Ili wanafunzi wanaofanya vyema waweze kwenda kusomea ualimu na kufunza ni muhimu wakapatiwa motisha ili kuwahamasisha. Ni muhimu kufanya hivyo kuwa kila binadamu ana uhuru wa kufanya aonavyo muhimu ili mradi tu hadhuru ama haathiri haki za wengine. Kuwe na utaratibu na sheria ya namna ya kuwafanya wanafunzi waliofanya vyema zaidi kwenda kusomea ualimu. Hiyo inaweza kuwa moja ya malengo ya kimaendeleo ya taifa hasa wakati huu ambapo hapa nchini kuna shule nyingi kama zilivyo kata. Ili kuepuka kuendelea kuwa na takwimu kubwa ya shule bila ubora stahiki basi hilo tuliangalie.
Shule ya Tusiime Picha na google












Sifa stahiki za walimu zinatupeleka kwenye sifa stahiki pia kwa shule zetu. Serikali ya Tanzania imepiga hatua kubwa kwenye sekta ya elimu, japokuwa, bado kuna mengi yanatakiwa kufanyika. Kuwa na shule kila kata ni hatua nzuri mno ya kimaendeleo, lakini aina gani ya shule ni muhimu zaidi kwa kuwa shule inaweza kuwa ni ukombozi ama utumwa. Mwanafunzi aliyefunzwa vyema yeye na jamii yote ya wanadamu itakuwa imekombolewa ilhali yule asiyefunzwa barabara atakuwa mzigo mkubwa kwa jamii; kwa vile atatazamwa kama aliyekombolewa na elimu. Mtu aliepata elimu katika mazingira duni ya kitaaluma ni mtu aliyeelimika nusunusu, mtu mwenye elimu nusunusu ni hatari kweli katika jamii kwani anaweza kuutumia, ashalkumu si matusi, umbumbumbu wake kuleta madhara akidhani kuwa anatoa msaada kwa jamii. Kwa hiyo wito hapa ni kuboresha walimu na mazingira yao ili wafanye kazi kwa uzuri na hivyo kuwa chachu kwa maendeleo ya taifa lote.

Thursday, September 29, 2011

Vijana wa CCM na CHADEMA


Picha kwa hisani ya mmiliki-Mtwara















Hawa ni vijana na wanafunzi; wataalamu wa leo na baadaye. Wana uwezo na nguvu nyingi zinazo hitaji kuelekwezwa sehemu sahihi kinyume na hapo ni maafa. Vijana kwa asili yao ni watu motomoto. Wana nguvu na hazina nyingi miilini na akilini mwao ambayo wanahitaji kuvifanyia kazi ili nguvu hizo ziwe na manufaa kwa jamii ya wanadamu.

Ili waweze kufanikiwa kuzitumia nguvu zao vyema ni lazima wapatiwe mafunzo ili watambue namna ya kuzigundua na kuzitumia vyema nguvu hizo; leo hii kuna AZAKI nyingi zinazotoa STADI ZA MAISHA kwa vijana.


Hilo ni jambo jema kwani bila kufanya hivyo huweza kuzitumia nguvu hizo vibaya. Wakitokea waharibifu wachache wenye kutambua vyema nguvu nyingi walizonazo vijana, huweza kuwaharibia kabisa  malengo yao ya maisha bila huruma. Hivi leo hapa Tanzania kwa sababu kadha wa kadha, baadhi ya vijana wanaingia kwenye Siasa kwa malengo ya kusaka ajira; siasa kwao ni ajira. Siasa, na hasa Siasa Safi (JK.Nyerere) ni muhimu na lazima kwa maendeleo ya watu. Lakini siasa isipokuwa safi ndipo hapo utasikia vijana wamefanya vurugu zilizohamasishwa na itikadi za kisiasa. Bila kuvurugwa na makundi ya wabinafsi wachache wenye kulenga kujinufaisha kupitia nguvu kazi na akili ya vijana, kundi la vijana ni hazina kuu kwa taifa lolote duniani, na halina haja ya fujo.Hayo yamedhihirishwa na makala hii ya Habari Leo: Vijana Chadema, CCM hawataki vurugu Igunga


MWANAFUNZI BORA


                                          Imepakuliwa hapa :https://www.youtube.com/watch?v=Y1JhL9FTA8Y                
Hapo juu wanafunzi wa moja ya shule za msingi hapa Tanzania. Mwanzo kabisa wa safari ndefu ya miaka kadhaa... wana mahitaji mengi kufanikisha ndoto zao.

Mwanzoni mwa mwaka huu shirika binafsi la HakiElimu lilitoa shindano la kuandika sifa za mwanafunzi bora. Shindano lilimtaka mshiriki aandike insha ama achore picha juu ya mada hiyo. Hatimaye hivi leo mshindi amepatika; unaweza kusoma mada hiyo kwenye Habari Leo Hapa  chini ni moja ya insha zilizoshiriki shindano hilo:

Mada hii ni muhimu kwa kuwa ni mwanzo wa maendeleo ya nchi yoyote duniani. Mwanafunzi mwenye sifa bora hufanya vyema katika masomo yake na kupata ujuzi wa aina fulani wenye manufaa kwa nchi. Mwanafunzi mwenye sifa bora hufaulu vyema masomo yake na kufaulu kwake ni lulu kwa nchi kwani kupitia ujuzi na weledi wake katifa fani aliyonayo huchangia katika maendeleo ya taifa lake.

Mwanafunzi ni mtu anayetafuta elimu ama maarifa fulani . Kwa kawaida mtu huanza kupata elimu toka utotoni. Ni vyema ikawa hivyo kwa kuwa mtoto anapokuwa mdogo ana uwezo mkubwa kwa maana ya wepesi wa kujifunza na kuelewa mambo mengi mapya kwa urahisi zaidi. Wakati wa umri mdogo mtoto anahitaji uangalizi wa karibu kabisa wa mzazi/ mlezi wake. Uangalizi huo ni vyema ukaangalia pia suala kujifunza kwa mtoto. Hivyo kujifunza kwa mwanafunzi wakati angali na umri mdogo ina maana kuwa huwahusisha pamoja naye mwenyewe, mwalimu, mzazi/mlezi, na familia yote kwa ujumla wake. Pamoja na hayo yote kuna vigezo na mazingira ambayo ni muhimu kwa mwanafunzi kuweza kutafuta maarifa kwa usahihi zaidi.

Ili mwanafunzi aweze kufanya vyema katika masomo yake na hivyo kuweza kuchangia katika maendeleo ya taifa lake na ya jamii yote ya wanadamu kwa ujumla wake, mara baada ya kupata ujuzi, ni lazima awe na sifa kadhaa. Sifa za mwanafunzi bora ndio hasa mada ya insha hii. Mwanafunzi bora anatakiwa awe na aina mbili ya sifa. Awe na sifa za ndani na za nje; nitazielezea kwa unagaubaga hapa chini.

Sifa za ndani ni za kimaumbile, hizi ni zile ambazo binadamu anazaliwa nazo. Hafanyi chochote kuzipata ni zawadi ya uumbaji na ni sifa za lazima kabisa; nazo ni akili na utashi. Akili ni ule uwezo wa kupokea, kuzisoma na kuzitafsiri taarifa zote toka nje ya mwili wa binadamu. Utashi ni ule uwezo wa binadamu kuamua kufanya jambo moja ama jingine baada ya utashi huo kupewa na akili taarifa zote zihusianazo na jambo fulani kabla ya kulifanyia maamuzi. Akili inampatia mwanafunzi uwezo wa kujifunza mambo mapya na kuyatunza kama ujuzi; hivyo ni jukumu la mwanafunzi, kupitia utashi, kuamua kujifunza. Sifa hiyo inatufikisha kwenye utashi; kazi ya utashi ni kuamua kufanya hili ama lile kisha kupewa taarifa zote muhimu. Hivyo basi, kwa sifa hii, mwanafunzi ana hiari ya ama kujifunza ama kutojifunza.

Sifa za nje za mwanafunzi bora ni usikivu, udadisi, heshima na matumizi sahihi ya ujuzi alioupata. Kijana wa kike ama wa kiume ili aweze kujifunza vyema hana budi kuwa msikivu. Asikilize kwa makini maagizo ya mzazi/mlezi nyumbani, mafunzo ya mwalimu shuleni na ni vyema pia milango yake yote ya fahamu ikawa na usikivu ili maarifa mapya yapatikane. Picha ya mtu mwenye masikio makubwa inaweza kuwakilisha twasira ya mwanafunzi mwenye usikivu.

Udadisi; hali ya kutafuta jambo kwa kuulizauliza . Kwa hakika hii ni sifa muhimu kwa mwanafunzi bora. Pamoja na kufundishwa na mzazi/mlezi nyumbani na mwalimu darasani, mwanafunzi mwenyewe inamlazimu ajifunze kutafuta elimu, mambo mbalimbali juu ya mafunzo yake bila ya kuwa tegemezi kwa mwalimu tu. Mwanafunzi mdadisi anaweza kuomba na kujiunga uanachama katika maktaba mahalia kwa lengo la kusaka mambo mbalimbali kwa kina zaidi.

Heshima, thamani ya utu, adabu ; hii ni sifa nyingine muhimu kwa mwanafunzi bora. Sifa hii humfanya mwanafunzi awe mwenye mahusiano mazuri na wazazi /walezi na walimu wake. Mahusiano mazuri ni kigezo na kichocheo cha muhimu cha udadisi na kujifunza. Mwanafunzi mwenye mahusiano mema na mwalimu wake hana hofu kuuuliza ama kutoa maoni yake juu ya mada fulani darasani.

Matumizi sahihi ya ujuzi alioupata. Mwanafunzi bora, si yule mwenyekukariri kila afundishwacho na kwa kurudia aliyoweka kichwani hupata alama nzuri katika mitihani, bali ni yule mwenye uwezo wa kutafsiri nadharia na masomo yake kwenda kwenye vitendo halisi. Mfano, kwenye somo la Sayansi kimu, mwanafunzi anajifunza juu ya utunzaji wa vyakula; swala hilo anaweza kulifanya kuwa kitendo halisi kwa kuwashirikisha wazazi wake kama simulizi inayoweza kufanyiwa kazi na hivyo kuipatia familia mbinu ya kuhifadhi chakula.

Kuhitimisha insha hii; wazazi/walezi na walimu wao pia wana majukumu makubwa juu ya wanafunzi wao. Kubwa na muhimu zaidi ni kuwajengea mazingira ya kujifunza na kuwatia shime ili wawe na hamu ya kuzitumikisha sifa zote za ndani na za nje. Akili, utashi wa kujifunza, usikivu, udadisi, heshima na matumizi sahihi ya ujuzi mpya ni sifa za mwanafunzi bora. Sifa hizi huleta matokeo mazuri mno pale zinapopatiwa mazingira na fursa sahihi na hiyo huweza kudhihirisha uwezo wa mwanafunzi bora.

Thursday, September 15, 2011

Chanzo cha Mapato kwa Wananchi

Hii ni sehemu ya soko la Samaki mkoani Mtwara.
Hapa ni sehemu samaki wanapochuuzwa mara  baada ya kuvuliwa.



Biashara ya samaki ni moja kati ya maeno yenye kutoa ajira kwa wananchi wengi wa kawaida hususan kina mama. Hii ni shughuli ambayo huwapatia wananchi wengi pesa za kuweza kuendesha maisha yao na pia huweza kuchangia pato la taifa kwa kulipa kodi hata kama ni kiasi kidogo.

Hivi karibuni nilitembelea soko hilo kujionea jinsi lilivyo na kuangalia uwezekano wa kujipatia kitowewo. Hali niliyoikuta sokoni hapo si ya kuridhisha sana. Soko la bidhaa hiyo muhimu kwa afya ya binadamu si nzuri kiafya. Hata hivyo nilipouliza kidogo wachuuzi sokoni hapo niliambiwa kuwa kuna mikakati na ujenzi wa soko la kisasa tayari umekwishaanza. Hivyo kuna matumaini ya kupata sehemu nzuri zaidi siku za usoni.

Hii ni sehemu ya muendelezo wa soko letu la samaki mjini Mtwara, wahusika wameliona na hivyo wanaendelea kuliboresha...



Bila shaka mazingira safi ni muhimu kwa akili safi... ni muhimu marekebisho yafanyike haraka... bila shaka tutahitaji soko la kisasa kama pale Magogoni...

Wednesday, September 14, 2011

Clouds Fm hongereni lakini...


Hiki ni kivuko kinachotoka Mtwara kwenda Msanga Mkuu.
Picha inaonekana kwa mbali kiasi; vitu unavyoona vya rangi ya pinki vikipepea ni maboya ya kuokoa maisha. Unaonaje yavaliwe wakati gani?

Kituo cha redio (Mawingu) Clouds Fm cha jijini Dar es Salaam, kimeanzisha mkakati wa kuchangia ununuzi wa maboya ya kuoa maisha-mkakati huo umepewa jina la "OKOA MAISHA"  Maboya hayo "life jackets" hutumika kuokoa maisha ya abiria endapo ajali ya majini itatokea. Maboya hayo huvaliwa na abiria kwenye ndege-ili kwamba chombo hicho kikiangukia majini, husaidia kuoa maisha ya abiria, vazi hilo hutakiwa kuwepo pia kwa chombo chenye kusafirisha abiria majini. Clounds wanapiga la mgambo ili kusaidia wasafiri majini. Kwa hili binafsi nawapongeza sana. Hata hivyo kuna mambo mawili hapa ya kutafakari si tu wa mpiga mwano huu bali ni kwa watanzania wote.

Mosi, binafsi natambua kuwa kwenye ndege maboya hayo, kwa kawaida, huwatosha abiria wote; kila abiria anakuwa na life jacket chini ya kitivchake. Na hivyo kikitokea kile ambacho katu hakitamaniki, bali kila abiria hupata kutumia boya lake. Nimesafiri mara mbili kwa maji toka Dar es Salaam kwenda Zanzibar, binafsi sikumbuki “boya langu” lilikuwa wapi. Kwa kusema hivi sina uhakika je, kila abiria kwenye vyombo vya maji hapa Tanzania, ana uhakika wa kupata boya lake ama, je idadi ya maboya inalingana na idadi ya abiria chomboni?

Swala la pili ni juu ya muda wa kuvaa boya hilo. Nilipokuwa mwanafunzi kule Uganda, nilipata nafasi ya kutembelea wafungwa kwenye gereza lililo kisiwani katika mji wa Jinja. Kwenda gerezani, chuo nilichosoma kiliweka utaratibu wa kila mwanafunzi kuvaa boya lake pale anapokuwa chomboni. Hi ili wanafunzi wasafiri kwa usalama na uhakika zaidi. Tunaweza kuanzisha utaratibu kama huo pia, kila abiria avae boya “life jacket” pale tu anapoingia chomboni. Najua utaratibu huu utazua hofu kwa abiria na wamiliki wa chombo.

Abiria, akivaa boya la kuokoa maisha, atajihisi kama anaingia kwenye ajali moja kwa moja na ataona kama anajiombea dua baya kwa kufanya hivyo. Mmiliki wa chombo atahisi kuwa abiria wataondoka ya maboya yake na safari inayofuata hakutakuwa na boya hata moja. Tukitaka kufanikiwa lazima tubadilishe tamaduni zinazobadilika.

Tuvae maboya mara tunapoanza safari majini; kwa kufanya hivyo ndo tutakuwa tunajali maisha hofu za kimazingaombwe kamwe haziwezi kutusaidia. Mmiliki wa chombo majini, aweke utaratibu wa kukusanya maboya mwisho wa safari; kila aingiaye chomboni apate boya na kila anapotelemka akabidhi, kama hana alipe gharama ya boya hilo hata kama hakuvaa. Kuokoa maisha ni lazima tuwe wabunifu, makini lakini pia wakali kwenye utekelezaji. Utaratibu huu kwa kiasi fulani unafanyika pale kituo cha mabasi, Ubungo, Dar es Salaam.(Kukagua abiria kama wamefunga mikanda)

Mandalu

Uzembe ukipungua ajali pia zitapungua !

Google Image
                                          Inapakiwa hapa https://www.youtube.com/watch?v=MpzE7flW9_A
Wakati tukiendelea na tafakari juu ya ajali ya meli kule Nungwi ni wasaa mwafaka kwa watanzania na wanadamu wote kwa ujumla na hasa wenye kutumia vyombo mbalimbali kusafirisha binadamu wennzao, iwe ni vya ardhini, majini ama angani, kuwa waangalifu zaidi. Ajali ya meli ya abiria LCT Spice Islanders, iliyokuwa ikitoka Unguja kwenda Pemba, imesababisha vifo vya ndugu zetu wengi. Ni msiba mkubwa kuona watu wengi wenye afya njema na ambao ni  nguvu kazi muhimu kwa ujenzi wa Taifa, wakiaga dunia.Tunamwomba Mwenyezi Mungu kwa huruma yake awapokee ndugu hawa kwenye makazi ya kudumu, na wafiwa na wajeruhi wote wapate faraja na kupona haraka! Kutokana na tukio hili serikali na wananchi wote kwa ujumla wetu tunapenda kuona wamiliki vyombo vya kusafirishia abiria, mamlaka za kudhibiti vyombo vya usafiri na wasafiri wenyewe wakiongeza umakini...

Tuesday, September 13, 2011

Vijana na Mabadiliko

Makala ya Mwandishi Ahmed Rajab; Vijana wa Afrika wanawaperemba tu viongozi... imejaa mambo anuai ambayo yana manufaa mengi kwa kijana mwenye malengo ya kuchangia katika jamii yake.

Mwandishi anaongelea mwamko mpya wa vijana barani Afrika katika kudai haki za jamii zao, aidha anatoa picha ya jinsi viongozi wabadhilifu wanavyo tumia vibaya mali za umma kwa manufaa binafsi.

Monday, September 12, 2011

Tandahimba Pia


















Sekondari ya Milongodi ilikuwa na walimu wetu pia. Hapa mkuu msaidizi wa shule hiyo akitushirikisha jambo kuhusu sekondari hiyo ambayo ingali ikikuwa kabisa.

Katika shule hii kidato kimoja kina wanafunzi wa kiume tu bila binti hata mmoja, Zaidi ya hayo walimu, kama ilivyo katika shule nyingine nyingi, ni wachache mno. Kwahiyo, walimu mafunzoni ilikuwa ni ukombozi mkubwa kwa shule nyingi za wilayani Newaala na Tandahimba, mkoani Mtwara. Pengine muda wa mazoezi uongezwe, ili huduma hiyo iendelee kwa muda mrefu zaidi? Tutawauliza walimu hawa mafunzoni.

Walimu mafunzoni

Nilipata fursa ya kukutana na walimu-mafunzo
sekondari ya kutwa Newala mjini

Alaa kumbe ni NEWALA !














Hapa nikijiandaa kuanza safari asubuhi na mapema- mjini Newala! Picha na Eric Wamalwa

Nipo wilayani Newala. Hii ndo wilaya ya kwanza kuandikishwa hapa Tanzania, ni moja ya wilaya tano za mkoa wa Mtwara. Wilaya hii, kama jinsi ilivyo kwa maeneo mengine, ina mahitaji ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kuna makundi yote ya lazima katika jamii; watu wazima, vijana, na watoto.

Kijamii; maji ni shida (jamii imejenga utamaduni wa kuvuna maji ya mvua: karibu kila familia ina mikingio maji kwaajili hiyo – huu ni utamaduni wa kuigwa hasa na sehemu zenye mvua za kutosha. Maji hayo ya akiba yaweza kuwa na matumizi kedekede. Mfano kumwagilia bustani za mboga mboga, kuanzisha mabwawa ya samaki n.k )

Elimu: wilaya ina shule kadha wa kadha; karibu kila kata ina shule yake. Hili ni moja ya mambo mazuri ya serikali iliyopo madarakani. Ni vyema kuwa na shule za kuweza kuandikisha wanafunzi wengi iwezekanavyo. Vijana wengi wakiandikishwa shule za sekondari ndo hasa mwanzo mzuri na wa uhakika wa kupiga vita umasikini kwa vitendo. Hata hivyo mtaala wa elimu uzingatie mfumo wenye vitendo zaidi kuliko nadharia kama ilivyo hivi sasa. Vijana wetu wengi wakimalima masomo yao, kwa mfumo tulio nao hivi sasa, hulazimika kusubiri ajira. Mfumo unaofaa ni ule wa kumuandaa kijana ili aweze kujiajiri; hilo hasa ndo liwe lengo la elimu yetu. Tukirejea mada yetu; shule nyingi huko Newala zina watenda kazi wachache sana.

Shule kadhaa zina walimu wawili, watano, sita, nyingi zina idadi isiyozidi walimu kumi. Hii ni changamoto kuu na kubwa mno katika sekta ya elimu. Wanafunzi wanapokuwa na walimu wa kutosha ndo inawarahisishia kujifunza kwa ufanisi zaidi. Kwa walimu wakiwa na wanafunzi kiasi, kwao inakuwa ni vyema zaidi katika utendaji kazi wao.

Ukosefu nyumba za walimu; shule nyingi za kata zipo vijijini hasa, ni sawa kwani huko ndiko wanapoishi wananchi na watanzania wengi zaidi. na vijiji vyetu vingi havina huduma kwa wageni hususani nyumba za kulala wageni. Ukosefu nyumba za kulala wageni vijijini unakwamisha hata wakaguzi na wataalamu wa kada zingine kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi. Shule nyingi hizi za kata ama hazina nyumba za kutosha kwa walimu ama hazina kabisa nyumba hizo. Ni kweli walimu waliopo katika shule hizo ni wachache pengine inajieleza sawa pia kutokuwa na nyumba kwa walimu. Kuwa na nyumba za ziada kwa walimu inaweza kuwa ni fursa ya kuwavutia walimu wageni, ambao wengi wafikapo kujitambulisha na kuona mazingira ya shule hugoma kurejea shuleni huko.

Kisiasa: Newala ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hivyo huko pia kuna mfumo wa vyama vingi vya kisiasa lakini wakazi wa huko wanaishi kwa amani na undugu. Hata hivyo hii ni tathmini yangu ya juma moja tu.

Kiuchumi: zao la korosho ni uti wa mgogo wa uchumi wa wilaya hiyo; wakazi wengi hujihusisha na kilimo cha zao hilo la msimu na lenye kuhitaji matunzo ya karibu hasa. Kwa wananchi wanaoweza kufuata vyema maelekezo ya wataalamu wa kilimo hujipatia mavuno na pesa nzuri kutokana na kilimo cha zao hilo. Hata hivyo mkulima siku zote huchukua tu bei inayopangwa sokoni na watu wengine; yeye hufanya kazi ngumu ya kutunza shamba na kufuatilia ukuazi wa korosho hadi kuwa tayari na kisha hapo watu wengine wenye “utu” zaidi ya mkulima hukaa meza na kupanga bei ya zao hilo kama ilivyo kwa mazao mengine ya wakulima wetu maskini hapa Tanzania na sehemu nyingi nyingine barani Afrika. Siku moja tufikie hatua ya kupanga bei ya mazao yetu wenye kwenye hilo soko la dunia; hii ni mantiki zaidi kwa kuwa wakulima wetu ndio wanafahamu haswa gharama za kilimo.

Ajira za vijana: Vijana kundi lenye nguvu na msukumo mkubwa wa maendeleo ya wakati uliopo na ujao katika jamii. Nikiongea na vijana kadhaa wa mjini Newala niligundua kuwa kuna idadi kubwa ya vijana wa kitanzania wanofanya shughuli za kiuchumi, hususan biashara nchini Msumbiji. Newala ni wilaya ya mpakani kabisa na Msumbiji. Upande wa kaskazini ya Msumbiji haujapiga hatua kubwa kimaendeleo na hivyo kutoa fursa nyingi kwa watafuta mali: hivyo vijana wetu hupitia huko na kufanya biashara za bidhaa anuwai. Vijana niliongea nao, wanijuza kuwa vijana hao wa kitanzania huko, hususani wale wenye bidii ya shughuli zao, ni wenye mafanikio makubwa.

Nyumba za kulala wageni chache: wilaya hii ina nyumba chache za kulala wageni. Upungufu huo hivyo unatoa fursa za kiuchumi kwa wananchi kujiimarisha kiuchumi na hivyo kujiongezea pato na pia kuongeza pato la taifa kwa ujumla.Kuna changamoto lakini pia fursa anuwi za kujiimarisha kiuchumi, kujiondoa kwenye umasikini na kuchangia kwa pato jumla la taifa.



Tuesday, August 23, 2011


Baadhi ya wadau wa Vijana tukisimama kwa picha ya pamoja

Wadu wa Vijana

Hapa ni Moro nikiwa na wadau wa vijana.
Hawa ni wadau toka mikoa mbalimbali waliokutana kujadili masuala ya afya ya uzazi na maendeleo ya vijana kwa ujumla.

Picha kwa hisani ya kiongozi wa mradi wa masuala ya vijana wa fhi









Saturday, August 20, 2011

Vijana Maji Moto

Picha kwa Hisani ya mtandao
Hivi karibuni tumeshuhudia harakati kubwa za vijana sehemu mbalimbali duniani. Harakati hizo zimekuwa na dhima na vyanzo tofauti tofauti. Harakati za vijana mashariki ya kati na Afrika kaskazini zilisababishwa na kukosa mahitaji yao muhimu hususani kukosa nafasi za kazi na kutokuwa na uhakika wa mustakabali wa maisha yao. Giza hilo kwa mustakabali wa maisha ya vijana ulisababishwa na ubinafsi wa viongozi wa nchi hizo. Kiongozi wa Tunisia, Ben Ali amekuwa madarakani kwa muda mrefu na amejikusanyia mali nyingi mno na hivyo kuharibu matumaini ya vijana na wananchi wake kwa ujumla. Hali kadhalika, Misri, Libya, Yemen na kwingineko mashariki ya kati.

Vijana wa Uingereza wao nao walisababisha fujo ama varangati (Kiswahili cha kizamani) lakini wao sababu ilikuwa tofauti. Makala ya mwandishi kutoka London Macha, inatoa sababu ambazo zinawapambanua vijana wa Uingereza na wale wa Mashariki ya kati. Wachambuzi wengine husema kuwa vijana wa dola hiyo kuu zamani, wanafundishwa tu/ ama zaidi juu ya haki zao, hawafahamu kuhusu wajibu wao kwa jamii. Hili ni tatizo kubwa. Vijana wanapokua ni vyema tukawajuza haki zao, lakini muhimu kabisa watambue pia namna ya kuwajibika kwa jamii zao. Hili ni jambo la kila mahali Tanzania na nchi nyingine zote duniani, na tena muhimu kwa wananchi na pia serikali kutoa mchango wo kwa maendeleo ya vijana.

Tanzania kuna asasi zisizo za kiserikali (AZAKI) lukuki zinazojihusisha na masuala ya vijana. AZAKI hizo zimeanzishwa na wananchi kwa malengo lukuki, ikiwa ni pamoja na kuwahudumia vijana. Hili ni jambo jema kwani vijana ni moja ya makundi yaliyo muhimu kwa maendeleo ya jamii ya wanadamu. Hata hivyo katika siku za nyuma kidogo kulizuka AZAKI nyingi ambazo hazikujali masilahi ya walengwa husika bali waanzilishi kujijaza mapesa.

Serikali yetu Tanzania, imepiga hatua kubwa hasa kwa kuwa na utashi muhimu wa kisiasa na kuazisha shule za sekondari kila kata. Bila ubishi hii ni hatua kubwa sana ya kuelekea maendeleo ya kweli. Elimu mwanzo wa ustaarabu wote duniani; elimu kwa upana wake si tu ile ya darasani. Hata hivyo changamoto kubwa kwa serikali ya Tanzania na wananchi wake kwa ujumla wao ni kuziboresha shule hizo lukuki za kata. Ni muhimu kufanya hivyo kinyume na hapo tunapata taifa la watu walioelimika nusu nusu. Hii elimu nusu ni hatari sana, pengine afadhali asiyeipata kabisa; mwenye elimu nusu hatokubalika katika kundi la wajinga kabisa kwani ana maarifa kiasi na hivyo kuwa tofauti na wasiosoma kabisa, lakini hawezi changamana pia na walioiva vilivyo kielimu kwake itakuwa ni kujinyanyapaa – “kujichora” (maarufu kwa vijana) mbele ya wasomi. Ni hatari kama nusu wasomi hawa watakuwa wengi; watadai haki kwa njia zisizokubalika kwani elimu yao yawatuma hivyo.

Hivyo AZAKI zilenge kuwasaidia vijana wapate stahili yao. Wananchi wote kwa ujumla na serikali kwa maana ya dola tujipange kuziboresha shule hizi haraka iwezekanavyo kama inavyoelezewa kwenye MKUKUTA II ili kuepukana na nusu wasomi na matatizo mengi toka kwa vijana wetu siku zijazo.

Wednesday, August 3, 2011

Familia Inafaa - Families Matter Program! FMP

Hapa nikiwa na mratibu wa Mradi wa Familia Inafaa huko mkoa wa Ruvuma. Wanakikundi ni wadau wa Familia Inafaa katika mkoa wa mashujaa wa kingoni, nyumbani kwa simba wa vita 



Hapa nikiwa na raia wa siku nyingi hapa Tanzania. Mzee huyu ananipatia somo juu ya malezi kulingana na uzoefu wake wa siku nyingi duniani hapa- asante mzee! 



      
                                                                                                                                                               Hapa nikiwa na wadau wa Familia Inafaa mkoani Mtwara; hapa ni kijiji cha Nanguruwe Mtwara Vijijini!


Familia Inafaa – Families Matter Program! (FMP)













Huu ni mradi unaongozwa na Kampuni ya T-MARC. Mradi huu unawalenga wazazi, walezi na wadau wa malezi ya watoto ambao bado hawajabalehe kwa wavulana na hawajavunja ungo kwa mabinti. Familia Inafaa! Ni mradi ambao tayari umeshaanza kutoa huduma kwa wazazi na walezi wa mikoa ya Mtwara na Ruvuma.
• Lengo la msingi kabisa la FMP ni kuwatia shime wazazi katika juhudi zao za kuwalea watoto wao ili wakue katika afya njema.

• FMP ni program mahususi kwa ajili ya wazazi. Imeandaliwa katika namna ambayo inawasaidia wazazi kutumia mbinu ambazo zinaweza kuwalinda watoto wao dhidi ya tabia hatarishi za afya ya jinsia, hivi sasa na wakati ujao pia.

• FMP inaamini kuwa wazazi wana nafasi yenye ushawishi mkubwa wa kujenga, katika namna chanya tabia za kiafya za watoto wao.

• Lakini hata hivyo ushawishi huo ni lazima ushindane na ujumbe wanaoupata watoto wao toka kwenye vyombo vya habari, vijana wenzao, na jamii yote kwa ujumla.

• Mawasiliano ya wazazi yanaweza kuwalinda watoto, kujenga uwezo wa kufanya maamuzi yafaayo, na kufikisha ujumbe sahihi.

• FMP inataka kuwasaidia wazazi “kuongeza ujuzi wao” kwa kuwapatia vifaa na mbinu mahususi kabisa ili waweze kuwa na mtindo bora wa afya katika familia zao.

Saturday, July 23, 2011

Tunu bora ni Msingi wa Maendeleo ya Watu:Je, Za Afrika ni zipi?

Mlima Kilimanjaro - TANZANIA, paa la Afrika, na Twiga, ambao hupatikana kwa wingi nchini Tanzania.
 Bila shaka hizi ni alama muhimu zinazoitambulisha TANZANIA na bara Afrika.
Hivi tunu za Afrika ya leo ni zipi hasa? Tunu za Afrika ya kina Julius Nyerere, Kwame Nkrumah, Patrice Lumumba, Kenneth Kaunda, Houphouët-Boigny, Frantz Fanon, Nelson Mandela, n.k zilikuwa za umoja, kuungana, kushirikiana, uzalendo kwa bara letu, na kufanya kazi kwa bidii. Tunu za leo ni kuhakikisha kuwa kiongozi anashinda uchanguzi kwa mbinu zozote zile halali ama haramu, mashindano ya kujilimbikizia mali kwa wingi iwezekanavyo. Kwa majumuisho ni ushindani wa ubinafsi. Viongozi na raia wanajenga ubinafsi kwa gharama yoyote ile ikiwa ni pamoja na kuzifanya nchi zetu kuwa vyama wanavyoweza kuvitawala kwa mihula mingi wapendayo wenyewe na mashwahiba wao. Nchi zetu nyingi hatujui hasa nini tunataka kukifanya; tuna maandishi, vielelezo na miongozo mingi mizuri lakini isivyofuatwa katu. Jambo tunalopaswa kujiuliza hapa ni je, kwa tunu hizi za kibinafsi bara Afrika linaweza kweli kuwa mshirika wa maendeleo ya dunia?


Afrika, nyumbani kwa watu zaidi ya milioni 900. Bara hili ni mama ya nchi zaidi ya hamsini. Wenyeji wa bara hilo huitwa Waafrika. Waafrika hawa wana asili mbalimbali; waafrika weusi, waafrika wenye asili ya bara asia, waafrika wa asili bara ulaya. Uanuwai huu unalifanya bara kuwa na utajiri wa tamaduni na hivyo kumiliki tunu kedekede. Kufuatia bahari hiyo ya tofauti, utaona kuwa kuna nafasi ya kupata tunu zilizo bora kabisa mithili ya mbegu za kisasa zenye kufanyiwa tafiti katika maabara na mashamba darasa ya wataalam wa kilimo.


Bara Afrika, kisayansi – daktari Leaky, lasemekana kuwa ndio nyumbani kwa binadamu wa mwanzo hapa duniani. Kwa mantiki hiyo bara hili ilifaa liwe limepiga hatua kubwa zaidi kimaendeleo katika nyanja mbalimbali kama vile (kv) kisayansi, kijamii, na kadhalika kuliko ilivyo hivi sasa. Barani Afrika nyanja iliyopiga hatua kubwa zaidi ni ile ya kijamii. Nyanja nyingine zingali nyuma mno. Sayansi na teknolojia, elimu bora kwa ujumla wake vingali nyuma mno.


Uwanda wa masuala ya kijamii umepiga hatua kubwa barani humo. Ni hulka ya wanyama wote, wawe wa mwituni ama binadamu mwenyewe, kuwalea na kuwatunza watoto wao na pia kuishi katika jamii. Utaona kuwa kwenye eneo hili Afrika imepiga hatua kubwa hasa. Jamii nyingi katika Afrika bado huishi pamoja watu, familia kadhaa zinazotengeneza ukoo bado huishi pamoja. Ni jambo la kawaida kwenye familia za Kiafrika kuona ndugu wa mbali kabisa ama msaidizi akiishi na kutendewa vyema kama mtoto wa familia mwenyeji. Ni barani humo ndo kijana wa miaka hata thelathini huendelea kuishi kwa baba na mama akiwa tegemezi kabisa. Tamaduni za sehemu nyingine duniani humtaka kijana wa miaka kumi na nane aanze kujitegemea; ajitenge na aanze kujenga maisha yake mwenyewe. Ndugu wa mbali katu hathubutu kuishi na familia ya mbali naye. Tamaduni zote hizi zina mazuri na mapungufu yake, hata hivyo hii si mada ya leo. Kwa leo tuendelee na suala la sayansi na teknolojia hapa barani.


Kwenye uwanja wa sayansi na teknolojia bara Afrika linashika nafasi mbili muhimu, ya mwanzo na ya mwisho kabisa; hakuna mkaganyiko, nitaelezea:

Kwenye ubunifu, ufikirivu; utengenezaji na matumizi ya bidhaa za kiteknolojia bara hilo li nyuma kuliko mabara yote.

Kwenye matumizi ya bidhaa za kiteknolojia na kwa kuwa jaa la bidhaa duni, dhaifu, mbovu, zenye  kukaribia kuisha muda wake na ambazo hutengenezwa ughaibuni, bara letu laongoza. Umeona, hakuna mkanganyiko wowote bali ni ukweli tupu ila tu wenye kuumiza.

Hivyo katika uwanda huu bara Afrika chini ya viongozi na waafrika wote kwa pamoja tunawajibika kujenga uzalendo wa kulipenda bara hili ili kuleta ustawi na maendeleo ya kweli kwa Waafrika na hivyo kutoa mchango kwa maendeleo ya dunia yetu. Kwenye moja ya mada zilizotangulia tuliona kuwa maendeleo huchangiwa kwa kiasi kikubwa na tunu zilizo mahali husika. Kwa mtiririko huo wa kimawazo basi, tujiulize je, hapa barani Afrika tunu zetu ni zipi hasa?

Aina ya maisha na jinsi mtu anavyoishi, ikiwa ni pamoja na nyanja za kijamii, sayansi na teknolojia, husaidia katika kumuainisha binadamu husika. Waafrika kwa asili yao ni wakarimu, marafiki, wenye uteremeshi, na wenye tabasamu la kweli lililo karibu mno takribani muda wote. Furaha, bashasha juu ya binadamu wengine ni tunu zilizojaa pomoni maishani mwa mwafrika. Kwenye sayansi na teknolojia ili mmoja aweze kupiga hatua kubwa kwenda mbele ni wajibu kuwa na tunu za kujali muda zaidi, kujituma na hata kuwa mtumwa wa muda kwa kupangilia kila jambo linalotakiwa kufanyika, mtu kujali na kupenda kazi aifanyayo na kubwa zaidi uzalendo kwa nchi, na bara lake. Tunu hizi na nyingine zenye kuleta tija kwa kazi ni muhimu hasa kwa kufikia malengo mahususi ya maendeleo. Tunu hizi zipo pia barani Afrika lakini zimefichwa mno mithili ya vinasaba dhaifu visivyo na athari yoyote katika maisha ya binadamu. Kisha maelezo hayo basi ni muhimu mno kuimarisha tunu zinazoweza kuchochea maendeleo ya kweli.

Bara Afrika kongwe kwenye tunu za ukarimu, upendo, undugu, n.k limeishangaza dunia baada ya kutumbukia katika lindi la kuporomoka kwa utu na upendo barani humo. Kwa miaka kadhaa kumekuwa na vita pande nyingi barani humo. Vita nyingi barani humo zimechochewa na sababu nyingi za kibinafsi; uroho wa mali nyingi kupindukia, uchu wa mamlaka, na hata hamu ya utukufu binafsi. Jamii ambazo zilitazamwa kama zenye wema, upendo na utu wa hali ya juu ziliingia kwenye janga la mauaji na kusababisha ulemavu wa kudumu kwa watu wao. Kumekuwa na vita pande zote; kaskazini, kusini, magharibi na mashariki hali kadhalika. Wakati jamii nyingi duniani kote zinaungana, baadhi ya jamii za kiafrika zinatengana, zinawindana na kudhoofishana badala ya kusaidiana kuleta maendeleo kwa watu wao.Tumeona kuwa watu hutambulika na kuainishwa kupitia tunu zao.

Hivi tunu za Afrika ya leo ni zipi hasa? Tunu za Afrika ya kina Julius Nyerere, Kwame Nkrumah, Patrice Lumumba, Kenneth Kaunda, Houphouët-Boigny, Fanon, Nelson Mandela, n.k zilikuwa za umoja, kuungana, kushirikiana, uzalendo kwa bara letu, na kufanya kazi kwa bidii. Tunu za leo ni kuhakikisha kuwa kiongozi anashinda uchanguzi kwa mbinu zozote zile halali ama haramu, mashindano ya kujilimbikizia mali kwa wingi iwezekanavyo. Kwa majumuisho ni ushindani wa ubinafsi. Viongozi na raia wanajenga ubinafsi kwa gharama yoyote ile ikiwa ni pamoja na kuzifanya nchi zetu kuwa vyama wanavyoweza kuvitawala kwa mihula mingi wapendayo wenyewe na mashwahiba wao. Nchi zetu nyingi hatujui hasa nini tunataka kukifanya; tuna maandishi, vielelezo na miongozo mingi mizuri lakini isivyofuatwa katu. Jambo tunalopaswa kujiuliza hapa ni je, kwa tunu hizi za kibinafsi bara Afrika linaweza kweli kuwa mshirika wa maendeleo ya dunia?

Monday, July 18, 2011

Siku ya Nelson Rolihlahla Mandela

Leo Jumatatu, 18 Julai ni kumbukumbu ya kuzaliwa Mzee Nelson Mandela, rais wa kwanza wa Afrika Kusini ya Kidemokrasia (18.07.1918). Kadri ya kumbukumbu zangu huyu ndiye mtu pekee ambaye Umoja wa Mataifa umemtengea siku katika mwaka mahususu kwa heshima yake. Hivi leo anatimiza miaka 93 toka azaliwe; ni mmoja kati ya viongozi wachache wa Afrika ambao wameishi kwa muda mrefu.

Nelson Mandela ni mtu anayepewa heshima kubwa duniani kote kwa wanaomfahamu na hata wasiomfahamu. Watu wengi hasa nje ya Afrika hususani katika jamii zinazopenda kusoma vitabu wamfahamu kupitia kitabu chake cha "Long Walk to Freedom". Hiki ni kitabu kinachoelezea historia ya maisha yake kwa kina kabisa. Sehemu kubwa ya kitabu hicho ameiandika yeye mwenyewe na tena akiwa gerezani. Hili ni moja ya mambo ya kujifunza toka kwa mzee huyu-maktaba kubwa duniani kote. Tujipange tuandike historia zetu sahihi ili kuiachia jamii na dunia kwa ujumla utajiri wa mawazo kama alivyofanya mzee Mandela. Wengine tulimfahamu mzee Madiba toka enzi za utoto; tukiwa shule ya msingi tuliimba nyimbo za kutaka Mandela achiwe huru na serikali ya makaburu. Utawala wa makabulu ulitawala Afrika Kusini kwa mabavu na kwa misingi ya kibaguzi ya rangi za binadamu; ni udhalimu wa aina yake kwa ustawi wa wanadamu.

Kwanini mzee huyu ni maarufu vile?

Saturday, July 16, 2011

Uhuru wa wahadhiri kimawazo

Makala ya Profesa Mbele juu ya uhuru wa kimawazo wa wahadhiri, kwa hakika, imenitia hamu kubwa kuendelea kuijadili. Nadhani ni suala la msingi kabisa kulitazama hasa hivi leo ambapo kuna vyuo vikuu lukuki hapa nchini. Ni muhimu kuupongeza uongozi wa nchi kwa kuruhusu kuanzishwa kwa vyuo vikuu vingi hapa nchini. Vyuo vikuu vingi moja kwa moja vinamaanisha kukua kwa wigo wa fikra nchini. Kuongezeka kwa fikra ni mwanzo wa ugunduzi na kichocheo kikuu cha maendeleo.

Moja ya masuala makuu katika kipindi cha " Scholarsticism" karne ya 12 na 13 ilikuwa ni kuibuka kwa wingi kwa vyuo vikuu vilivyotoa maarifa ya aina mbalimbali. Kipindi hicho Kanisa lilikuwa na mamlaka makubwa hata juu ya kilichofunzwa vyuo vikuu. Matokeo yake kazi za mwanafalsa Aristotle (384—322 BCE) zilikataliwa, hata hivyo kukataliwa huko kulikuwa kwa muda mfupi tu kwani baadaye kazi za gwiji huyo zilianza kufundishwa katika vyuo vikuu na kuboresha zaidi mawazo kwa wanavyuo na wanazuoni.

Kwahiyo basi ni vyema kwa viongozi wa nchi yetu kulitambua hilo na kuwaacha huru wahadhiri wafanye kazi yao, ambayo kimsingi hulenga kujenga wananchi wenye ukomavu wa kujenga hoja na kuzisimamia ili kuendeleza nchi yao na dunia kwa ujumla.

Kupata mawazo zaidi ya Profesa Mbele soma makala hiyo murua kabisa hapa








.

Tuesday, July 12, 2011

MITUME WA BWANA KATIKA MAZIWA MAKUU


Hiki ni kitabu kinachoelezea safari za mwanzo kabisa za wamisionari wa shirika la wamisionari wa Afrika. Shirika hilo la dini lilianzishwa na Kadinali wa Algiers Charles-Martial Allemand Lavigerie wa Ufaransa.

Kwa hivi wengi wa wamisionari hao walitoka Ufaransa na kuja kutangaza neno la Mungu. Hawa walifika eneo la maziwa makuu hasa Afrika ya Mashariki ya leo; hivyo kitabu hiki kinaelezea historia nzuri ya ndugu hao waliofika kwa mara ya kwanza mwaka 1878. Mbali na kutangaza neno la Mungu, kitabu kinatoa pia historia ya Tanzania toka Bagamoyo hadi Kagera.

Maelezo zaidi juu ya historia ya eneo na habari hizo inapatikana hapa:  http://www.africamission-mafr.org/bagamoyo.htm

Thursday, July 7, 2011

KAZI YA TANU NA TANZANIA YA LEO


Viongozi wa TANU
Flag of TANU.svg
Bendera ya TANU
Tarehe 7 mwezi Julai, 1954 (7.7.1954) ni siku ya kuzaliwa kwa chama cha kisiasa kilichosaidia kudai uhuru wa Tanganyika. Tanganyika National Union (TANU) kilikuwa Chama cha kisiasa kilichowaunganisha wananchi wengi wa kawaida wa Tanganyika na kuwa na nguvu ya pamoja kupigania uhuru wao.

Chama hicho kilikuwa na imani na ahadi za mwanachama. Nazipenda hasa ahadi za mwanaTanu. Ahadi hizo kwa hakika inafaa ziwe ndo TUNU za taifa letu la jamuhuri ya muungano wa tanganyika na Zanzibar- Tanzania. Ahadi za TANU ambazo zimeasiriwa na Chama cha Mapinduzi, (CCM), ni mali ya watanzania wote kwa sababu zililenga kuikomboa nchi na wananchi wote kwa pamoja bila kujali itikadi zao za kisiasa, rangi, dini, wala kabila. Chama cha TANU na pia CCM ndani ya mfumo wa chama kimoja kilikuwa ni mali ya waTanzania wote na hivyo basi ahadi hizo za mwanaTANU ni mali ya waTanzania wote.

Hivi leo tunapokuwa katika mfumo wa vyama vyingi ni dhahiri kuwa vyama vya kisiasa vina katiba, imani na miongozo mbalimbali ya kisiasa, hiyo ni vyema kwa ushindani wa kisiasa. Tanzania kama nchi, pmoja na kwamba ina mwongozo mama-Katiba, inafaa iwe na TUNU ambazo zitafuatwa na wananchi wote bila kujali itikadi zao za kisiasa. Ahadi za mwanaTANU zinaweza kutufaa sana.

AHADI ZA MWANATANU

(1)Binadamu wote in ndugu zangu na Afrika ni moja

(2) Nitaitumikia nchi yangu na watu wake wote

(3) Nitajitolea nafsi yangu kuondosha umaskini, ujinga, magonjwa na dhuluma.
(4) Rushwa ni adui wa haki, sitapokea wala kutoa rushwa.
(5) Cheo ni dhamana, sitatumia cheo changu wala cha mtu mwingine kwa faida yangu.
(6) Nitajielimisha kwa kadri ya uwezo wangu na kuitumia elimu yangu kwa faida ya wote.
(7) Nitashirikiana na wenzangu wote kujenga nchi yetu.
(8) Nitasema kweli daima, fitina kwangu mwiko.
(9) Nitakuwa mwanachama mwaminifu wa TANU na raia mwema wa Tanzania na Afrika.


Tuesday, July 5, 2011

SIKU YA JUMUIYA SAUT - Mtwara

Sehemu ya kwaya ikiongoza maandamano ili kuanza ibada. Naam waimbaji walipendeza hasa! 

SIKU YA JUMUIYA SAUT - Mtwara

Sehemu ya wanajumuiya wakifuatilia matukio ya siku yao kadri yalivyokuwa yakitokea

SIKU YA JUMUIYA SAUT - Mtwara

Jumuiya za watu duniani zinajenga utamaduni wa kukutana kwa malengo mbalimbali. Kuimarisha umoja wao, kujenga uzalendo kwa jumuiya na kadhalika. SAUT Mtwara ni jumuiya ya wasomi; watu wanaoandaliwa kuwa wajenzi wa dunia. Kwa kuwa jumuiya ya aina hiyo ina jukumu kubwa la kujielimisha zaidi ili kuondoa ujinga binafsi na kuisaidia jamii yake, basi inafaa mara mojamoja kupata nafasi ya kujipumzisha. Tarehe 4 Juni, 2011 ilikuwa ni siku ya jumuiya hiyo.

Kulikuwa na shughuli kadha wa kadha kuishi siku hiyo; ikiwa ni pamoja na hotuba anuwai za kitaaluma na maonyesho toka idara za hapo chuoni.

Sehemu ya wanajumuiya ya Saut wakianza sherehe za siku yao kwa maandamano.

Monday, June 27, 2011

UTANDAWAZI NA MALEZI

Na. Mdee Mwanahiza

Picha kwa hisani ya mtandao

Kamusi ya Kiswahili sanifu toleo la pili (2010) imeelezea maana ya utandawazi kua ni mfumo wa uhisiano wa kimataifa katika nyanja mbalimbali kama vile biashara, uchumi au siasa uliowezeshwa na maendeleo ya teknolojia ya habari yanayofanya mataifa kuwasiliana kiurahisi


Malezi ni njia ya ukuzaji wa mtoto kwa kutarajiwa kufuata tabia na mwenendo unaostahiki, makuzi na mafunzo.kwa watoto na vijana wanaokua katika jamii husika. Kwa ujumla utandawazi ni hali ya mabadiliko katika nyanja mbalimbali za kimaisha ya mwanadamu kama vile Uchumi, Siasa Jamii na Utamaduni na kuwa katika hali ya mfanano mmoja duniani kote. Mabadiliko haya yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na kukua na kuenea kwa sayansi na teknolojia ambayo imesambaa kwa kiasi kikubwa sana na kugusa karibu kila sekta ya maisha ya mwanadamu.

1:1 CHANGAMOTO KATIKA MALEZI

Kutokana na kukua na kuenea kwa utandawazi kumeathiri suala zima la malezi na kupelekea watu hasa watoto na vijana kukosa mwelekeo bora wa kimaisha kutokana na kulega kwa wakala wa malezi.

1:2 WAKALA WA MALEZI

Wakala wa malezi ni vyombo vinavyofanya kazi kwa niaba ya jamii husika katika kuhakikisha kwamba watoto na vijana wanapata malezi na mafunzo mema yanayoendana na jamii hiyo kama vile heshima, nidhamu, staidi mbalimbali za kimaisha ili waweze kujiandaa na maisha yao ya baadae na kuweza kushiriki katika shughuli mbalimbali za uzalishaji bila kupotoka na mambo mabaya yasiyostahiki katika jamii.

Hapo awali wakala wa malezi walikua ni familia, shule na dini pamoja na jamii yote kwa ujumla. Lakini kutokana na jamii kuzidi kukua na kuongezeka katika masuala ya uzalishaji, biashara na kupelekea kukua kwa miji kumesababisha kuongezeka kwa wakala wengine wa malezi kama vile vyombo vya habari hasa runinga, tovuti na simu za mkononi, magazeti na majarida mbalimbali. Makundi rika ambayo yanatokana na kukua na kuenea kwa sayansi na teknologia nayo yamekua ni miongoni mwa wakala wa malezi.. Hivyo kwa pamoja tunaweza kusema kisosholojia kwamba kuna wakala watano wa malezi ambao ni Familia,Dini ,Shule, Vyombo vya habari pamoja na makundi rika.

Wakala hawa wa malezi kila mmoja ana nafasi yake katika suala zima la kutoa malezi kwa vijana na watoto wa jamii husika. Kutokana na kipaumbele cha jamii hiyo kwa vijana na watoto.

1:3 FAMILIA

Kisosholojia familia ni muunganiko wa Baba, Mama na Watoto pamoja na ndugu wengine wa karibu. Kimsingi familia ndiyo muhimili mkubwa katika jamii yoyote ile. Mtoto anapozaliwa huanza kupata malezi kutoka kwa Baba na Mama yake pamoja na ndugu wengine wanaoizunguka jamii hiyo ili aweze kukua kwa kufuata mila na desturi za kimaisha katika jamii yake. Mtoto hufunzwa mambo muhimu kama vile heshima,Utii, adabu na nidhamu mbele ya wazazi wake na watu wengine nje ya familia yake pia hufundishwa stadi mbalimbali za Kimaisha na kujiingiza katika shughuli mbalimbali za uzalishaji mali ndani na nje ya familia.

Takribani miongo mitatu imepita tangu tulipopata mafanikio ya sayansi na teknologia ambayo yamekua ni chachu ya mageuzi katika familia zetu na maisha ya jamii nzima kwa ujumla. Mageuzi haya yameziathiri sana familia zetu katika suala zima la malezi, hi imesababisha baba na mama kuwaacha watoto wao wadogo na kwenda kufanya kazi za Ofisini mbali na nyumbani kwa siku nzima na kuwaacha watoto na walezi wengine..Hapo awali mwanamke ndiye aliyekua mlezi mkubwa wa familia wakati baba alikua anatoka nyumbani na kumuacha mama na kwenda kutafuta riziki kwa ajili ya familia yote. Mabadiliko haya ya baba na mama wote kwenda kutafuta riziki mbali na familia yao yameleta mmomonyoko wa maadili kwa watoto kwa kiasi kikubwa na kupelekea familia nyingi kusambaratika. wazazi wenyewe kwa wenyewe kulaumiana mwishowe tunaona wazazi wanaanza kupeana talaka.

Wazazi kuachana imekua ni jambo la kawaida katika karne hii ya utandawazi ambako kumepelekea athari mbalimbali katika familia kama vile.

i) Watoto kukosa malezi ya wazazi sahihi

ii) Ongezeko la familia za mzazi mmoja

iii) Ndoa za mikataba

iv) Kuongezeka kwa Umasikini katika ngazi ya kaya na Taifa kwa ujumla.

Kutokana na huu utandawazi tumeona wazazi hawawanyonyeshi watoto wao kwa wakati muafaka unaoshauriwa na wataalamu wa afya ili aweze kuendelea na majukumu yake ya kazini alipoajiriwa au kujiajiri. Hii inapelekea watoto na vijana kupoteza uwezo wao wa kufikiri na kushuka kwa kinga na hivyo kupelekea kupatwa na maradhi ya mara kwa mara na kushindwa kuwa wabunifu wanapokua wakubwa.

Na pia kutokana na huu utandawazi wazazi wanaona kua suala la kulea ni sawa na kupoteza muda wao kwani wana majukumu bora na mazuri kwao wao wenyewe na wala sio kwa watoto wao na kuona kwamba kulea ni kupoteza. bora wawe bize makazini. Hii .inachangia watoto kukosa mwongozo wa maisha yao na kushindwa kutatua matatizo yanayowakabili mbele yao na kushindwa kuendeleza vipaji vyao vya asili kwa ajili ya ;.

i) Kutokujua lugha zao za asili

ii) Kushindwa kumiliki miili yao

iii) Kutokufahamu taratibu na sheria za kijamii

iv) Kutojua mila na tamaduni zao

v) Kutokua na huruma kwa ndugu zao

vi) Uvunjifu wa maadili na kupoteza kabisa malengo ya kimaisha.

Utandawazi huu umeweza kusambaratisha familia zetu moja kwa moja ambapo hapo awali mtoto alikua ni mali ya jamiinzima, anaongozwa na kujirekebisha. Huu utandawazi umesababisha watoto kujitegemea na kujilea wenyewe pasipo kujua mwenendo mzima wa maadili ya jamii zao na matokeo yake ni kama vile.

i) Vijana kutosaidiana na kuthaminiana wao wenyewe.

ii) Kukosa umoja na mshikamano kama ndugu wa moja.

iii) Vita vya wenyewe kwa wenyewe ndani ya jamii moja.

vi) Umimi, Udini, Ukabila na Ukanda vimeyatawala maisha yetu

1:4 MAKUNDI RIKA

Rika ni watu ambao wana umri unaokaribiana na kulingana. Kundi rika anaweza kuwa rafiki ,yako jirani yako au hata mwanafunzi mwenzako. Watu wa kundirika wana uwanda mpana wa mazungumzo tofauti na mazungumzo katika familia au jamii kwa ujumla. Makundi rika ya zamani yaliongozwa na mafunzo ya jamii ya jando na unyago. Walifundishwa namna ya kuishi katika hali ya usawa, upendo, uvumilivu na maarifa mbalimbali ili waweze kukabiliana na changamoto za kimaisha pindi watakapokua na familia zao wenyewe ili nao waweze kuwalea watoto wao katika misingi hiyo hiyo yenye tija kubwa katika maisha yao. Kulingana na mabadiliko ya kimaisha yaliyoletwa na utandawazi yameharibu maana halisi ya mafunzo ya jando na unyago kwa vijana katika jamii nyingi za kiafrika ikiwemo Tanzania.

Makundi rika ya sasa hayana mafunzo yoyote ya kimaadili kwa wakubwa na wadogo zao, yametawaliwa na jaziba, hasira, chuki majivuno na dharau kutunushiana misuli mizozo isiyokua na tija kwao, fujo subira imepotea kabisa. Umaarufu ndio ngao ya maisha yao, kudai haki bila kufanya kazi, hawajui wajibu wao sio kwa wao wenyewe kwa familia zao wala kwa jamii zao. Mwelekeo potevu kwa makundi rika haya ni kutokana na utandawazi ambao umepelekea kulega na kupotea kwa mafunzo yetu ya asili ya jando na unyago na kutekwa kwa kiasi kikubwa na tamaduni za kimagharibi hivyo kujishughulisha zaidi na mambo ya kuiga na kushindwa kufanya mambo yao ya ubunifu na kusahau kabisa tamaduni zao katika suala zima la malezi na kujishughulisha na mambo ambayo hayana tija katika maisha yao.

1:5 TAASISI ZA ELIMU

Taasisi za elimu zinajishughulisha na malezi na mafunzo kwa niaba ya jamii husika. Husaidia vijana na watoto kupata mafunzo na stadi mbalimbali za maisha, taaluma na ujuzi ili waweze kukabiliana na changamoto mbalimbali za kimaisha pindi wanapohitimu mafunzo yao.

Taasisi hizi huongozwa na sera na mafunzo mbalimbali ambapo wakati mwingine hubadilika kutokana na huu utandawazi tulionao hivi sasa. Utandawazi huu kwa kiasi kikubwa umechangia kuwa na mabadiliko katika sekta ya elimu kama vile mabadiliko ya mara kwa mara katika mitaala yetu ya masomo na kusababisha kubadilika kwa mwenendo mzima wa utoaji elimu katika jamii husika. Kwa mfano hapa kwetu Tanzania kuongezeka kwa mtaala na teknolojia ya habari na mawasiliano (Teknohama) ambapo imepelekea watoto na vijana kuweza kutumia tovuti mbalimbali ambapo zingine hazina maadili kwa umri wao na hivyo kuwapelekea kuiga na kufanya vitendo ambavyo havina maadili katika jamii yetu.

Kwa upande mwingine vijana hawa ndiyo wanakua waalimu wa shule hapo baadae ambapo inapeleka ukosefu wa maadili shuleni kwani tayari wameshajifunza mambo tofauti ambayo yameathiri saikolojia zao na hivyo kuwafanya wanafunzi ambao ni watoto kuiga mienendo mibaya ya walimu wao na kupelekea utovu wa nidhamu kwa wanafunzi dhidi ya waalimu wao na kusababisha wanafunzi kutowasikiliza waalimu wao na hivyo kupelekea kuwa na matokeo mabaya katika masomo yao, kupata mimba wakiwa bado shuleni, matumizi ya simu darasani huku mwalimu akiwa anafundisha na kufuta ile dhana ya hapo awali kwamba mwanafunzi ni sawa na mtoto wa mwalimu lakini kutokana na utandawazi mwanafunzi anamwona mwalimu kama rafiki yake wa mtaani tu.

1:6 DINI

Dini ni mojawapo ya wakala wa malezi katika jamii toka jadi mpaka sasa. Dini zinatoa mafundisho mbalimbali ya kimwili na kiroho kwa watu wote hasa hasa watoto na vijana ili waweze kuwa na tabia na mienendo mema katika jamii kama vile namna kuabudu, kuheshimu wakubwa, nidhamu katika kazi na huduma nyingine za kimalezi katika jamii.

Utandawazi umeibua taasisi mbalimbali za kidini ambazo zimekua na mitazamo tofauti tofauti kuhusiana na suala zima la Kimungu na kimalezi katika jamii kama vile kuamini kuwa maombi yanaweza kumsaidia mtu awe na hali nzuri na ustawi wa kijamii katika maisha yake bila kufanya kazi. Hali hii imewafanya watu wengi kuacha kufanyakazi za kijamaa za uzalishajimali na malezi kwenye familia zao na kwenda kwenye vituo mbalimbali vya mahubiri na kukaa huko kwa muda mrefu huku wakiwa na imani kwamba watafanikiwa kimaisha kwa njia ya mahubiri na kumkemea shetani kama ndiye adui mkubwa wa hali ngumu ya maisha yao. Viongozi wa madhebu haya wameshindwa kuwafunza watu mbinu mbalimbali za kupambana na hali ngumu ya maisha kama vile kujituma bila kukata tama na kua waadilifu na waaminifu katikakazi mbalimbali za maendeleo katika jamii zao. Kwa mfano kwa sasa kuna vipindi vingi sana vya maombi na mahubiri kwa njia ya runinga kama vile Saa ya Maajabu.Tutashinda, Joshua Tv, Emanuel Tv ,ukiangalia vile vipindi kuna watu wengi wamehudhuria na sisi wengine huku nje tumekuwa watazamaji hivyo wote kwa pamoja tunaibiwa muda wetu badala ya kwenda kujishughulisha na shughuli zingine za uzalishajimali. Pia kuna baadhi makanisa yanaidhinisha kufunga ndoa za jinsia moja. Huu ni upotoshaji wa maadili kwa viongozi wa dini dhidi ya wafuasi wao wanaowaamini kama sehemu ya malezi kwao na jamii kwa ujumla.

1:7 VYOMBO VYA HABARI

Vyombo vya habari ni pamoja na runinga, tovuti ,magazeti , simu za mkononi na majarida mbalimbali. Vyombo hivyo ni sehemu mojawapo ya malezi na mafundisho kwa watu wa jamii mbalimbali, huelimisha, huburudisha na vilevile huonya kwa kupitia vipindi mbalimbali vinavyooneshwa kwenye runinga kama vile taarifa za habari vipindi vya uzalishaji mali, miradi mbalimbali vipindi vizuri vya watoto na elimu,.kwenye magazeti huandikwa habari na makala mbalimbali. Husaidia kuibua matatizo mbalimbali yanayoikabili jamii yetu kuonya na kukosoa viongozi wetu kuanzia ngazi ya kaya. hadi Taifa kwa ujumla.

Kwa upande mwingine vyombo hivi vimeweza kupotosha watoto na vijana ambao hawana muongozo mzuri katika matumizi ya vyombo hivi. Kuna mambo mengine yanaoneshwa na kuandikwa katika vyombo vya habari ambavyo havina maadili mazuri katika jamii yetu. Watoto na vijana wasiokua na muongozo ndio waathirika wakubwa kwani hutumia muda wao mwingi kuangalia na kusoma mambo haya kama vile picha za ngono kwenye filamu na tovuti, kusoma majarida ya udaku na kimapenzi, kuangalia tamthilia na vichekesho mbalimbali kama vile Vichekesho vya Hinye Gwedegwede ambvyao kwa sasa imepigwa marufuku. Hali hii imechangia uvunjifu wa maadili kwa kiasi kikubwa sana kwa watoto na vijana wa Taifa letu.

Utandawazi umepelekea vijana kuiga tabia na mienendo mibaya kama vile hisia za kimapenzi na utumiaji wa madawa ya kulevya na kujiingiza katika vitendo vya uhalifu. Hii ni kutokana na kuoneshwa kwa filamu za kiuhalifu na ngumi katika runinga zetu ambayo inapunguza ubunifu na kuendeleza vitendo vya uigaji na vijana kushindwa kujiingiza kwenye shughuli za uzalishaji mali na hatimaye kuwa wahalifu na kushindwa kufanya mambo yenye manufaa katika jamii.

NINI KIFANYIKE ILI KUKABILIANA NA CHANGAMOTO HIZI

• Wazazi watambue umuhimu na wajibu wao katika suala zima la malezi kwa watoto wao kwani wao ndio walezi wa kwanza katika jamii yoyote ile.Kwani wazazi ndio muhimili mkuu katika familia na taifa kwa ujumla,hivyo waoombwa wayajue na kuyatafakari upya majukumu yao kama wazazi ili waende sambamba na mabadiliko ya kisayansi na kiteknolojia pamoja na changamoto zake katika malezi ya familia na taifa kwa ujumla.

• Walimu inawapasa kutambua kwamba wanafunzi wa sasa ni mayatima,wengine hulelewa na baba au mama tu pia wengine wanatoka katika familia zenye migogoro,hivo wanahitaji msaada wao si wa kielimu tu bali hata wa kimalezi ili nao waelewe misingi ya maisha ya jamii zao pindi wanapohitimu masomo yao.Nahii itawasaidi kupambana na hali mbaya za maisha yao ya huko majumbani mwao na kuweza kuishi kwa kufuata mila na tamaduni za jamii zao.

• Viongozi wa dini waache tabia ya kumkemea shetani kana kwamba yeye ndiye chanzo cha matatizo na migogoro katika jamii zetu bali watumie nafasi zao kuwakeme wale ambao ni wafuasi wao katika kuwafunza zaidi masuala yanayotukabili kwa sasa na mienendo mema katika jamii ili nao weweze kuwaunza wanaowategemea na kumuomba mungu awape wepesi katika katika shunguli zao za kila siku na si kumkemea tu shetani.

• Serikali itilie mkazo na isimamie uuzaji wa filamu za ngono na urushaji wa vipindi ambavyo haviendani na maadili ya jamii yetu.isiangalie tu maslahi na haki za watunzi wa tunzi wa mambo haya bali wapige vita mambo ambayo yanaipotosha jamii.Wazazi nao wawaongoze watoto wao katika vipindi vyenye manufaa kwao na kwa jamii kwa ujumla.

• Wazazi na walezi wanatakiwa kuwafahamu kwa undani marafiki wa watoto wao.,na pia wajue walipo watoto wao na wanafanya nini.vilevile watumie muda wao mwingi wa kukaa na watoto waokuliko kuwaacha watumie muda wao mwingi kucheza na marafiki.Hii itawaepushi watoto kujiingiza katika mienendo mibaya.

HITIMISHO

Wakala hawa wa malezi huweza kujenga na pia kubomoa misingi ya jamii.hivyo vinahitaji ushirikiano wangu na wako katika malezi ya jamii ili kuleta maendeleo ya familia zetu na taifa kwa ujumla.

ASANTENI KWA USIKIVU WENU

.

Tuesday, June 7, 2011

Tasnia Ya Muziki Mkombozi wa Vijana

    Tasnia ya Muziki
Mkombozi wa Vijana

Hiki ni kitabu ambacho kinatokana na utafiti uliofanywa kitaalam. Kitabu hiki kinaelezea tatizo la ajira nchini Tanzania. Ukosefu wa ajira ndo hasa tatizo linalowakabili vijana wa Tanzania.

Vijana wengi huko Tanzania wanajituma ili kuepukana na tatizo hili la ukosefu wa ajira. Vijana wa mijini huko Tanzania, wameingia katika tasnia ya Muziki, hususani katika muziki wa vijana al maarufu Bongo flava. Muziki huu unachukuliwa na vijana hao kama aina ya ajira na kwa hiyo basi ilitarajiwa kuwa kazi hii ingekuwa ni mkombozi kwao. Taarifa ambapo hazikuwa zimefanyiwa utafiti zilionyesha kuwa vijana hao hawakunufaika kama ambavyo ilifaa wanufaike. Hali hii kwa hakika ilionyesha ombwe la maelezo; ni kwa sababu ya kutaka kutoa maelezo ndo hasa utafiti ulifanyika ili kuelezea kilichojiri.

Katika ukurasa huu tutakuwa na mfululizo kukielezea kitabu ambazo kinatoa mchango wa namna ya kukabiliana na tatizo hili la ukosefu wa ajira kwa vijana wetu hapa Tanzania.

Sunday, April 24, 2011

Ufufuko

Ufufuko unamaanisha matumaini!

Kutokana na ufufuko kifo kilipoteza nguvu zake zote; hivyo basi kifo hakina tena nguvu mbele ya maisha!