Wednesday, May 30, 2012

BASATA YAWATAKA WASANII KUONGEZA THAMANI KATIKA KAZI ZAO



Na Mwandishi wa BASATA

Huku kukiwa na juhudi za kutambuliwa na kuthaminiwa kazi za wasanii ndani na nje ya nchi, Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewataka wasanii kuongeza thamani kwenye kazi zao ili kuzipa ubora zaidi.

Wito huo umetolewa mapema wiki hii na Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari wa BASATA Godfrey Lebejo wakati akihitimisha programu maalum iliyohusu Ubunifu, Utengenezaji na Uongezaji thamani katika Kazi za Sanaa kupitia Jukwaa la Sanaa.

Alisema kuwa, ubora katika Sanaa unapatikana pia kwa Wasanii kuangalia wenzao wanafanya nini na wao kupata ubunifu mpya kwa kuongeza vionjo, uthamani na ubunifu binafsi katika kuifanya kazi ya Sanaa kwanza kupendwa na baadaye kupewa thamani kubwa sokoni.

“Ni wazi Wasanii wetu wanapaswa kuzingatia uongezaji uthamani kwenye kazi wanazozifanya. Kubuni kazi ni suala moja lakini kuongeza uthamani katika kazi yako ili ivutie wengi na kuuzika kwa thamani kubwa ni suala lingine la kuzingatia” alisistiza Lebejo.

Aliongeza kuwa, kwa sasa kuna taarifa za Wakenya kununua kazi za Wasanii wetu kwa bei ya chini na baadaye kuziongezea ubunifu, thamani na kuziuza nje kwa bei kubwa. Katika hili anasema, inatokana na wasanii wetu kutokuzingatia falsafa hiyo ya ubunifu na uongezaji thamani wa kazi zao.

“Tuna bahati ya kuwa na malighafi nyingi sana, baadhi zimeoneshwa hapa lakini suala hapa ni sisi kutumia ipasavyo malighafi hizo katika kubuni kazi zenye ubora na kuhakikisha tunazipa thamani stahiki tunapozisafirisha nje” alizidi kusisitiza.

Awali akiendesha darasa hilo maalum ambalo wiki hii lilikuwa mahsusi kwa ajili ya wasanii na wajasiriamali wa Sanaa za mikono (Handcrafts), Haroun Sabili kutoka asasi ya Musoma Handcraft alisema kuwa, Sanaa hizo zinahitaji ubunifu na umakini mkubwa kwani kinyume chake ni kutokuvutia na kupoteza uthamani.

Alitoa wito kwa Wasanii kujiunga katika vikundi na kuwa rasmi ili kuhakikisha kwanza,wanajenga mazingira ya kuwezeshwa lakini pia kupata mafunzo mbalimbali ambayo yatawafanya wazalishe kazi za Sanaa zenye ubora na thamani kubwa.

“Ni ngumu sana kuhudumia msanii mmoja-mmoja lakini mkiwa kwenye umoja ni rahisi sana kupata fursa za uwezeshaji hususan mafunzo katika kuongeza ubunifu na uthamani wa kazi zenu” alishauri Haroun.

Katika programu hiyo iliyohudhuriwa na wadau 72, elimu kuhusu ubunifu na uongezaji thamani kwenye kazi za Sanaa ilitolewa sambamba na malighafi mbalimbali na jinsi zinavyoweza kutumika kuzalisha kazi za mikono kuoneshwa.

Tuesday, May 22, 2012

NAFASI ZA MASOMO ZAIDI (UZAMILI)

Nchini Tanzania, idadi ya vyuo vikuu imeogezeka kutoka chuo kikuu kimoja tu cha umma mwaka 1961 hadi kufikia zaidi ya vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki 60 mwaka 2012. Takwimu hizi ni kulingana na kitabu cha mwongozo wa kuomba nafasi za masomo vyuo vikuu toka mamlaka ya kudhibiti vyuo vikuu nchini TCU.

Kuongezeka huko kwa vyuo vikuu nchini pamoja na kuja kutokana na sheria ya kuruhusu vyuo hivyo, imekuja hasa baada ya kuonekana mahitaji dhahiri nchini. Idadi ya watu, hususani wanafunzi imeongezeka kwa kiasi kikubwa. Makadirio yanaonyesha kuwa kuna zaidi ya wananchi milioni arobaini hapa Tanzania, na wengi kati ya watanzania hao ni vijana. Na zaidi, kuanzishwa kwa shule nyingi za kata, japo nyingi zingali duni kiubora, kumeongeza idadi ya vijana wenye uhitaji wa elimu ya chuo kikuu. Na ukweli huo unapatikana kwa uwazi zaidi katika malengo ya kimaendeleo ya Tanzania 2025; kwamba kufikia wakati huo watanzania wengi wawe wamefikia daraja la kati.

Elimu ni njia ya uhakika ya kumuweka mtanzania wa kawaida kwenye daraja la kati kuliko njia nyingine nyingi zinazofahamika. Kwa mantiki hiyo inafaa zaidi watanzania wengi wapate elimu yenye lengo la kuwakomboa, kifikra na kiujuzi na hatimaye waelimike kwa lengo la kuwasaidia kwa maana ya kuwatumikia wananchi wenzao wengi.

Kwa mantiki hiyo vijana ama wanafunzi wengi wanahitajika kujikita vyema katika masomo wanayoyafanya, wabobee kwa uhakika hasa. Wanaokwenda kazi wakafanye kazi kwa bidii na ujuzi zaidi wanaotaka kuendelea na masomo zaidi wafanye vivyo hivyo kwa bidii bobevu. Hapa ni nafasi moja kwa wanaopenda kuendelea na masomo zaidi. Wasome hapa kuna nafasi za kutoa udhamini kwenye masomo ya juu zaidi. Udhamini wa masomo - Sholarship hapa...

Thursday, April 26, 2012

MASHINDANO YA SU-SAUT KATIKA PICHA

Kikundi cha uhamasishaji STEMMUCO
Mashabiki katika mduara wa sherehe
Mchezo baina ya STEMMUCO NA JUCO UKIENDELEA
Mashabiki wa STEMMUCO wakishangilia ushindi wa timu yao


                                                                                                                                  
   
                                                        

                          

Wednesday, April 25, 2012

Siku ya Malaria Duniani

Ugonjwa wa malaria ambao ni wakitropiki, unaendelea kuuwa watu wengi duniani na hasa barani Afrika hususani kusini mwa jangwa la Sahara. Ungonjwa huu ambao inasemekana umekuwa ukimsumbua binadamu kwa zaidi ya miaka 50'000 ni tishio kwa afya za Waafrika wengi.

Malaria huuwa zaidi kina mama na watoto
picha hii kwa hisani ya blogu hili
Asilimia 90% ya vifo vyote vya malaria hutokea barani mwetu, ambapo asilimia sitini ya vifo vyote huwa ni watoto wadogo chini ya miaka mitano. Mara nyingi malaria huambatanishwa na umasikini, na huenda ukawa moja ya vyanzo vya umasikini barani. Kuhusiswa huko na umasikini ni kutokana familia nyingi barani kushindwa kumudu manunuzi ya dawa za kuzuia maambukizi lakini pia mara nyingine kukosa uelewa wa namna ya kujikinga hususani vijijini na mijini kwenye familia zenye elimu na kipato cha kadri ama chini .
Chandarua chaweza kuzuia maambukizi
Ugonjwa huu unaweza kuzuiwa kwa kutumia chandarua kilichotiwa dawa ya kuua mbu na wadudu wengine, kusafisha vyema mazingira ya maeneo tunayoishi ili kuharibu mazalia ya mbu, kukausha na kuondoa maji yote yaliyotuama. na kadhalika.

Ugonjwa wa malaria unazuilika na inawezekana kufanya hivyo kama usemavyo ujumbe wa kataa Malaria. Na ukweli huu umedhihirika huko Zanzibar na Zambia ambapo katika ripoti za hivi karibuni, ugonjwa huo umedhibitiwa kwa asilimia zaidi ya hamsini.

Kwa kumbukumbu ya siku hii tujihadhari zaidi na kuhadharisha wenzetu wawe makini na ugonjwa huu unaoendelea kuuwa binadamu wengi zaidi mithiri ya vita.  

Taarifa za Malaria zaidi zinaweza kupatikana katika blogu hii pia. na katika blogu la unicef, who nk




Sunday, April 22, 2012

JE UMEANDIKA NINI?

Kipanya kikitoa huduma ya usafiri kwa umma. Picha toka blogu

















Hivi karibuni nilikuwa kwenye basi dogo la usafiri wa umma daladala; toka Mtwara kwenda Mikindani. Usafiri maarufu kwa daladala za Mtwara ni vipanya; vibasi vidogo vidogo ambavyo nadhani vingi ni mitumba toka Dar es Salaam. Vipanya vingi mjini hapa vimechoka na vinakwenda kwa mwendo wa kusuasua vinapokuwa barabarani. Hakuna mabasi makubwa mithili ya yale ya Mwenge Posta kwa Dar es Salaam, pamoja na hayo ule udaladala upo pale pale. Daladala ama vipanya hivi vinajaza kama ilivyo ada ya daladala sehemu nyingi Tanzania. Hapo juu nimegusia Mikindani; huu ni mji mkongwe, mji wa zamani ambao kwa bahati mbaya umesahaulika, hauendelezwi tena. Pengine kwa kuwa neema ya gesi mjini hapa imefunguliwa basi mambo huenda yakawa sawia  kwa mji huu wa kihistoria.Sasa nirejee kwenye mada ya makala hii.

Mikindani chakavu, picha na blobu ya wadau wa safari


















Katika kipanya nilichokuwa abiria, utakumbuka kuwa kwenye daladala huwa kuna mada nyingi, kondakta wetu alikuwa muongeaji kupindukia. Kodakta, konda ndivyo wanavyofahamika zaidi, huyu hatofautiani na wengi walio mikoa mingine; ni kijana aliyevalia sare chakavu ya kazi na ambapo kama walivyo wengi wao suruali yake ilikuwa ikining'inia zaiki kuliko kuvaliwa, namna hiyo ya kuvalia huitwa na vijana wa leo "kata k". Koda yule katika utani na abiria mmoja ndani ya daladala letu, ambaye nadhani ni shwahiba wake kwa jinsi walivyokuwa wameshibana kwa simulizi za kutosha bila shaka kwa lengo la kufupisha safari. Basi yule konda alimtupia rafiki yake swali ambalo hasa nd'o linabeba kichwa habari cha mada hii, hivi wewe toka umalize shule ya msingi umeandika chochote kweli?
Hivi wewe umeandika chochote kweli? Kwa hakika hili ni swali dogo sana na lategemea uzito ambao mtu ataamua kulitilia mkazo. Lakini ni jambo kubwa na muhimu sana pia. Mtu anayeandika kwa kawaida ni mtu anayesoma pia. Kwa hivi swali la konda lauliza pia, je, umesoma nini hivi karibuni? Sina hakika kama yeye mwenyewe ameandika ama amesoma chochote hivi karibuni. Tafiti na ripoti mbalimbali zinaonyesha kuwa moyo na tabia ya kujisomea kwa watu wengi imepotea ama inapotea kwa kasi kubwa . Hapo zamani ilikuwa ni lazima kuandika barua ili kujua nini kinaendelea nyumbani kwa wazazi wako walio mbali nawe, siku hizi inatosha kuweka salio katika simu ya mkoni, simu hizo karibu kila mmoja anayo yake; hii ni moja ya sekta ambazo Tanzania imepiga hatua kubwa sana, na kuanza kuongea. Anayejua kuandika ataongea kama asiyejua kuandika halikadhalika. Kukua kwa tekinolojia ya habari nako kwa kiasi kikubwa kinachangia kushuka kwa moyo wa kuandika na kusoma kama hapo awali. Hivi leo hata zile huduma za kibenki ambazo humlazimu mtumiaji kuandika japo sentensi mbili tatu zinafanywa kwa wepesi na urahisi kabisa kupitia simu ya mkononi hata na mtu asiyejua kusoma na kuandika ila tu masuala ya lazima hususani yahusuyo pesa. Maendeleo ya tekinolojia ya habari ni muhimu lakini tuendelee kujifunza kusoma na kuandika.

Hivi wewe umeandika chochote toka uhitimu elimu ya msingi, sekondari, chuo kikuu, toka upate udaktari wa falsafa?Swali hili la konda mhitimu wa darasa la saba lamgusa kila mmoja wetu toka wale wa shule ya msingi hadi madaktari wasiotimu watu ila falsafa. Nchini Tanzania pamoja na juhudi nyingi za wasomi wetu mahitaji ya vitabu vya mafunzo mbalimbali bado ni vichache; tunaendelea kutumia vitabu toka ng'ambo. Hili si jambo jema hata chembe.

Wito kwa kila mmoja wetu tuongeze muda wa kusoma vitabu zaidi na kufanya hivyo tutapata hamu na ujumbe wa kuandika chochote kitu kwa lengo la kuielimisha jamii, ambalo ni jukumu la kila mmoja wetu.

Monday, April 16, 2012

MANENO MAKALI HAYAVUNJI MFUPA

The image by the courtesy of Google
                                   
"The smallest deed is better than the greatest intention." John Burrough.
Maneno Makali hayavunji mfupa!

Wazo hili nimelipata katika mtandao wa advance Africa. Mtandao ambao siku zote hutoa kwa wahitaji fursa za masomo na kazi zaidi . Mtandao huu ni nyenzo nzuri wa vijana walio masomoni na wanaotarajia kumaliza masomo yao na kujiunga na ulimwengu wa kazi.

Mtandao huu huonyesha fursa za kazi kwenye nchi mabalimbali ikiwa ni pamoja na ughaibuni. Kwanza nieleweke vyema kuwa jambo muhimu kwa mwenye kuweza kulifanyia kazi, ni mtu binafsi kujiajiri ni vyema akafanya hivyo japokuwa si vibaya kama atafanya kazi sehemu nyingine kwanza ili apate mtaji wa kuanzisha shughuli zake binafsi. Kwa wale wanaopenda kufanya kazi za kuajiriwa, wanaweza pia kufikiria kazi za hapa nchini na pia zile za kimataifa. Vijana wetu wafahamu kuwa kazi hizo zipo pia kwaajili yao si tu kwa watu wa mataifa mengine. Hata hivyo ili kuweza kupata fursa hizo ni vyema kuzingatia masuala kadhaa yenye umuhimu usio kifani. Weledi, uaminifu, kujiamini na kujituma, ujuzi wa lugha za kigeni, utayari kuishi katika tamaduni mchanganyiko na kadhalika.

Weledi ni kigezo cha uhakika kwa mtu kufanya kazi popote apendapo. Weledi ni msamiati ulioibuka hivi karibuni ukimaanisha ujuzi na uwezo wa kufanya kazi. Wanachuo ama mtu yeyote anayetaka kufanya kazi ni vyema awe na ujuzi wa kile anachotaka kufanya hii ni muhimu hasa. Hapa linaibuka swali la mtu anapata vipi uwezo na ujuzi wa kazi ili hali ndo kwanza anatoka masoni? Swali hili lafaa kujibiwa na fursa za kujitolea; vijana wanafunzi, wanavyuo tujenge utamaduni wa kujitolea kufanya kazi katika makampuni, mashirika na hata kati taasisi za kidini ili mradi kuwe na fursa ya kujijenga katika utendaji kazi na hapo hakutakuwa na ukosefu wa ujuzi.

Uaminifu; ni moja ya mahitaji muhimu katika ulimwengu wa kazi na ujasiriamali. Katika ulimwengu wa mtaji jamii "social capital" uaminifu ni suala la lazima katika mafanikio, ili ufanikiwe ni lazima uwe na mtandao mkubwa na mpana, huwezi kupata mtandao mkubwa vile kama wewe si mwaminifu. Kwa hivi basi ni lazima kujifunza kuwa mwaminifu. Tunu ya uaminifu ni moja kati ya zawadi amabazo watu wengi hujifunza toka katika familia zetu; huwatazama wazazi wetu jinsi wanavyoishi na hii hurithi toka kwao. Hata hivyo kulingana na uwezo mkubwa wa ubongo wa binadamu; unaweza kujifunza kila kitu mradi tu upatiwe mazingira na kuwe na nia na ulazima wa kufanya hivyo.

Kujiamini na kujituma; hivi ni vigezo muhimu katika mafanikio. Ili uweze kufanya jambo fulani ni lazima kwanza wewe mwenyewe ujiamini kuwa unaweza kulifanya, lakini kujiamini peke yake haitoshi ni lazima kujituma katika kile unachonuia kukifanya. Tunu hivi mbili ukiziweka pamoja basi una uhakika wa kufanikiwa. Msemo wa Kiswahili Penye nia pana njia unafaa uwe kielelezo na mwongozo katika malengo yako maishani.

Ujuzi wa lugha za kigeni; hiki ni kitendea kazi muhimu hasa hususani katika zama zetu za utandawazi. Katika nyakati hizi watu wengi zaidi husafiri, kufanya hivyo kuna walazimu kujifunza lugha kadhaa. Wewe huna sababu ya kutojifunza lugha muhimu za maitaifa mengine hasa zile zenye ushawishi kwa mataifa mengi. Unaweza kujifunza na kutawala vyema zaidi Kiingereza, Kifaransa, Kispanyola, na sasa kwa sababu za kiuchumi, watu wanajifunza kichina. Ujuzi wa lugha nyingi utakufanya uwe mshindani mkubwa na kujitofautisha na hata wale waliofanya kazi siku nyingi.

Utayari kuishi katika tamaduni mchanganyiko; binadamu sisi ni wamoja kwa namna zote muhimu. Binadamu ana undwa kwa chembe hai ndogo ndogo ambazo ni sawa kwa kila binadamu, ana mifumo kadhaa ambayo hufanya kazi sawa sawa na kadhalika. Hata hivyo tamaduni, mazingira, makuzi n.k huleta tofauti tulizonazo katika jamii za binadamu zilizosambaa katika uso wa sayari ya dunia. Tofauti hizi muhimu ndo hutufanya tufanikiwe kwani hutujengea ushindani mioyoni mwetu. Sasa kama unataka kufanikiwa ni lazima ujifunze kuishi na watu wa jamii zingine; kupitia wao utajifunza taaluma na tekinolojia za watu wengine. Ukipata fursa hiyo; itumie vyema kwani unaweza kuibadilisha dunia toka duniani kote!

Kwa wanaotafuta nafasi za kazi na masomo nje ya nchi tafuta kwa kubonyeza hapa


Saturday, March 31, 2012

KIFO: UKAMILIFU WA UBINADAMU

Sehemu ya umati uliofika kumuaga mwanachuo aliyeaga dunia
















Kama ilivyo kwa mawiyo na macheyo ya jua, ndivyo ilivyo kwa kuzaliwa na kifo. Msemo mmoja wa kiafrika wasema: "Kamwe ardhi haichoki kutupokea" ama kama inavyojidhihiri katika vitabu vitakatifu; kuna muda wa kila jambo: kupanda na kuvuna, kuzaliwa na kufa... ama tena binadamu u mavumbi na mavumbini utarudi. Na zaidi na pengine muhimu kupindukia; mbegu isipoanguka ardhini na kufa hubaki kama ilivyo, lakini ikianguka na kufa huzaa zaidi na zaidi kuliko ilivyokuwa hapo kabla. Mbegu ya mmea wowote inaweza kufananishwa na maisha ya binadamu.

Inafaa kukumbushana kuwa mara tu binadamu anapotungwa kwenye tumbo la mamaye, tayari anakuwa na sifa za kuaga dunia, kufa. Hii inadhihirisha kwa maisha ya vichanga ambavyo hata kabla ya kuzaliwa, hufariki dunia. Vijana wengi hudhani ya kuwa kifo ni kwaajili ya wazee; watu walioishi kwa miongo kadhaa hapa duniani. Ni vyema tuambiane kuwa hii si kweli, kila binadamu yupo tayari, ameiva, amepevuka kwaajili ya kifo. Kama isemwavyo hivi leo kila mtu ni marehemu mtarajiwa. Kwa mantiki hiyo basi hatuna haja ya kuogopa. Kinyume chake inafaa tujiandae kwa tukio hilo la uhakika kama ilivyo kwa kuchomoza jua bila juhudi zetu kila asubuhi, kwa uzoefu tu twafahamu kuwa jua litachomoza. Pamoja na kujua ukweli huo bado hatuzoei suala hili.


Jeneza likiwa ndani ya ndege tayari kwa safari

Kamwe hatuzoei kifo kwa sababu kila kinapotokea, kinatokea kwa mtu ambaye hajawahi kufa. Najua hili si jambo geni lakini huo ndo ukweli wenyewe, je ni kwanini? Jambo hili li hivyo? Bila shaka ni kwa sababu kila mtu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kiimani twaelewa kuwa binadamu ameumbwa na Mungu na kuwa binadamu nd'o kazi nzuri kuliko kazi nyingine zote za Mungu na ni kwa sababu hiyo kila anapofariki dunia mwenzetu basi sisi hupatwa na simanzi lisiloelezeka, hata wale wenye mioyo migumu huguswa pia na kifo cha mpendwa ama mwanadamu ambaye walimfahamu, kuishi naye na kadhalika. Kifo ni sehemu ya ukamilifu wa binadamu.

Katika vitabu vitakatifu twaambiwa ya kuwa Mwenyezi alitufahamu hata kabla ya kuiumba dunia hii, kama nilivyoeleza hapo awali, binadamu kwa hakika ni kazi bora kabisa ya Mwenyezi Mungu. Twajua pia kuwa binadamu huanza kibaiolojia pale yai la mwanamke linaporutubishwa na mbegu ya mwanamume: kuanzia hapo safari ya binadamu fulani kibaiolojia huanza, na maisha yake huanza hapa duniani kwa kuzaliwa. Binadamu anazaliwa anaishi na hatimaye lazima afariki dunia. Kupitia kifo mzunguko wa binadamu unakamilika. Hivyo tukichukulie kifo kama ukamilifu wa ubinadamu wetu. Hata hivyo jambo la msingi hapa ni je, maisha hayo tunayaishi vipi hapa duniani?

Hivi leo wengi tunadhani kazi yetu katika sayari hii ya dunia ni kukusanya na kujilimbikizia mali nyingi iwezekanavyo. Tunajisahau, ukweli na wito wa binadamu ni kutoa mchango wa kuiboresha zaidi dunia kwaajili ya utukufu wa Mungu kama asemavyo Inyasi wa Loyola (1491-1556) . Tunaweza kuiboresha dunia kila mmoja kwa nafasi yake; mwalimu afanye kzi yake ya ualimu vyema, mwanasiasa afanye kazi yake vizuri, mwandishi, mkulima, mwanasayansi, mwanafalsafa, mwanafunzi na kila mmoja wetu afanye vyema kabisa kazi yake. Kushidwa kufanya vyema ama kutimiza wajibu wetu ni sawa na kushindwa kuitikia wito wa maisha yetu na tukishindwa kufanya hivyo basi maisha yetu yanakosa maana!

Tafakari hii imenijia baada ya kuona nyuso nyingi za huzuni wakati wa kumsindikiza mwanachuo wa stemmuco hivi karibuni baada ya kukamilisha safari yake hapa duniani.

Saturday, March 17, 2012

Mkanganyiko wa Maisha: Misitu ama Maisha?


Baiskeli hii TZ MKAA ikiwa imeengesha bidhaa kusubiri wahitaji mjini Mtwara
Kuishi kwenye jumuiya ya wasomi ni faida kubwa. Msomi, kwa tafsiri yangu ni mtu yeyote mwenye elimu kuanzia darasa la saba, ama kwa upana zaidi anayejua kusoma na kuandika, lakini mwenye moyo wa utafiti, kujisomea na kuwashirikisha wengine taarifa ya anachosoma ama anachotafiti.

Mwanachuo wa Stella Maris Mtwara University College (STEMMUCO), ambao kwa maelezo yangu ni wasomi, wapo katika harakati za kuandika taarifa, ripoti ya tafiti walizofanya sehemu mbalimbali hapa nchini. Kuna mada nyingi karibu kadri ya idadi ya watafiti hao. Kuna ripoti juu ya hali ya uchumi nchini, hali ya hisabati shuleni, nafasi ya sayansi katika elimu ya tanzania, hali ya elimu nchini, ushiriki wa wasichana katika elimu, jando na maendeleo, kwa ufupi nyanja zote muhimu zimeguswa, kuanzia siasa, uchumi, sayansi, na jamii. Zaidi tasnifu hizo za wasomi zimeangazia makundi mbalimbali katika jamii; wazee, wanawake, walemavu, vijana na kadhalika.

kwa ufupi, makala hii inagusia mkanganyiko unaowakuba vijana wanaofikia kundi la kujitegemea maishani. Hili ni kundi muhimu mno; hii ndio nguvu kazi hitajika ya ujenzi wa taifa letu. Tafiti zinaonyesha kuwa kundi kubwa la vijana karibu ya vijana milioni mbili na laki tatu (2.3), takwimu rasmi za serikali ya Tanzania 2005, hawana ajira zinazoeleweka. Kumbuka hii ni idadi ya makadirio tu, kuna idadi kubwa sana ambayo mara nyingi haijumuishwi kwenye taarifa rasmi, kwa hivi basi, vijana wengi hawana kazi. na wanakumbana na mkanganyiko wa maisha.

Baadhi ya sera zinakataza ama zinapiga vita shughuli ambazo vijana huzitegemea kuendesha maisha yao. Bishara ya mkaa ni moja ya biashara zinazopigwa vita kwa vile watayarishaji mkaa wengi huvuna miti kwaajili ya kuni bila mpangilio maalumu. Ni kweli zao la mkaa linaharibu mazingira na kuhatarisha dhana ya maendeleo endelevu. Wakati zao hili linapigwa vita, mahitaji na matumizi yake ndo kwanza yanazidi kuongezeka kila uchao. Na hii ni dhahiri kuwa mkaa ni bidhaa ambayo itaendelea kutumika kwa miaka mingi ijayo; kama wasemavyo vijana wa Bongo Flava; mkaa bado tutakuwa nao kwa muda mrefu sana. kumbe tufanye nini sasa.

1. Mosi, maafisa misitu, ama wataalamu wa maliasili waweke utaratibu wa kupanda miti kuwe na maeneo maalumu ya kupanda miti na vijana wavuna miti kwaajili ya mkaa wapewe maeneo ya kupanda miti na kuitunza ili hali waonyeshwe eneo maalumu la kuvuna miti ya kazi yao hiyo.

2. Pili, mamlaka husika zenye kujihusisha na gesi ya kupikia majumbani waangalie uwezekano wa kupunguza kwa kiasi kikubwa kodi za chanzo hicho mahususi cha nishati hitajika ili wananchi wengi ikiwa ni pamoja na mashambani waweze kuitumia pia.

3. Tatu, tafiti zifanyike kuangalia upunguzaji wa bei ya umeme ili walio na fursa ya kutumia nishati toka shirika la taifa la umeme watumie pia kwa kupikia; kwa sasa bei yake ni kubwa mno kwa mwananchi mwenye kipato cha wastani kumudu gharama hizo.

Mpanda baiskeli akitafuta wahitaji wa biadhaa yake manispaa ya Mtwara-Mikindani
Nchini Tanzania hali halisi ndivyo ilivyo vijana wengi wamejiajiri kuuza mazao ya miti

Tukifanya haya kuna uwezekano wa kufikia ndoto tuliyonayo ya kuwa na Watanzania wa daraja la kati ifikapo 2025 kama inavyoelezwa kwenye mpango wa maendeleo wa taifa. Kinyume na hivyo vijana wetu wataendelea kuwa kwenye mkanganyiko mkubwa wa misitu ama maisha ya leo; je nikate miti ili nichome mkaa ama nisikate na kufa njaa? 

Wednesday, March 14, 2012

Siku ya Wanawake STEMMUCO - MTWARA


Sehemu ya wanawake wakifuatilia matukio

Wajumbe wakifuatialia mtiririko wa matukio
Akina mama wakifanya utambulisho siku ya kimataifa ya wanawake duniani



http://www.stemmuco.ac.tz/index.php

Sunday, March 11, 2012

Mashindano ya PRO-LIFE - MTWARA

Picha kwa hisani ya google
Mashindano ya Pro life, ambayo yanaanza kujenga mizizi mjini Mtwara, kwa mwaka huu 2012 yamefunguliwa rasmi hapo jana. Mashindano hayo yanajumuisha taasisi kadhaa za elimu mjini Mtwara.

Moja ya malengo la mashindano haya ni kujenga uhusiano baina ya wanavyuo katika manispaa ya mji huu wa kusini mashariki mwa Tanzania. Yanatumika pia kama sehemu ya matumizi sahihi ya nguvu za vijana; kundi la watu wenye nguvu kubwa za mwili. Mashindano ni sehemu ya mazoezi muhimu yanayohitajika kwaajili ya kujenga na kuulinda mwili.

 Pamoja na malengo mengine mahususi na mazuri mno yaliyotajwa; Jina la mashindano haya lengo lake hasa ni kutetea na kulinda uhai kama jinsi ilivyo kwa malengo halisi ya "Pro-life". Pro life ni vuguvugu lenye lengo mahususi la kutetea na  kulinda uhai wa binadamu. Binadamu huanzia kwenye muungano wa yai la mama na mbegu ya baba, na hapo safari ya mwanadamu mpya huanza. Kwa hiyo binadamu anaanzia tumboni mwa mama hata kabla ya kuzaliwa. Kutokana na maelezo hayo basi utaona kuwa Prolife hutetea uhai wa mtoto anayekuwa tumboni mwa mama na kwa hivi hupinga utoaji mimba kwa lengo la kutetea na kulinda uhai.

Kwa hiyo basi vijana wa kike na wa kiume wanaalikwa kuheshimu uhai wa mwanadamu kwa kujizuia kabisa kushiriki katika utoaji mimba. Kunaweza kuwa na sababu lukuki za kuhalalisha utoaji mimba lakini ukweli ni ule ule kwamba utoaji mimba ni uuaji ni uharibifu wa maisha. Vijana hivi leo wanashindwa kujizuia kushawishiwa kutoa mimba; njia rahisi ya kuepuka kujiingiza kwenye kosa hilo ni kuwa na mahusiano yenye heshima. Mvulana na msichana wawe marafiki ili kusaidiana kukua kikamilifu katika ubinadamu (mwanaume hujifunza toka kwa mwanamke na kinyume chake pia) mahusiano ya kimwili yasubiri vijana watakapofunga ndoa na kutambulika mbele ya jamii na mwenyezi kuwa wao ni bwana na bibi fulani. Kufanya hivyo kutasaidia kuondoa utoaji mimba-uuaji!

Katika tafsiri ya leo ya kutetea na kulinda uhai vijana tunaalikwa kuacha mambo yote ambayo yanapunguza maana ya maisha yetu. Vijana tupunguze ama kuacha kabisa unywaji wa pombe, tuache uvutaji wa sigara kwa kuwa hasara na matatizo yanayosababishwa na uvutaji ni makubwa kuliko furaha ya uvutaji. Kwa wale tunaotumia dawa za kulevya tuache na tuwashawishi rafiki zetu waache ushiriki na utumiaji wa vitu hivi vinavyopingana na maisha. Tukifanikiwa katika hayo amani, upendo na mafanikio vitatamalaki kote duniani, lakini vianzie kwa kila mmoja wetu.

Kwa hivi basi mashindano ya "STEMMUCO Pro-life 2012" yanalenga kutetea na kulinda uhai wa binadamu. Vijana wote walio mashindanoni wanapaswa kufahamu hilo na kwamba wao tayari wanakuwa ni mabalozi wa uhai-ni watetezi na walinzi wa uhai. Mashindano mema!!!

Thursday, March 8, 2012

Siku ya Wanawake duniani katika matukio Mtwara

Vazi rasmi siku hiyo ilikuwa kitenge - Naam kina mama wanapendeza
na kuongeza staha sana kwa mwanamke pale wanapovalia mavazi ya heshima




























Hii ni siku mahususi kwa wanawake duniani. Hutumika kuwakumbusha wanawake wenyewe, watunga sera, na jamii yote kwa ujumla juu ya haki na nafasi ya mwanamke katika nyanja zote za maisha.































Tafiti nyingi hapa Tanzania zinaonyesha kuwa mwanamke hususani yule wa kijijini anafanya kazi nyingi kuliko mwananchi mwingine yeyote. Pamoja na mchango huo mkubwa wa wanawake, mara nyingi juhudi zao hazitambuliki vya kutosha na wala hawathaminiwi na jamii kwa kiasi stahiki. Hivyo kwa siku ya leo ni fursa kuikumbusha jamii na wanawake wenyewe hasa wale wa mashambani. Ni dhahiri kuwa wanawake wengi vijijini wanafanya kazi nyingi kwa kuwa tamaduni nyingi, zenye mfumo dume, zinawalazimu kufanya hivyo.





























Tunawaomba na kuwapa changamoto wanawake wa mijini, kulihamasisha kundi hili lenye mchango mkubwa kwa uchumi wa nchi yetu. Mwaka huu, kwa kutambua nafasi ya elimu kuleta mabadiliko kwa jamii, wito umeelekezwa kwa ushiriki wa mtoto wa kike katika elimu kama kichocheo kikubwa kuleta maendeleo ya jamii.

Saturday, March 3, 2012

Duh angurumapo simba mcheza nani?


Hii toka kwa kaka michuzi
Hakuna ubishi kuwa watu wengi tunapenda mchezo wa soka hapa Tanzania.

kupitia huu upenzi wa mpira kwanini tusibuni njia ya kuhamasishana kwenye elimu kupita soka ili kiwango na ubora wa elimu yetu vikue pamoja na soka hasa la kina mama; soka la kina mama Tanzania ni bora zaidi kuliko la kina baba, kwa kigezo cha matokeo. Taifa Stars imewahi kuifunga timu nyingine mabao matano?


Hii ni keki tuliyokula siku ya ufunguzi wa Simba TV. Hata hivyo TV hiyo inayorusha vipindi vyake kupitia clouds tv inaishia tu mikocheni, haifiki walipo watazamaji wa mdenga, Mtwara, Lindi, Mazoo, Shytown, Ta etc fikisheni mapema basi! 

Harakati za Ubunifu wa vazi la Taifa?




Picha zote kwa hisani ya blogu la UDADISI

Thursday, March 1, 2012

Mtazamo Chanya Humjenga Binadamu!

Maneno haya ya kiingereza juu ya rais huyu wa Marekani ni fundisho la aina yake
tujifunze kupenda tunachofanya na tukifanye kwa moyo wote matokeo yake ni furaha na amani
Ujumbe huu nimeupata toka kwenye e-mail niliyotumiwa na Edward Ezekiel, kwa hakika ni ujumbe mzuri na wa maana mno.

Huu unawafaa vijana wote ambao ni wepesi wa kukatishwa tamaa na watu wengine. Kumbuka hakuna mtu mwenye mamlaka ya kukufanya ukose furaha, ili ukose furaha, ukasirike ama uwe kwenye aina yote ya hisia ni lazima wewe mwenyewe uamue; Lincoln ni mfano mzuri mno. Maneno ya watu wengine si yenye kutubomoa.

Fundisho la pili ni kufanya kazi zetu kwa uadilifu, ubunifu, umakini na zaidi ya yote upendo. Mambo hayo husaidia kuvumbua mbinu mpya za kurahisisha maisha na kuleta maendeleo kwa watu haraka. Ndugu huyu japo si Mwafrika na atukumbushe kutenda mema!

Je Afrika imejididimiza yenyewe?

Ndugu zangu salam,
Kigoda cha Taaluma cha Mwalimu Nyerere kinawakaribisha wote kwenye , Malumbano ya Hoja baina ya Wanafunzi wa Sekondari na Chuo Kikuu, mada ni " Handira hii inaamini kwamba Afrika imejididimiza yenyewe" ikifuatiwa na filamu ya "The Last Days of Walter Rodney" hapa UDSM-katika ukumbi wa Nkrumah, tarehe 03.03.2012 siku ya Jumamosi kuanzia saa 4:00 asubuhi mpaka 8:15 mchana. Malumbano haya ya hoja yatakuwa katika lugha ya Kiswahili. Nawaombeni tusambaze tangazo hili kwenye mitandao yetu ya jamii. Karibuni sana.
Nimeambatanisha ratiba na bango bonyeza hapa.

Walter Rodney Luanda
Mwalimu Nyerere Chair-Senior Administrative Officer

Tuesday, February 28, 2012

Kumbe wabunge wetu ni maskini vile !

Jengo la kisasa la Bunge la Tanzania huko Dodoma
Mbunge ni mwakilishi wa moja kwa moja wa wananchi wengine kwenye chombo rasmi cha kuwasilishia mawazo na maoni ya wakaazi wa nchi wenzake. Kwa hivi ni mtu muhimu katika jamii, japokuwa anabaki kuwa mtumishi wa wananchi, kwani wao ndio hasa wanaompatia ridhaa ya kuwaongoza.

Sasa ili mtu huyu aweze kufanya kazi yake vizuri ni vyema kwa hakika kuwa na mazingira stahiki ya kufanya kazi zake kwa weledi na hasa kwa uzalendo unaojidhihirisha kabisa.

Ili kuwa mbuge kwa Tanzania, tunahitaji mtu mwenye kuwa na sura na mfano wa watu anaowawakilisha ndio maana enzi zile wakaitwa 'ndugu' hivi leo ni waheshimiwa. Pamoja na kufanana na waajiri wake kwa maana ya kuyafahamu vyema mazingira yao na inafaa zaidi akiishi huko huko na wala si mjini tu, inafaa awe na nafasi kiasi ya kiuchumi kiasi ili mambo mengine yanayohusu kazi yake aweze kuyamudu kwa pesa zake mwenyewe. Si saw kila kazi ihitaji kodi za watanzania, hapo ndio has inafaa ajiulize anaifanyia nini Tanzania?

Makala hii imechochewa na taarifa niliyoiona kwene televisheni hivi karibuni na hatimaye kuingia kwenye mtandao wa youtube ikielezea japo kwa kifupi tu hali ngumu kiuchumi ya ndugu zetu wabunge. Hayo yamedhihirishwa na kiongozi wa bunge hilo la Tanzania alipoongea na wananchi wa jimbo lake huko Njombe. Kwa habari zaidi tazama hapa

Kwa hakika jambo hili nimeniacha na maswali mengi kuliko majibu. Kwanini watangaza nia hutumia nguvu na wakati wao mwingi vile kujinadi mbele ya wapiga kura ili wapate nafasi hii yenye umasikini wa kutupa?

Je, wengi wao huenda bungeni bila kujua kuwa kuna umasikini wa kiwango hicho?

Uwezekano mwingine wa suala hili ni kuwa watangaza nia na hatimaye wabunge wetu ni watanzania wenye uzalendo sana na  hakika maslahi ya taifa letu yamo mioyoni mwao kiasi kwamba pamoja na umasikini ulio bungeni, ambao nadhani watakuwa wakiufahamu kwani kwa hali ya kawaida mtu hufanya kwanza utafiti wa kile anachokitatuta, bado huamua kwenda bungeni kwenye umasikini wa kutupa.

Wabunge ni wawakilishi wa moja kwa moja wa watanzania. Na hivi wanabeba sura ya nchi yetu; bunge pale Dodoma likiwa kazini inamaanisha kuwa Tanzania yote kupitia majimbo ipo pale katikati ya nchi hii tukufu, na hivyo wawakilishi hawa lazima kuwajali vilivyo. Sasa kwa kuwa kiongozi wa moja ya nguzo kuu za uongozi wa taifa letu amesema kuwa kuna umasikini katika chombo hicho, itakuwa vigumu kwa hawa watumishi wetu kufanya kazi vizuri. Inafaa tutatue tatizo hili kwa kuwawekea wazalendo na watanzania wenzetu hawa mazingira mazuri ya kufanya kazi. Kwa kuwa tuna uzoefu wa kutatua matatizo yetu wenyewe basi natulitatue njia mojawapo ni kuunda tume kwaajili ya kuchunguza ukata unaowakabili waheshimiwa wetu.

Kupitia uchunguzi huo tupate mwongozo wa nini cha kufanya...
Picha zote kwa hisani ya google!