Wednesday, November 30, 2011

Vijana watanzania: Wamachinga wa China!

Picha kwa hisani ya mtandao

Ukosefu wa ajira za kutosha kwa vijana ndo hasa tatizo kuu linaloipasua kichwa serikali ya Tanzania. Hakuna ajira za kutosha kuwapatia fursa vijana wote wanaomaliza vyuo hapa nchini. Hivi karibuni tumesikia idadi ya wahitimu toka vyuo mbalimbali; kati yao wapo walio na ajira na wasio na ajira; kundi la pili likiwa kubwa zaidi. Wahitimu hao kwa baadhi ya vyuo ilikuwa kama ifuatavyo: Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine, SUA, walihitimu zaidi ya 1000, Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino, Mwanza, zaidi ya wahitimu 2000, Chuo Kikuu cha Dodoma wahitimu lukuki, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wahitimu lukuki pia. na kadhalika. Utaona ya kwamba kila uchao Vyuo vingi zaidi vinazidi kuongeza idadi ya wahitimu na hili ni jambo jema.

Kwa upande mmoja hili ni suala jema sana kwa nchi yetu, kwamba tunapata wasomi wengi zaidi. Lakini jambo hili halifariji sana pale unapoona kwamba wasomi wote ama wengi kati yao wanasubiri tu kuajiriwa. Hapa ndipo penye changamoto kubwa kwa mitaala ya elimu tunayoitumia toka shule zetu za msingi hadi sekondari. Wengi wa vijana wetu kulingana na mitaala tunayotumia ni tegemezi mno kiuchumi, kimsingi elimu wanayoipata haiwakwamui kiuchumi; pamoja na kumaliza kidato cha sita kijana wa kitanzania bado anaomba pesa kwa wazazi ama walezi kwaajili ya matumizi yake ya kawaida kama kununua nguo n.k; hii ni aibu. Mfumo wa elimu inafaa uweze kumfunza kijana kujitegemea, kuweza kuzalisha mali kwa kiwango fulani hata kama ni dhaifu lakini mtaala huo umsaidie kuwa na uthubutu; kijana awe na moyo wa kujaribu kufanya shughuli fulani halali kwa lengo la kuzalisha mali hata kama ni kidogo tu.

STEMMUCO/SAUT MTWARA
Vijana wanaojiunga na vyuo vikuu wengi ni wale ambao wamepitia mfumo wa kuulizwa maswali, kuyajibu na kupatiwa alama basi. Hakuna nafasi ya kutosha ama hakuna tu kabisa fursa kwa wanafunzi kufikiri ama kujifunza kufikiri vya kutosha. Hii ni hatari sana kwa mustakabali wa nchi na ulimwengu, kama taifa tunawajibika kuwapatia wanafunzi wetu fursa nyingi zaidi za kufikiri na kutafakari mambo, wasiyajibu tu kwa mazoea na kupata alama kubwa za juu ilhali hawafahamu masuala hayo kiundani. Na kukosekana moyo wa kujaribu /na kufanya mambo huwafanya hata wanaojaribu waonekane tofauti na jamii kubwa. Mambo haya yanajitokeza pia kwenye maisha yetu ya kila siku. Hapa naangalia shughuli ya biashara ndogondogo na hata zile za kati zinazofanywa na wananchi wengi hususani katika miji mikubwa nchini.

Vijana wengi wa kitanzania wanafanya shughuli za umachinga; naambiwa machinga moja ya tafsiri zake ni ile ya “marching guys” jamaa watembeao (tafsiri si rasmi). Kwa mtazamo wangu hiki ni kitu muhimu kabisa vijana na ndugu wengine wanaofanya shughuli hizo ni kielelezo tosha kabisa cha ulazima wa kuwa na mitaala ya kufunza ujasiriamali (ujasiri wa kutafuta mali kihalali – tafsiri yangu mwenyewe). Ujuzi wa ujasiriamali na hamu ya kufanya majaribio katika masomo uguse aina zote za masomo yaani ya sayansi, sanaa na kadhalika. Kwa kufanya hivyo utaona kwamba hata machinga wetu watafanya mambo kizalendo tofauti na ilivyo hivi sasa.

Bidhaa za Wajasiriamali - twahitaji kuongeza tu
ubora katika bidhaa zetu na mambo yatakuwa
safi. Picha kwa hisani ya blogu la marchingguys

Wengi wa machinga wa Tanzania kwa hakika ni vibarua wa nchi ya Uchina na nchi nyingi zilizoendelea. Wafanyabiashara wengi wanafanya biashara ya bidhaa zinazotoka nje ya Tanzania. Mfumo wetu wa uchumi, kwa kujua ama kwa kutokujua, umetufanya kuwa soko zuri sana la bidhaa za watu wengine. Fikiri kuhusu vitu ulivyonunua juma hili, bidhaa kumi; pengine sita hadi saba zimetoka nje ya Tanzania, japokuwa zinauzwa na wamachinga wetu ambao kimsingi ni vibarua wa uchina, Afrika Kusini n.k. Serikali ina nia njema sana ya kuwasaidia vijana, ndio maana ikaamua kujenga Machinga Complex pale Ilala. Nimesikia kuna mpango wa kujenga Machinga Complex kadhaa katika mikoa mingine kwa lengo lilelile la kuwakwamua vijana na kina mama. Ukiachia mbali kuhusu ufanisi wa jengo hilo, angalia bidhaa zinazouzwa ndani ya jengo hilo, asilimia kubwa zinatoka Jamhuri ya watu wa Uchina, mita chache toka pale Machinga Complex unakutana na iliyogeuzwa kuwa Dubai ya Tanzania Kariakoo, chunguza bidhaa zinazotoka, Dar es Salaam, Tanga, Iringa, Mwanza, Mbeya, Tabora, Arusha, Kilimanjaro, Mtwara n.k; ni chache mno. Hii ni changamoto kubwa kwa nchi yetu; hizi “Machinga Complexes” zinazowalenga vijana wetu inatakiwa ziuze bidhaa zitokazo Kigoma, Iringa, Ruvuma, Manyara, Mwanza, Shinyanga, Rukwa, Njombe n.k - bidhaa za Tanzania. Tazama hata sekta zingine; usafirishaji: foleni za motokaa kwenye majiji hapa nchini; Dar es Salaam, Mwanza na kwingineko pamoja na magari mengi vile, sina hakika kama kuna moja lililotengenezwa pale Kibaha. Tazama baadhi ya miji yetu ilivyojaa na kuwa jaa la pikipiki, bajaji, baiskeli, hakuna zinazotoka Tanzania, lakini wamachinga na wajasiriamali ni wengi kupindukia, huoni kuwa sisi ni wamachinga wa wachina tu!

Sunday, November 27, 2011

Huu ndo uzuri wa akili ya binadamu...

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndugu Jakaya Kikwete akiongea na Ujumbe wa Chama cha CHADEMA

Ni busara sana kwa kiongozi wa nchi kukubali kukutana na viongozi wa chama cha Demokrasia na Maendeleo.

Ni busara hali kadhalika kwa CHADEMA kutoka na wazo la kuomba fursa ya kukutana na kiongozi wa juu wa nchi ili kujadili suala hili la msingi kabisa.

Nini viongozi hao wataafikiana ni suala la kusubiri na kujua. Moja ambalo ni dhahiri kwa hakika itakuwa ni fursa nzuri kabisa ya kuweza kufikia muafaka wa mtiririko sahihi wa utaratibu upi utumike kupata chombo cha kukusanya kuratibu, kujumlisha na kutoa majibu ya mawazo na maoni ya watanzania. Kumbe kuna njia lukuki za kusikilizwa kama sehemu moja inashindikana basi unajaribu njia nyingine. Ni vyema sana kuwa viongozi wa CHADEMA wameamua kufanya hivyo. Muhimu kuliko vyote ni amani ya kweli; amani ya kweli ni utulivu unaoendana na haki, hivyo wananchi tunahitaji utulivu lakini pia na hasa haki na usawa katika masuala yanayohusu maliasili za nchi yetu na maendeleo ya watu wake. Tanzania ni muhimu kuliko chama chochote cha kisiasa, Tanzania itakuwepo tu na si vyama vya siasa.  

Thursday, November 24, 2011

UTANZANIA HALISI

Bendera za vyama kadhaa vya siasa zikipepea nje
ya jengo la Nyumba ya Demokrasia - huko Buguruni Dsm


















Tanzania ni nchi ya kipekee sana hapa duniani. Ndani ya nchi hiyo kuna zaidi ya makabila 120, watanzania hao wana dini nyingi na tofauti tofauti mithili ya nyuki mzingani, itikadi za kisiasa anuwai, kuna vyama vya
kisiasa zaidi ya kumi. Pamoja na mambo yote hayo hulka ya watanzania ni kuishi pamoja bila kujali tofauti zao. Hili ni jambo la msingi na maana zaidi. Utanzania ni muhimu zaidi kuliko dini zetu, itikadi zetu za kisiasa, tofauti zetu za rangi, misimamo yetu ya kitaaluma na kadhalika. Kama jinsi ilivyo kwa Mungu, yeye ni muhimu zaidi kuliko dini ama madhehebu yetu, Mungu hana dini, analojia hiyo tunaweza kuitumia pia kwa Tanzania. Nchi yetu ni muhimu kuliko tofauti zetu zote kama jinsi ilivyo katika vitambaa hivi vyenye rangi tofauti tofauti lakini vyote vinawakilisha watu wa taifa moja la Tanzania. Mungu Bariki Umoja na amani yetu!

Wednesday, November 23, 2011

Nyumbani kwa utajiri na ubinafsi mkubwa?


Nyumbani kwa utajiri mkuu na ubinafsi kupindukia?
Picha kwa hisani ya google


Fikra za watu na tafsiri zao!



Hivi mawingu huko angani hutoa ramani za sehemu mbalimbali
ama hutokea tu yakawa jinzi yalivyo kwa bahati tu? Wataalaam
wa Jiografia tafadhali tunaomba maelekezo ama tafiti kujielimisha zaidi  
Hivi karibuni nimesikia mtu aliyetoa tafsiri ya kuwa barani Afrika kumejaa migogoro inayochelewa kutatuliwa na mingine iliyodumu kwa miongo kadhaa sasa kwa sababu ya umbile la bara hilo. Ndugu huyo amedai kuwa bara la Afrika lina umbile la silaha aina ya bastola. Kwamba umbile hilo linalisababishia bara letu kukosa amani ya kudumu.

Bila shaka huu ni mtazamo wa mtu mmoja. Inafaa kuongelea kitu ambacho mtu amekifanyia tafiti ili kuepukana na taarifa  ambazo hazina ukweli wowote ila tu kuipotosha jamii ya wanadamu. Tujenge utamaduni wa kufanya tafiti za kina na si kwenda kwa sangoma kwa mambo ambayo tunaweza kuyapatia suluhu. Bila kufanya tafiti na kuwaelewesha watoto wetu kwa uhakika mambo tuliyoyatafiti tutajijengea hofu na kuendelea kuwa jamii ya hofu na kuogopana.
  
Wingu hili linaonyesha ramani ya wapi na nini tafsiri yake?

Tuesday, November 22, 2011

Sheria ya Mazingira inaishia wapi...?






Plastiki na chupa za maji zikiwa zimetupwa huku na huko na abiria waliochoka
 kutoka na adha ya usumbufu unaoletwa na ubovu wa eneo lisilo na lami.


Barabara kwa Maendeleo

 

Abiria wa Mtwara - Dar es Salaam wakimbilia mabasi yao
baada ya kukwamulia toka tope lililotamalaki barabarani
Usafiri wa uhakika ni moja ya viashiria vya kimaendeleo. Njia za usafirishaji zikiwa nzuri hurahisisha maisha ya watu na kuharakisha maendeleo ya jamii husika na taifa kwa ujumla. Mtwara ni moja kati ya mikoa ambayo imekiwa kisiwa kutokana na miundo mbinu mibovu kwa muda mrefu. Mtwara inafikika kwa njia mbalimbali; kwa ndege, kwa meli, na kwa barabara. Watu wengi zaidi nchini Tanzania husafiri kwa barabara, japokuwa njia hii ya usafiri imejaa damu. Kujegwa daraja la Mkapa ulikuwa ni ukombozi mkuu kwa ukanda wa kusini. Serikali ya Tanzania imeendelea na juhudi kubwa kuijenga barabara ya Dar es Salaam – Mtwara, zaidi ya kilometa 500 kwa kiwango cha lami.

Matembezi ya hiari yaendelea
Ni kipande kidogo kisicho na lami ndo kinaendelea kuwatesa na kuwanyanyasa wananchi wa ukanda huu maarufu kwa zao la korosho na sasa gesi asilia. Kukamilika kwa ujenzi wa barabara hiyo kutaboresha maisha ya wakazi wa mkoa huo ambao ni tegemezi kiasi kikubwa kwa jiji la Dar es Salaam.

Wednesday, November 16, 2011

UDHAIFU CHAMA CHA WASANII TATIZO KWA MAENDELEO YAO

Na Mwanndishi wa BASATA
Mhadhiri Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino Martin Mandalu akifafanua jambo wakati akiwaeleza wadau wa Jukwaa la Sanaa juu ya utafiti alioufanya kwenye Muziki wa kizazi kipya. Kulia ni  Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari, BASATA, Godfrey Mungereza.







Utafiti uliofanywa kwenye muziki wa kizazi kipya ukilenga kubaini changamoto na mafanikio yake umebainisha kuwa, kukosekana kwa umoja miongoni mwa Wasanii ni moja ya sababu kubwa ya kudumaa kwa maendeleo yao.

Sababu zingine zilizotajwa ni pamoja na Wasanii kutokuzingatia mikataba kwenye kazi zao, utengenezaji wa kazi za sanaa zenye ubora hafifu, usimamizi dhaifu wa kazi zao, kukosekana kwa viongozi thabiti katika tasnia ya muziki na sababu zingine.

Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego akionesha kitabu kilichoandaliwa na Mhadhiri Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino, Martin Mandalu kinachohusu Tasnia ya Muziki Mkombozi Kwa Vijana kwenye Jukwa la Sanaa wiki hii. Kulia ni mtunzi huyo, Bw. Mandalu.

Akiwasilisha utafiti wake alioukamilisha Mwaka huu kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) mapema wiki hii , Mhadhiri Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino, Martin Mandalu alisema kuwa, bila wasanii kuzifanyia kazi changamoto hizo bado kutakuwa na safari ndefu katika kuyafikia mafanikio ya kweli.

Wadau wa Jukwaa la Sanaa wakimsikiliza mmoja wa Wasanii aliyekuwa akihoji sababu hasa zinazowafanya Wasanii wasiwe kwenye umoja pamoja na juhudi zinazofanywa  za kuunda umoja wao.

“Asilimia 80 ya Wasanii waliohojiwa kwenye utafiti huu hawakuwa na taarifa ya uwepo wa umoja unaowaunganisha. Hii ni hatari kwa sababu nilipofika katika vyombo rasmi nilipata taarifa za uwepo wa vyama na mashirikisho ya wasanii. Hii ina maana wasanii hawatambui uwepo wa umoja huo” alisema Mandalu.

Kwa mujibu wa utafiti huo, Wasanii wengi waliohojiwa walikiri kuwa, wamekuwa wakipata mapato kidogo ikilinganishwa na kazi wanazofanya lakini hili likielezwa kuwa linasababishwa na kutozingatia mikataba, kukosekana kwa ushirikiano miongoni mwao na Wasani kutaka kufanya kila kitu yaani utunzi wa nyimbo, usambazaji na hata umeneja.

“Wasanii wengi waliohojiwa walionekana kukosa uongozi na usimamizi thabiti. Walionekana kufanya kila kitu kuanzia utunzi wa nyimbo, kuzifanyia matangazao, kutafuta kazi za maonyesho na umeneja kwa ujumla” alisisitiza Mandalu wakati akifafanua utafiti wake.

Kuhusu utayari wa Wasanii kutoa taarifa au kufika maeneo wanayohitajika, Mhadhiri huyo msaidizi alisema kuwa, ni tatizo kubwa kwani wasanii wengi wamekuwa wazito katika hilo na hata kutokutoa ushirikiano wa kutosha katika masuala yanayowahusu.

“Wengi wa wasanii niliokuwa napanga kukutana nao, walikuwa hawaoneshi ushirikiano. Anaweza kukwambia tukutane saa tano lakini ukifika muda huo anakwambia ana kazi nyingine kwa hiyo haitawezekana” alisema Mhadhiri huyo wakati akieleza changamoto alizokumbana nazo.

Utafiti huo ambao umechapishwa kwenye Kitabu cha Tasnia ya Muziki Mkombozi kwa Vijana umefanywa na Mhadhiri huyo kama sehemu ya kupata shahada yake ya uzamili katika stadi za Maendeleo.

Friday, November 11, 2011

Vimbwanga vya 11.11.11


Bila ubishi hii ni moja ya tarehe za aina yake ambapo kukutana nayo tena katika maisha ya hapa duniani unahitaji kupingana na uzoefu uliopo duniani mpaka hivi sasa. 11.11.11 inatazamwa kwa namna tofauti tofauti na watu tofauti tofauti soma hapa kupata mtazamo wa wanahisabati wanasema nini juu yake.

Vazi la kitaifa na miaka 50 ya Uhuru Tanzania

 Mwanamitindo maarufu nchini Tanzania, Asia Idarous akipita jukwaani na mwanamitindo kuonyesha ubunifu wake katika ufunguzi wa Swahili Fashion week.

Picha kwa hisani ya blogu la michuzi








Umri wa miaka hamsini kwa binadamu si umri haba. Katika umri huo kwa hakika binadamu anaanza kuhesabu mengi aliyoyafanya; lugha yake inaanza kuwa ya wakati uliopita. Utamsikia nilipokuwa fulani, nilipokuwa na kina fulani, nilipokuwa sehemu fulani, nilifanya hivi, nilikuwa hivi... hata hivyo hiyo ni lugha hiyo ni watu tu wa sehemu fulani tu. Kuna wengine ambao husema miaka hamsini ndo kwanza maisha yanaanza na hivyo lugha zao ni zile za wakati ujao, nitafanya hiki, nitakuwa fulani... nita... nita... nita...

 Hata hivyo muhimu zaidi kwa Tanzani hivi sasa ni kuwa baada ya miaka 50 ya Uhuru wa taifa hili ambalo ni nyumbani kwa Serengeti,mlima Kilimanjarokreta ya Ngorongoro, nyumba kwa visiwa vya karafuu Zanzibar bado haina VAZI RASMI la kitaifa. Huu ni wakati kwa wanamitindo na wanasanaa kutumia ujuzi wao kutoa kinachoweza kuwa vazi la taifa na hivyo kuwasaidia watanzania kuwa na vazi lao la kujivunia lenye kubeba na kuheshimu tamaduni zetu. 




Thursday, November 3, 2011

KUMBE KWELI SISI SHAMBA LA BIBI...

Picha kwa hisani ya google
Moja ya makala za HabariLeo katika chapisho lake la leo, imetoa habari inayotufanya nchi yetu kuonekana kama shamba la bibi lisilo na mmiliki...

Bibi ni mama mzazi wa baba ama mama; ni mtu muhimu kwani, huyu pamoja na mumewe ama mwanaume flani ambaye tutamuita babu, ameshiriki moja kwa moja kuwaleta duniani wazazi wetu. Mtu huyu ki-umri amekula chumvi nyingi, na kitamaduni sehemu nyingi barani ni mahiri katika mambo mengi. Ujuzi na busara ya mambo ipo katika uzoefu wa siku nyingi.

Bibi ndiye aliyewalea baba na mama (kila mmoja na mzazi wake - wote waitwa bibi ); hivi basi kwa jinsi wazazi wetu walivyo na nidhamu na utaratibu wa maisha, sehemu flani wamevipata toka kwa bibi. Ni yeye hasa ndio aliyewalea na kupata watoto wenye maadili mema na staha kama tuwajuavyo wazazi wetu. Ni kweli kuwa hupata ujuzi mwingine kwenye mazingira waliokulia, mafunzo sehemu mbalimbali lakini nafasi ya bibi kwa maana ya mzazi na mlezi ni kubwa hasa. Hata hivyo kuna jambo jingine ambalo hushangaza sana toka kwa bibi.

Kina bibi wengi wanaelezewa kama watu wenye kuwadekeza kupindukia watoto wa watoto wao; wajukuu. Kiasi cha kuwadekeza huko, huwashangaza watoto wao yaani baba na mama zetu, ambao mara nyingine hulazimika hutoa simulizi za namna ambavyo bibi alivyokuwa mkali enzi za malezi yake kwao. Kuna sababu kadhaa zinazoeleza kwanini bibi anakuwa mpole na rafiki mno kwa wajukuu zake. Moja ya sababu hizo ni uzee, uchovu na upweke wa utu uzima. Bibi anawahitaji watoto wa watoto wake ambao kwake ni marafiki; ili kuwapata mara nyingi huweza kutumia rasilimali alizonazo kuwaweka kwenye himaya yake. Ni kupitia mwanya huo basi mali za bibi huweza kutumika vibaya; kuharibiwa, kuhujumiwa, kila mmoja akachukua anachotaka na tena kwa nafasi yake. Katika hili bibi hajali mali yake inaharibiwa kiasi gani, muhimu kwake ni kujenga mahusiano na wajukuu wake wakiharibu ama wasiharibu hilo si muhimu kwake muhimu ni kwamba uhusiano wa kirafiki na wajukuu unakuwa bora zaidi na zaidi. Ni kutokana na masuala hayo ndo analojia ya shamba la bibi ikazuka.

Habari Leo hivi leo wametoa taarifa yenye kufanana na analojia ya shamba la bibi. Hapa nchini, katikati ya kitovu cha uchumi wa nchi, Dar es Salaam kumekuwa na shule ikiendeshwa kinyume na sheria kwa miaka kumi na miwili. Hii inaweza kuwa kipande cha pande kubwa la “jabari” la barafu baharini. Si ajabu kuna mengi ambayo hayajagunduliwa na tena yenye madhara makubwa kwa taifa.  Nchi ina mali asili nyingi tena za kila namna; je ni namna gani rasilimali hizo zinaendeshwa katika namna inayowanufaisha wananchi walio wengi na taifa kwa ujumla wake.

Tanzania ina mbuga lukuki za wanyama pori, je shughuli za kiuchumi za wanyama pori zinafanyika kwa jinsi inayotakikana? Je, taifa linapata pato stahiki? Tanzania ina bahari, maziwa, mito na mabonde yenye uwezo wa kunufaisha taifa kwa namna anuwai; je watu waliokabidhiwa madaraka kuendesha vyanzo hivyo vya mapato wanaitendea haki jamii na taifa kwa ujumla? Je, shughuli hizo zinaendeshwa katika namna endelevu? Ili kwamba wajukukuu wa wajukuu wetu wakute mali hizo ama faida zake na wao pia wamudu kuendesha maisha yao kwa furaha? Tunaweza kuorodhesha utajiri na zawadi nyingi zilizopo nchini  hata hivyo si nia yangu kufanya hivyo lengo ni kukumbushana juu ya taifa letu na mustakabali wake.

Kuhitimisha tunasema kuwa kila mmoja wetu awajibike kizalendo ili kulinda na kutetea maslahi ya taifa letu la Tanzania, na kuboresha maisha ya jamii ya wanadamu wanaoishi sasa na wale watakao kuja baadaye kwa taratibu na sheria zinazokubalika.

Monday, October 31, 2011

KIBANGA AMPIGA MKOLONI

Na. Maisha na Mafanikio
Zamani za ukoloni, palitokea Mzungu mmoja. Mzungu huyo hakuwa mtu mwema. Alikuwa mkali na mkatili sana. Kwa ajili ya ukatili wake watu walimwita mkoloni. Wanancgi wote walimchukia sana popote pale alipokwenda.


Mzungu huyo alikuwa Bwana Shamba. Alikuwa na bakora iliyokuwa imetengenezwa kwa mkwaju. Kila alipokwenda kukagua mashamba, alikuwa na bakora hiyo mkononi. Alipendelea sana kuitwa "Bwana Mkubwa". Mkolono huyo alifurahia sana kupiga watu. Aliwapiga watu waliposhindwa kupalilia mashamba. Aliwapiga pamba yao ilipokuwa chafu. Aliwapa taabu sana.

Friday, October 28, 2011

Mtwara by Night

Mmoja wa mitaa ya mji wa Mtwara ukiwa ndani ya giza licha ya umeme wa uhakika mkoani humo- mipango miji wako wapi?

















Mkoa wa Mtwara ni moja kati ya mikoa michache nchini Tanzania isiyofahamu kadhia ya mgawo wa umeme. Mkoa haujaunganishwa kwenye mfumo mmoja wa taifa, hapa ni kwa faida ya wakazi wa Mtwara. Kwani hakuna maana kuwa chanzo cha umeme na usiupate umeme huo. Kwa Mtwara ni tofauti na maeneo yenye utajiri mkubwa ilihali watu wake hohehahe wa kutupwa.

Mkoani Mtwara kuna umeme utokanao na gesi asilia; gesi hii asilia inapatikana mkoni humu na hii inajidhihirisha kwa wakazi wa mkoani humo kwani hakuna mgao. Nafahamu kuwa hii ni hali ambayo wakazi wa mikoa mingi wangependa kuiishi. Na katika hali ya kawaida, ungetarajia kukutana na mitaa yenye kumulikwa vyema na taa nzuri za barabarani nyakati za usiku, lakini hali si hiyo. Nyakati za usiku mjini Mtwara kuna giza kubwa sawa sawa na mikoa yenye mgao wa nishati hiyo muhimu kwa maendeleo ya binadamu. Wazo kwa wahusika wakuu hususani wapanga maendeleo ya mji, wajipange na kuweka taa za barabarani katika mitaa ya mji huo wa kusini mwa nchi yetu ili kuupendezesha mji huo, kuongeza usalama wa mji na hivyo kuvutia wawekezaji wengi zaidi mjini humo.

Elimu kwa Maendeleo

Wanafunzi wa Stella Maris Mtwara University Collegge wakijisomea katika maktaba mpya ya chuo hicho.

Tuesday, October 18, 2011

WASANII WATOA ELIMU

Msanii wa Kundi la Orijino Komedi, Lucas Mhavile ‘Joti’ akisisitza jambo wakati akizungumzia Changamoto anazokumbana nazo kwenye Sanaa ya Vichekesho anayoifanya.


 
 
Picha na maelezo kwa hisani ya BASATA

BASATA NA HAKI ZA WASANII

Meneja Mzalishaji wa Kundi la Vichekesho la Orijino Komedi, Sekion David ‘Seki’ (aliyesimama) akiongea na wadau wa Jukwaa la Sanaa wiki kwenye Ukumbi wa BASATA.Wengine kutoka kulia ni Kaimu Mratibu wa Jukwaa hilo, Aristide Kwizela, Msanii Lucas Mhavile ‘Joti’ na Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari, BASATA Godfrey Mungereza.

Picha zote na maelezo kwa hisani ya mwandishi wa BASATA

BASATA YAWATAKA WASANII KUJITAMBUA

Na Mwandishi  BASATA
Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewataka wasanii kujitambua kwa kuwa na mipango ya muda mfupi na mrefu katika kazi zao na kutambua thamani yao.

Akizungumza wiki hii kwenye Jukwaa la Sanaa linalofanyika makao makuu ya BASATA, Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari, Godfrey Mungereza alisema kuwa, kujitambua kwa msanii ni mwanzo wa kuipa kazi yake thamani kubwa kuliko ilivyo sasa ambapo wasanii wamekuwa wakikubali kulipwa malipo kidogo.

“Sanaa ni kazi, sanaa inalipa, ni lazima wasanii wawe na mipango ya muda mfupi na mrefu. Muhimu ni kwa wasanii kutambua thamani yao na kazi wanazozifanya. Ifike mahali wasanii watambue thamani yao ni nini” alieleza Mungereza...

Friday, October 14, 2011

Julius Kambarage NYERERE (1922-1999)







Huko Tanzania, Oktoba 14 ya kila mwaka imetangazwa kuwa siku mahususi ya kumkumbuka na kumuenzi Julius Kambarage Nyerere, maarufu zaidi, Mwalimu Nyerere, ni siku aliyofariki huko Uingereza mwaka 1999. Rais wa kwanza wa nchi hiyo, MwanaAfrika na mjengadunia halisi; mpigania uhuru wa nchi nyingi barani humo, mwanafalsafa, mwandishi, mzalendo, mcha Mungu na binadamu mwadilifu.

Mwalimu ni mmoja kati ya viongozi wachache wa kiafrika aliyekuwa kwenye mamlaka kwa muda mrefu. Alikuwa waziri mkuu wa kwanza wa Tanganyika mara tu baada ya kupata uhuru 1961  (1962 -1985) bila kujilimbikizia mali kama wafanyavyo viongozi wengi barani humo, mwalimu hakuwa mbinafsi. Alijitahidi kuishi vyema na kufuata misingi ya fikra za ujamaa na kujitegemea alizoziasisi.




Mwalimu pamoja na wenzake aliasisi Azimio la Arusha ambalo lilitoa maelekezo ya kuliongoza taifa ikiwa ni pamoja na maadili ya viongozi. Hii ilisaidia kuongoza nchi kwa uadilifu na ubadhilifu ulidhibitiwa kwa umakini, “Awamu ya kwanza rushwa ilikuwepo, lakini mtoa na mpokea rushwa wote walitiwa msukosuko mkubwa,… aliyebainika kupokea rushwa alicharazwa viboko 24, kumi na viwili kabla ya kwenda gerezani na kumi na viwili akimaliza kifungo chake ili akamwonyeshe mke wake…”

Julius Nyerere alikuwa na fikra binafsi ambazo aliziasisi, moja ya fikra hizo ni ile ya Ujamaa na kujitegemea. Katika nadharia hii Mwalimu alilenga kujenga taifa lenye uwezo wa kujipatia mahitaji yake lenyewe bila kutegemea sana mataifa ya ng’ambo. Mwalimu alijaribu kusimamia nadharia hiyo kwa mfano hata kama haikufanikiwa kama ambavyo angependa.

Zaidi Mwalimu aliwaunganisha watanzania wenye makabila zaidi ya miamoja na ishirini; wakati Tanganyika ikipata uhuru, kulikuwa na vijitaifa vingi, hivyo kazi aliyoifanya Mwalimu na viongozi wenzake ilikuwa ni kuunganisha mataifa hayo madogo madogo kuwa taifa moja kubwa. Kazi hiyo nzuri ilisaidia kuliepusha taifa hili la Tanganyika, na kisha muungano wa Tanganyika na Zanzibar 26. 04. 1964, Tanzania, toka kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe ambazo zimesambaa kote barani Afrika.

J.K Nyerere aliasisi mbio za Mwenge kwa tukio lenye hisia, kumbukumbu, na ujumbe mzuri hasa. Mwenge huo wa uhuru ulisimikwa kileleni mwa mlima mrefu kuliko yote barani Afrika; Kilimanjaro. Ni kapteni Alex Nyirenda wa jeshi la wananchi wa Tanganyika ndiye aliyefanya kazi hiyo nzuri. Akihutubia mjumuiko wa Umoja wa mataifa Mwalimu Nyerere alisema sisi tumeamua kuuwasha mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro ili umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete tumaini pale walipokata tama, heshima palipojaa dharau (si maneno halisi)…………Ni dhahiri kuwa makala hii ni fupi mno kumuelezea mmoja wa waasisi wa taifa tukufu la Tanzania. Hata hivyo jambo la msingi ni je, tunamuenzi  kwa kiasi gani Mwalimu Julius Nyerere?

Miaka kadhaa baada ya kifo cha Mwalimu, Tanzania inaendelea kumuenzi mzee huyu aliyefanya mambo mengi makubwa kwa taifa hili la Afrika Mashariki, lenye utajiri mkubwa japokuwa utajiri wake hauwafikii wote kwa usawa. Taifa linaendelea kumuenzi sana Mwalimu kwa sifa na sherehe zenye mbwembwe nyingi kote nchini. Lakini hatumuenzi Mwalimu kwa mambo ambayo yeye mwenyewe aliyataja kama muhimu kufikia maendeleo ya kweli ya watu. Kwani lengo kuu la kuongoza nchi ni kuleta maendeleo kwa wananchi; mwalimu alisema ili tuendelee tunahitaji mambo manne;

1. Watu,

2. Ardhi,

3. Siasa safi na

4. Uongozi bora

Ili nchi zetu ziweze kuendelea tunawahitaji watu wenye elimu nzuri, afya njema, chakula cha kutosha na mahitaji yao muhimu ya kila siku ili kushiriki katika ujenzi wa taifa lao, jamii ya wanadamu na dunia kwa ujumla wake. Lakini hivi leo watu wengi wa nchi hiyo bado hawana huduma za lazima kufikia wanapotaka kufika.
















Ardhi, ni chanzo cha vyakula vingi anavyotumia binadamu na ni sehemu ambapo shughuli za kijamii na kimaendeleo za binadamu hufanyikia. Hii leo hiyo yenye utajiri, rutuba na mengine muhimu wanapatiwa wananchi wachache wenye pesa nyingi na wageni wenye mapesa na ushawishi mkubwa.

Siasa safi na uongozi bora ni tunu muhimu na za lazima kwa maendeleo ya watu…tunu hizo zimepiga hatua kubwa kwa malengo nia ile ile ya kuleta maendeleo kwa watanzania. Hata hivyo bado kuna mapungufu katika nyanja hiyo ya siasa safi na uongozi bora; kwa hivi kuna haja ya kuendelea kufanya marekebisho kwenye suala hili la uongozi. Hivi leo huko Tanzania, siasa inaonekana kama ni ajira yenye kuleta kipato kikubwa kwa haraka, matokeo yake watu wengi wenye kutaka utajiri wa haraka haraka, ikiwa ni wasomi, wafanyabiashara, wakulima hukimbilia siasa hata kama hawana wito huo. Viongozi wengi hivi leo hawana maadili sahihi ya uongozi, wameingia siasa kwa malengo mbalimbali; wengine wameingia kulinda biashara zao, wengine kujiongezea heshima tu na kulinda malengo yao binafsi. Azimio la Arusha lilitoa mwongozo namna gani kiongozi aongoze watu wake. Siasa safi na uongozi bora ni muhimu mno kwa maendeleo ya kweli ya WATANZANIA WOTE! Hivyo lazima kuwe na namna flani ya Azimio la Kujenga maadili ya viongozi nchini!

Picha kwa hisani ya tovuti ya nyerere.info

Thursday, October 13, 2011

MUDA WA KUSAKA FIKRA ZAIDI


Mtaalamu wa burudani za mafunzo akiburudisha na kuelimisha wageni waalikwa siku ya hiyo ya ufunguzi wa mwaka wa masomo.

         MJ wa Mtwara hakukosa kwenye orodha ya waelimisha jamii wa siku                                      
   



                                                                                                                                                                
Burudani hii murua ilitufunza namna ya kupokea tofauti na vipaji vyetu na kuendelea kuishi kati jumuiya moja kwa upendo na mafanikio. Burudani nyingi zilitolewa na kundi hili maarufu la SAUT TRAVELLING GROUP (STG)




MUDA WA KUSAKA FIKRA ZAIDI

Picha kwa hisani ya blogu ya mdau Muliriye

Jumatatu ya 10.10.2011 ilitumika kufungua mwaka wa masomo Chuo Kikuu Cha Mtakatifu Agostino – Mtwara. Masomo ni njia ya kumwezesha mtu kugundua vipawa vyake na kuvitumia kwa malengo yale yale ya kuweza kuitawala dunia na vilivyomo humo ilikuboresha maisha ya jamii ya wanadamu.

Elimu ya Chuo Kikuu, kwa kutumia maneno ya Mwalimu Nyerere, ni elimu hasa yenye malengo ya kumfunza mtu kuwa na fikra bayana, kuwa na uhuru wa fikra, kuchanganua, na kutatua matatizo kwa kiwango cha juu kabisa, haya ni mawazo ya Mwalimu kwa maneno yangu. Kwa hivi basi elimu ya Chuo Kikuu imjenge kijana kuwa na fikra binafsi na tena zenye nia ya kuiendeleza jamii ya wanadamu.

Kumbe elimu hiyo ya juu haina lengo la kumfanya mwanafunzi akariri, lengo kuu ni kumfanya awe na uwezo wa kujenga fikra binafsi, zenye kuweza kuijenga jamii na awe na uwezo wa kuyatetea na kuyasimamia mawazo yake, kwa kufanya hivyo ndio tunaweza kupata wagunduzi (wavumbuzi), wanasayansi na watu waliotayari kuijenga dunia.

Huko SAUT Mtwara, shughuli za kuanza mwaka wa kuendeleza ujenzi wa fikra mpya ulianza kwa kuomba msaada wa Mwenyezi Mungu na kisha kufuatiwa na shughuli mbalimbali za kijamii.



Baadhi ya wageni mashuhuri wakielekea eneo la tukio


Wageni Maarufu na mashuhuri mno walikuwepo, hapa Profesa kijana akiwa na wadau wengine wakielekea eneo la tukio katika viwanja mahususi kwa tukio la siku

Hapo chini wadau wakiimba wimbo wa Taifa kabla ya kuanza shughuli yenyewe