Monday, October 29, 2012

Mhadhara wa Katiba CHUONI STEMMUCO

Nchi ya Tanzania,  inaendelea na mchakato wake wa kuandika katiba mpya yenye mguso wa moja kwa moja toka kwa WaTanzania walio wengi. Katika juhudi hizo wadau mabalimbali ikiwa ni pamoja na taasisi, watu binafsi na kadhalika wanafanya juhudi kuwaelimisha wananchi walio wengi na wasio na ujuzi na uelewa wa katiba inayotumika nchini hivi sasa. STEMMUCO kwa nafasi yake imefanya kazi hiyo ya kuwaelimisha wanachuo juu ya katiba inayoiongoza Tanzania kwa sasa. Idara ya sheria, chuoni hapo imeongoza mhadhara wa wazi kwa wote waliopenda ili kuielezea katiba hiyo.








Thursday, October 25, 2012

MCHWA NA MAENDELEO MTWARA

Nguzo yenye kusambaza nishati ya umeme ikisaidiwa kazi hiyo na mti jirani
Manispaa ya Mtwara - Mikindani ina utajiri mkubwa wa kila namna. Kwa uchache utajiri huo unajumuisha, ujuzi wa uchongaji vinyago, ngoma za aina yake, mazao ya kibiashara; korosho, karanga na kadhalika, mali asili lukuki, kina bandari asilia, gesia asilia na kadhalika na kadhalika.





Mchwa ni moja ya utajiri mkubwa wa Mtwara, wataalamu wa masuala ya viumbe hai tunawaomba wafanye tafiti zinazowalenga mchwa kuona ni namna gani Mtwara -Mikindani na taifa kwa ujumla linaweza kunufaika na viumbe hawa. Wapo karibu kila sehemu na hushamiri zaidi kipindi cha ukame, huvamia karibu kila kitu kikavu kilicho mbele yao.





Sehemu ya nguzo iliyooza kwa karibu inavyoonekana


Hii nd'o nguzo iliyooza vibaya kwenye picha ndogo hapo juu

Katika pitapita zangu nimekuta mji kati kabisa wakiwa wamekula nguzo zisambazazo nishati ya umeme na sikuona juhudi za maana zikichukuliwa kunusuru linaweza kuwa tishio la maisha mjini humo.

Thursday, September 27, 2012

SIKU YA UTALII TANZANIA NA DUNIANI

Kazi ya Sanaa Mji mkongwe MIKINDANI
Wanayama wakivuka mto huko Serengeti - Tanzania



Sanaa MIKINDANI - MTWARA

Faru weusi huko Ngorongoro - Tanzania





















Leo ni siku ya UTALII TANZANIA NA DUNIANI: Utalii ni moja kati ya vyanzo vikubwa vya uchumi duniani. Kuna nchi kadhaa ambazo hutegemea tu uchumi kujiendesha na kuendelea kuwepo. Kikubwa ni uwekezaji wa makusudi na lazima katika sekta hiyo yenye uwezo wa kuzalisha ajira lukuki. Tanzania ina mali asili nyingi mno ambazo ni vivutio tosha vya utalii; moja ya mambo yanayoturudisha nyuma katika hili ni uwekezaji hafifu kwa watu wetu.

 Uwekezaji huu utazame kwa makini hasa aina ya elimu tuitoayo kwa wanafunzi wetu; kwa kuwa tuna vivutio vingi vya utalii basi tuwe na mitaala yenye kulenga utalii toka shule ya msingi. Shule zetu ziwe na michepuo yenye kuendana na mahitaji ya karne ya ishirini na moja. Kuwe na shule zenye kuangazia masomo ya sayansi na teknolojia yenye kujibu mahitaji ya moja kwa moja ya watu wetu. Tukirudi kwenye utaliii, shule na mitaala yenye kufunza huo utalii zianze mapema kufunza yaliyo ya lazima; uaminifu, ukarimu, lugha za kigeni, na mengine muhimu hiyo itasaidia kutumia vyema rasilimali na utajiri mkubwa tuliopatiwa na Mwenyezi Mungu, kinyume na hivyo tutaendelea kuwalaumu majirani waliojipanga kunufaisha jamii zao na hiyo nd'o hasa jukumu la serikali.    


Friday, September 21, 2012

Mashindano ya Hisabati, kemia, Fizikia, Jiografia n.k

Msaani Akitoa burudani kwa umma- Mashindano ya mavazi, mavazi sahihi- picha kwa hisani ya google?
Hapa duniani kila jamii ina aina fulani ya burudani na hiyo muhimu kwa maisha ya binadamu. Hata hivyo maisha ya nchi na watu wake ili yaweze kwenda mbele na nchi kupiga hatua za kimaendeleo ni muhimu ikawekeza kwa kiasi kikubwa zaidi katika elimu. Elimu kama tuambiawavyo nd'o ufunguo wa maisha. Elimu ndio inaweza kuwaweka sawa, kwa kiasi fulani, watoto wa tajiri na wamasikini. Ni kupitia hiyo elimu ndo mambo mengi iwe ni burudani; muziki, mpira, urembo, sana ya mavazi, iwe ni mawasiliano, sheria, tiba, taja tasnia zote; zinahitaji elimu ili kufanya vyema zaidi.

Nchini Tanzania, nchi yangu hii, kwa maoni yangu naona elimu hatuipatii fursa ya kutosha; ni kweli Serikali na wadau wengine wengi wanajitahidi kwa kiasi kikubwa kutoa huduma hiyo muhimu kwa jamii. Hata hivyo juhudi mara dufu bado yahitajika. Kuna njia na mbinu nyingi elimu inaweza kuiga toka kwenye kada nyingine hapa nchini.

Kwenye Muziki, filamu na sekta nyingine, wadau kadhaa wameanzisha tamasha maalumu kutafuta vijana wenye vipaji, na tamasha hizo zinafanywa kwa mbwembwe,ubunifu na bila shaka udhamini mkubwa na wenye gharama kubwa tu. Jambo hili ni jema sana kwani shughuli hizi zinachangia kuwakwamua vijana toka kwenye kukosa ajira na kuweza kupata kipato ambacho bila shughuli hizo wasingekipata.  Hata hivyo wazo na wito wangu: kuibuke wadau wengine watakao fanya mashindano ya vijana kwenye hisabati, fizikia, baiolojia, jiografia, kiswahili... wazunguke mkoa mmoja hadi mwingine kupata wataalamu wa hisabati, na kadhalika. Kufanya hivyo kutatuwezesha kupata teknolojia na kujenga hamu ya kubobea na kujikita zaidi  katika ulimwengu wa sayansi na teknolojia.   

Monday, August 27, 2012

Wasanii watakiwa kujiendeleza kitaaluma


Na Mwandishi BASATA

Mkufunzi wa masuala ya uandaaji wa Filamu Ngalimecha
 Ngahyoma akizumza jambo na wadau wa sanaa
ukumbi wa Basata

Wasanii wa nchini wametakiwa kujiimarisha katika masuala ya taaaluma ili waweze kufanya kazi zenye ubora na zinazokidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchini.

Akizungumza katika Jukwaa la Sanaa jana, mkufunzi wa masuala ya uandaaji wa filamu hapa nchini Ngalimecha Ngahyoma amesema kumekuwa na matatizo mengi katika uandaaji wa kazi za filamu hapa nchini kutokana na wasanii kutokuelewa misingi ya uandaaji wa filamu.

“Kuna maeneo ya msingi ambayo yanahitaji watu kubobea ili kuyafanya kwa utimilifu, na hakuna njia ya mkato ni lazima kuyapata shuleni kwa maana lazima mtu ufundishwe. Wasanii wengi wanatumia vipaji vyao, lakini matokeo ya kufanya mambo kwa vipaji ndiyo haya ambayo yanatupa filamu zenye matatizo katika maeneo mbalimbali,” alisema.

Tuesday, August 7, 2012

BASATA LAKERWA NA WASANII KUNG’ANG’ANIA FILAMU NA MUZIKI PEKEE

BASATA LAKERWA NA WASANII KUNG’ANG’ANIA FILAMU NA MUZIKI PEKEE


Na Mwandishi wa BASATA

Sehemu ya wadau waliohudhuria kwenye Jukwaa la Sanaa
wiki hii wakifuatilia kwa makini programu
Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limeeleza kusikitishwa na hali iliyopo sasa ya wasanii kuzipa kisogo Sanaa zingine na kung’ang’ania filamu na muziki pekee hali inayowafanya wengi wao kubaki wakihangaika na kulalama.

Akizungumza wiki hii kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa inayofanyika makao makuu ya Basata, Katibu Mtendaji wa BASATA Ghonche Materego alisema kuwa, ni jambo la kushangaza kuona wasanii wakifunga milango yote katika sekta ya Sanaa na kubaki wakihangaika na madirisha mawili tu ya filamu na muziki.

“Ndugu zangu hebu tujiulize tu, Sanaa ni pana sana na ina fursa nyingi katika kutupa ajira na kuzalisha kipato kwa vijana wengi lakini kwa nini wote tunang’ang’ana na filamu na muziki pekee? Fursa nyingine tunamwachia nani? Alihoji Materego.

Monday, August 6, 2012

Wabunge ‘wala’ rushwa marufuku kuingia China

Bunge la Tanzania Mjini Dodoma















Tumeambiwa na tunafahamu siku zote kuwa rushwa ni adui wa haki, na ni ya wananchi, ya binadamu, ama ya viumbe vilivyo hai walau kulingana  na miongozo na makubaliano yetu. Moja ya makubaliano hayo, kwa Tanzania ni kuwa rushwa ni adui wa haki, na kwenye kanuni/ ahadi za mwanaTANU (chama kilichopigania uhuru wa Tanganyika) kulikuwa na ahadi ya kutotoa na kutopokea rushwa kwani hupinga ama huzuia watu wengine kupata haki zao.

Katika nchi nyingi duniani, Tanzania ikiwa mojawapo, kuna utaratibu wa kuwa na chombo cha kutolea mawazo, kuihoji serikali iliyo madarakani, kutunga sheria n.k. Chombo hicho kinafanya kazi kwa uwakilishi; si rahisi kwa mwananchi mmoja mmoja kuingia katika chombo hiko kutetea, kudai haki yake ama/ na kufanya shughuli zingine za chombo hicho ambazo kwetu kinajulikana kwa jina la BUNGE. Kwa kuwa si rahisi wote kuingia basi tumelazimika kuwa na wawakilishi wachache ili wawe SAUTI zetu na waseme na kutenda kwa niaba yetu. Hivi karibuni tumesikia habari ya kushangaza juu ya hawa wawakilishi wetu. Tumesoma na kusikia vyombo vya habari vikielezea juu ya baadhi ya wawakilishi wetu hawa wakifanya kile tulichofundishwa kuwa ni adui wa haki, sio lengo la makala hii kuongelea suala hilo bali tu kuiwasilisha makala iliyo katika gazeti la MTANZANIA inayoeleza juu ya kicha habari.   

Mwalimu JKNyerere aliwahi kusema IKULU ni patakatifu nadhani BUGENI halikadhalika ni vivyo hivyo. Je, kama kweli kuna wabunge wameenda kinyume na utakatifu inafaa kweli waendelee kuwepo patakatifu?

Na Arodia Peter .

TUHUMA za rushwa zinazoendelea kuwaandama wabunge, zimechukua sura mpya, baada ya Serikali ya China kujiandaa kupiga marufuku wabunge wote wanaotuhumiwa kujihusisha na rushwa kuingia nchini humo.

Habari za uhakika ambazo MTANZANIA imezipata kutoka ubalozi wa China hapa nchini, zinasema umepokea taarifa rasmi kutoka kwa viongozi wakuu wa China, wafuatilie kwa karibu wabunge wote wanaotuhumiwa kwa rushwa, kisha watume taarifa ili wakibainika wasiingie kwenye nchi hiyo.
“Tumeletewa taarifa na viongozi wetu wa ngazi za juu, kuwa tufuatilie kwa kina wabunge wote ambao wanatuhumiwa na wakibainika majina yao yatumwe China, ili wazuiliwe kuingia kule,

…unajua taifa letu ni taifa ambao halina mchezo na mtu anayepokea rushwa ovyo ovyo na ni kosa la jina. kwa kiongozi kama hawa wabunge kujihusisha na siasa,

“Kwa kipindi chote hiki, kama wabunge hawa wangekuwa China leo hii, tungekuwa tunazungumza mambo mengine, wangekuwa wamechukuliwa hatua kali,

“Tunashangaa kuona kwa nini hapa kwenu, bado wanaendelea kuruhusiwa kuingia bungeni… au wanasubiri majibu ya kamati ndogo iliyoundwa kuchunguza tuhuma hizi,” kilihoji chanzo chetu.

Chanzo hicho, kilisema ubalozi wa China hapa nchini, umetuma maofisa wake mjini Dodoma kwa ajili ya kupata mwenendo wa wabunge wote wanatuhumiwa.

“Hivi sasa hapa Dodoma kuna maofisa wa ubalozi wa China, wanaendesha uchunguzi kuhusu tuhuma hizi, ikibainika ni za kweli baada ya majina ya wabunge ‘wala rushwa’ kutajwa, watachukua picha zao kwa ajili ya kuzituma China, ambako hawataruhusiwa kukanyaga kwa sababu kwao rushwa ni kosa la jinai,” kilisema chanzo chetu.

Naye Mratibu wa maombi yanayoendeshwa na Umoja wa Makanisa ya Kikristo Tanzania, mjini Dodoma Mchungaji William Mwamalanga alisema kwa kauli moja viongozi wa dini, wamesikitishwa na tuhuma hizo.

Alisema viongozi wa dini ambao wamepiga kambi mkoani Dodoma, kwa ajili ya kuliombea taifa, wamewataka wabunge wote waliotajwa wajiuzulu mara moja.

“Viongozi wa madhehebu mbalimbali tupo hapa Dodoma, kwa ajili ya kuliombea taifa, lakini moja ya jambo kubwa ambalo tumekubaliana kupita katika majimbo yao, kueleza waumini wetu matatizo haya ya rushwa… tunataka wajiuzulu kwa ajili ya kulinda heshima zao,  

Saturday, July 28, 2012

TAARIFA YA SERIKALI KUHUSU KUSUDIO LA WALIMU KUGOMA


SERIKALI kupitia Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi leo, Ijumaa, Julai 27, 2012 majira ya saa tisa alasiri, imepokea notisi ya saa arobaini na nane (48) ya kusudio la walimu wanachama wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kugoma kuanzia Jumatatu tarehe 30 Julai 2012 saa moja na nusu asubuhi.

Kabla ya notisi hii kutolewa, Serikali imekuwa ikifanya jitihada nyingi za kujadiliana na viongozi wa CWT kuhusu jinsi ya kuboresha maslahi ya walimu kwa nia ya kumaliza suala hili kwa maelewano kwa kutumia vyombo na ngazi mbali mbali za kisheria.

Kwa sasa, shauri hili liko Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na leo hii siku ya Ijumaa tarehe 27 Julai, 2012 majira ya saa sita mchana pande zote mbili zilifika Mahakamani, na Mahakama ikaamuru kwamba pande zote zikamilishe maelezo yao ifikapo siku ya Jumanne tarehe 31 Julai, 2012 saa sita mchana, ili kuiwezesha Mahakama kuendelea kusikiliza shauri hilo na hatimaye kutoa uamuzi.

Kwa hiyo, Mgomo huu siyo halali kwa sababu shauri hili bado liko Mahakamani.

Kwa msingi huo hatua ya CWT kutoa notisi ya kuanza kwa mgomo kabla ya kukamilika kwa shauri hili ni kukiuka taratibu halali za Kimahakama ambazo kila mmoja anawajibika kuziheshimu.

Serikali inapenda kuwafahamisha walimu wote kuwa kujihusisha na mgomo huu ni kwenda kinyume cha Sheria, Kanuni na Taratibu za kazi. Hivyo, walimu wanapaswa kupima madhara ya mgomo huu usiokuwa halali na Serikali inawataka walimu kupuuza mgomo huo na kutokujihusisha nao. Walimu wote wanatakiwa waendelee na kazi kama kawaida.



Peniel M. Lyimo
KAIMU KATIBU MKUU KIONGOZI
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
27 Julai, 2012

Tuesday, July 17, 2012

MKUTANO WA WAKUU AFRIKA WAMALIZIKA


Viongozi wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika Jijini Addis Ababa.
Viogozi wa Afrika wakimaliza mkutano wa 19 wa kawaida wa Umoja wa bara hilo makao makuu ya Umoja huo jijini Addis Ababa. Pamoja na kumchangua kiongozi mpya mtendaji bi Nkosazana Dlamini-Zuma, ambaye anakuwa mwanamke wakwanza kuuongoza umoja huo, viongozi hao wamekubaliana pia kuangalia na kuifanyia kazi migogoro mikubwa miwili inayoendelea barani humo. Mgogoro ule wa kaskazini mwa Mali na ule wa Mashariki wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Kiongozi mpya wa Umoja wa Afrika
bi Nkosazana Dlamini Zuma picha kwa hisani ya blogu wadau

Mama Nkosazana Dlamini Zuma akifurahia jambo. Picha na wadau

 












Friday, June 22, 2012

Nafasi ya Masomo ya juu zaidi



Wanachuo wakifanya mitihani yao Picha kwa Hisani ya wadau wa blogu
Wanavyuo katika vyuo kadhaa nchini Tanzania hivi sasa wanaendelea na mitihani yao ya mwisho wa mwaka.

Tunawatakia mafanikio katika mitihani yao. Mitihani kwa maoni yangu si kipimo bora zaidi kuliko vipimo vingine, ila ndo kipimo cha uelewa kinachokubalika, inawezekana kabisa kukawa na njia nyingine bora zaidi lakini bora hazijakubalika.

Kwa kuwa mitihani ndo njia inayokubalika kupima uwezo wetu basi tuiheshimu na kuifanya kwa bidii na maarifa. Bidii na maarifa vinatakiwa kuja wakati wa maandalizi ili kuweza kumudu na kutawala somo kabla ya kuingia chumba cha mitihani. Ni m uhimu kufanya hivyo ili kujiamini katika kufanya mitihani, kuthibitisha utu na maadili yetu. Ni vyema mtu akafanya mitihani yeye mwenyewe bila kutumia vyanzo visivyoruhusiwa. Kufanya hivyo ni kipimo cha utu bora na faida kwa taifa na dunia kwa ujumla, kwani viongozi na watu wema wamo miongoni mwa wanavyuo wanaoendelea na mitihani yao hivi sasa.

Ili kujijenga zaidi kitaaluma nhapa chini kuna nafasi ya masomo ya uzamili kwa wanaopenda ila nafasi ijazwe haraka kwa kuwa muda umekwisha. Fanya haraka kupata nafasi hii:

 
MASTERS STUDIES - MPhil in African Studies
Our aim is to offer students a window into the cultural, intellectual, and political dynamism of African societies. At a time when Africa is often represented a place in need of outsiders' benevolence and direction, we hope to give students the linguistic and interpretive tools to study African societies on their own terms. The degree will provide an excellent foundation for those who wish to expand their knowledge of Africa, and particularly for students entering positions in the arts, the media, NGOs, and other professions.

The application deadline for MPhil in African Studies 2012-13 is the 30 June 2012

KWA TAARIFA ZAIDI SOMA HAPA

Tuesday, June 19, 2012

BASATA, GABA ARTS WAENDESHA SEMINA KWA WASANII WA FILAMU

Na Mwandishi Wetu
Mkurugenzi wa asasi ya Gaba Arts James Gayo
akisisitiza jambo wakati akitoa mafunzo kwa wasanii wa filamu
Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) na asasi ya Gaba Arts mapema wiki hii wameendesha semina fupi kwa Wasanii wa filamu ili kuwajengea weledi katika eneo la uandishi bora wa miswada ya sinema (script writing).

Semina hiyo iliyoendeshwa kupitia programu ya Jukwaa la Sanaa kwenye Ukumbi wa BASATA ilijikita katika maeneo ya namna ya kuendeleza wazo hadi sinema ya kusisimua, namna ya kufikia hisia za watazamaji,ujenzi mzuri wa matukio,kutengeneza wahusika na mfumo wa hadithi, Mwanzo, kati na hitimisho.

Akitoa mada kwenye programu hiyo maalum, Mkurugenzi wa asasi ya Gaba Arts James Gayo alisema kuwa, muda umefika sasa kwa wasanii wa filamu kusaka maarifa ili kutengeneza sinema zenye visa vipya, zenye weledi na zisizosukumwa na matakwa au maelekezo ya wasambazaji.

“Wenzetu kutoka nje wanatamani sana kupata vitu kutoka Afrika vyenye kuzungumza uhalisia wa maisha ya kwetu, wanataka kuona vitu vipya hivyo, katika uandishi wa muswada wa sinema suala la uhalisia na visa vyenye utofauti ni la msingi sana” alisisitiza Gayo.

Alizidi kueleza kuwa watazamaji wa sinema (filamu) huwa wana kawaida ya kuchoka pale wanapolishwa visa vya aina moja muda wote na akaonya kuwa kama wasanii hawatajikita katika kubuni visa vipya na vyenye kugusa uhalisia wa maisha yao wadau watasusia kununua.

“Ikiwa tutaendelea kutengeneza filamu zisizo na weledi, zenye visa vilevile na zenye kusukumwa na wasambazaji au haja ya kuchuma fedha za haraka tu watu watatuchoka na baadaye soko litakufa” alionya Gayo.

Gayo ambaye amepitia mafunzo ya utengenezaji filamu katika mataifa mbalimbali ikiwemo Marekani alitaja sifa za muswada (script) bora kuwa ni pamoja na kubeba wazo linalozalika kwenye jamii, visa vyenye uhalisia na vipya, utengenezaji mzuri wa wahusika na sifa zingine nyingi.

Kwa upande wake msanii wa mashairi Mrisho Mpoto ambaye alikuwa miongoni mwa waliohudhuria semina hiyo alisema kuwa, wasanii wa filamu wanahitaji kusaidiwa kwani kwa sasa soko la filamu limekuwa la kitumwa na lenye kuburuzwa na matakwa ya wasambazaji bila weledi.

Akihitimisha programu hiyo, Katibu Mtendaji wa BASATA Ghonche Materego alishauri wasanii wa filamu kujipanga kushirikiana na wasomi wenye weledi katika maeneo yao ili kuzalisha kazi zenye weledi la ubora.

“Tuna wataalam wengi katika Sanaa, wamebanana na mambo mengi lakini ni vema wasanii tukawatumia na kushirikiana nao katika kuboresha kazi zetu” alisisitiza Materego.

Friday, June 15, 2012

FURSA YA WASANII KUJIFUNZA JINSI YA KUANDAA SCRIPT MAKINI KATIKA FILAMU


Ndugu mdau wa Sanaa,
Wadau wa Sanaa wanataalifiwa kuwa Gaba Art Centre wataendesha warsha ya masaa mawili kuhusu Stadi za uandishi wa miswada ya Sinema ( Script writing skills), Siku ya Jumatatu 18,June 2012, saa 4 kamili kwenye jukwaa la sanaa katika ukumbi wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA)

Baadhi ya mambo yatakayojadiliwa ni;

1. Namna ya kuendeleza wazo hadi sinema ya kusisimua (Idea to a good film)

2. Namna ya kufikia hisia za watazamaji (Reaching Audience emotion)

3. Ujenzi wa Action na Dialogue nzuri.

3. Kutengeneza Wahusika (Characters)

4. Mfumo wa hadithi, Mwanzo, kati na Hitimisho ( Ploting, beginning, middle and end)

Ni fursa nzuri kwa Wasanii kuleta mabadiliko kwenye tasnia ya filamu kwani kumekuwa na changamoto mbalimbali katika tasnia hii ambazo kwa njia moja au nyingine zimekuwa kikwazo katika kufikia ufanisi unaohitajika

Mbali ya kukualika wewe binafsi, ninakuomba uwaalike wanachama wako wote wanaoweza kunufaika na mafunzo haya.

KARIBUNI SANA

James Gayo (coordinator)

+255270006

Monday, June 11, 2012

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


National Arts Council BASATA

FURSA YA WASANII WA TANZANIA KUSHINDA EURO 5,000 KATIKA SHINDANO LA KUTUNGA WIMBO RASMI WA KUNDI LA MATAIFA YA AFRIKA, KARIBIANI NA PASIFIKI

(ACP GROUP OF STATES)

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo limepokea mwaliko wa Wasanii wa Tanzania kujitokeza kushiriki shindano la kutunga wimbo utakaokuwa unatumiwa kama wimbo rasmi wa mataifa ya Afrika, Karibiani na Pasifiki (ACP Group of States).

Shindano hili ambalo litahusisha mataifa 79 wanachama wa umoja huu limeandaliwa na Sekretarieti ya ACP kwa lengo la kupata wimbo ambao utabeba dhana ya mataifa ya Afrika, Karibiani na Pasifiki.

Kwa mujibu wa taarifa ya Sekretarieti ya ACP, shindano hili linamhusu msanii mmoja-mmoja au Kikundi cha wasanii ambao watapaswa kutunga wimbo huo kwa kuzingatia lengo kuu la umoja huo ambalo ni Maendeleo Endelevu na Upunguzaji Umaskini sambamba na Ushawishi mkubwa kwenye Uchumi wa Dunia.

Aidha, wimbo huo utatakiwa uwe wenye kujenga moyo, fikra na kutangaza malengo ya kundi hili la mataifa ya Afrika, Pasifiki na Karibiani.

BASATA inatoa wito kwa wasanii wa Tanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki shindano hili kwani ni heshima na fursa pekee tumepewa kama taifa kuonesha vipaji na uwezo wetu kimataifa katika eneo la utunzi wa nyimbo.

Ni wazi kuwa, kujitokeza kwa wasanii wetu wengi kushiriki katika shindano hili si tu kutaonesha utayari wa sisi kama taifa katika kushindana na mataifa mengine wanachama bali utakuwa ni mwanya wa kuitangaza Sanaa yetu ya muziki nje ya mipaka yetu.

Ikumbukwe kuwa, ushindi wa Msanii kutoka Tanzania kwenye shindano hili kutamjengea heshima msanii husika na taifa kwa ujumla.

Maelekezo kuhusu Wimbo utakaotungwa

• Tungo zote lazima ziandikwe katika moja ya lugha rasmi za ACP ambazo ni Kiingereza, Kifaransa, Kiispaniyola na Kireno.

• Wimbo huo uliokamilika lazima uambatanishwe na tunzi (lyrics) zilizoandikwa na zitumwe katika mfumo wa MP3/DVD/WAV Format

• Tungo ziguse maeneo yafuatayo

i) Fikra ya umoja ambayo itaunganisha nchi wanachama wa ACP

ii) Utajiri na tamaduni mbalimbali zilizo katika nchi wanachama wa ACP

iii) Mataifa wanachama wa ACP na kuheshimu Demokrasia, Haki za Binadamu na Utawala Bora.

iv) Nchi wanachama wa ACP na msisitizo katika maendeleo yenye usawa pia kusimamia mikataba ya kimataifa ya Haki na Amani.

Jinsi ya Kushiriki

Nyimbo zilizotungwa kwa kufuata mwongozo huo wa ACP zitumwe kupitia anuani ifuatayo ;-

Josephine Latu-Sanft (Press Office)

Avenue Georges Henri

451,1200 Brussels, Belgium

E-mail : latu@acp.int.
Mwisho wa kutuma  Agosti 31, 2012

Imetolewa na;

Ghonche Materego

Katibu Mtendaji - BASATA

Wednesday, May 30, 2012

BASATA YAWATAKA WASANII KUONGEZA THAMANI KATIKA KAZI ZAO



Na Mwandishi wa BASATA

Huku kukiwa na juhudi za kutambuliwa na kuthaminiwa kazi za wasanii ndani na nje ya nchi, Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewataka wasanii kuongeza thamani kwenye kazi zao ili kuzipa ubora zaidi.

Wito huo umetolewa mapema wiki hii na Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Habari wa BASATA Godfrey Lebejo wakati akihitimisha programu maalum iliyohusu Ubunifu, Utengenezaji na Uongezaji thamani katika Kazi za Sanaa kupitia Jukwaa la Sanaa.

Alisema kuwa, ubora katika Sanaa unapatikana pia kwa Wasanii kuangalia wenzao wanafanya nini na wao kupata ubunifu mpya kwa kuongeza vionjo, uthamani na ubunifu binafsi katika kuifanya kazi ya Sanaa kwanza kupendwa na baadaye kupewa thamani kubwa sokoni.

“Ni wazi Wasanii wetu wanapaswa kuzingatia uongezaji uthamani kwenye kazi wanazozifanya. Kubuni kazi ni suala moja lakini kuongeza uthamani katika kazi yako ili ivutie wengi na kuuzika kwa thamani kubwa ni suala lingine la kuzingatia” alisistiza Lebejo.

Aliongeza kuwa, kwa sasa kuna taarifa za Wakenya kununua kazi za Wasanii wetu kwa bei ya chini na baadaye kuziongezea ubunifu, thamani na kuziuza nje kwa bei kubwa. Katika hili anasema, inatokana na wasanii wetu kutokuzingatia falsafa hiyo ya ubunifu na uongezaji thamani wa kazi zao.

“Tuna bahati ya kuwa na malighafi nyingi sana, baadhi zimeoneshwa hapa lakini suala hapa ni sisi kutumia ipasavyo malighafi hizo katika kubuni kazi zenye ubora na kuhakikisha tunazipa thamani stahiki tunapozisafirisha nje” alizidi kusisitiza.

Awali akiendesha darasa hilo maalum ambalo wiki hii lilikuwa mahsusi kwa ajili ya wasanii na wajasiriamali wa Sanaa za mikono (Handcrafts), Haroun Sabili kutoka asasi ya Musoma Handcraft alisema kuwa, Sanaa hizo zinahitaji ubunifu na umakini mkubwa kwani kinyume chake ni kutokuvutia na kupoteza uthamani.

Alitoa wito kwa Wasanii kujiunga katika vikundi na kuwa rasmi ili kuhakikisha kwanza,wanajenga mazingira ya kuwezeshwa lakini pia kupata mafunzo mbalimbali ambayo yatawafanya wazalishe kazi za Sanaa zenye ubora na thamani kubwa.

“Ni ngumu sana kuhudumia msanii mmoja-mmoja lakini mkiwa kwenye umoja ni rahisi sana kupata fursa za uwezeshaji hususan mafunzo katika kuongeza ubunifu na uthamani wa kazi zenu” alishauri Haroun.

Katika programu hiyo iliyohudhuriwa na wadau 72, elimu kuhusu ubunifu na uongezaji thamani kwenye kazi za Sanaa ilitolewa sambamba na malighafi mbalimbali na jinsi zinavyoweza kutumika kuzalisha kazi za mikono kuoneshwa.

Tuesday, May 22, 2012

NAFASI ZA MASOMO ZAIDI (UZAMILI)

Nchini Tanzania, idadi ya vyuo vikuu imeogezeka kutoka chuo kikuu kimoja tu cha umma mwaka 1961 hadi kufikia zaidi ya vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki 60 mwaka 2012. Takwimu hizi ni kulingana na kitabu cha mwongozo wa kuomba nafasi za masomo vyuo vikuu toka mamlaka ya kudhibiti vyuo vikuu nchini TCU.

Kuongezeka huko kwa vyuo vikuu nchini pamoja na kuja kutokana na sheria ya kuruhusu vyuo hivyo, imekuja hasa baada ya kuonekana mahitaji dhahiri nchini. Idadi ya watu, hususani wanafunzi imeongezeka kwa kiasi kikubwa. Makadirio yanaonyesha kuwa kuna zaidi ya wananchi milioni arobaini hapa Tanzania, na wengi kati ya watanzania hao ni vijana. Na zaidi, kuanzishwa kwa shule nyingi za kata, japo nyingi zingali duni kiubora, kumeongeza idadi ya vijana wenye uhitaji wa elimu ya chuo kikuu. Na ukweli huo unapatikana kwa uwazi zaidi katika malengo ya kimaendeleo ya Tanzania 2025; kwamba kufikia wakati huo watanzania wengi wawe wamefikia daraja la kati.

Elimu ni njia ya uhakika ya kumuweka mtanzania wa kawaida kwenye daraja la kati kuliko njia nyingine nyingi zinazofahamika. Kwa mantiki hiyo inafaa zaidi watanzania wengi wapate elimu yenye lengo la kuwakomboa, kifikra na kiujuzi na hatimaye waelimike kwa lengo la kuwasaidia kwa maana ya kuwatumikia wananchi wenzao wengi.

Kwa mantiki hiyo vijana ama wanafunzi wengi wanahitajika kujikita vyema katika masomo wanayoyafanya, wabobee kwa uhakika hasa. Wanaokwenda kazi wakafanye kazi kwa bidii na ujuzi zaidi wanaotaka kuendelea na masomo zaidi wafanye vivyo hivyo kwa bidii bobevu. Hapa ni nafasi moja kwa wanaopenda kuendelea na masomo zaidi. Wasome hapa kuna nafasi za kutoa udhamini kwenye masomo ya juu zaidi. Udhamini wa masomo - Sholarship hapa...

Thursday, April 26, 2012

MASHINDANO YA SU-SAUT KATIKA PICHA

Kikundi cha uhamasishaji STEMMUCO
Mashabiki katika mduara wa sherehe
Mchezo baina ya STEMMUCO NA JUCO UKIENDELEA
Mashabiki wa STEMMUCO wakishangilia ushindi wa timu yao


                                                                                                                                  
   
                                                        

                          

Wednesday, April 25, 2012

Siku ya Malaria Duniani

Ugonjwa wa malaria ambao ni wakitropiki, unaendelea kuuwa watu wengi duniani na hasa barani Afrika hususani kusini mwa jangwa la Sahara. Ungonjwa huu ambao inasemekana umekuwa ukimsumbua binadamu kwa zaidi ya miaka 50'000 ni tishio kwa afya za Waafrika wengi.

Malaria huuwa zaidi kina mama na watoto
picha hii kwa hisani ya blogu hili
Asilimia 90% ya vifo vyote vya malaria hutokea barani mwetu, ambapo asilimia sitini ya vifo vyote huwa ni watoto wadogo chini ya miaka mitano. Mara nyingi malaria huambatanishwa na umasikini, na huenda ukawa moja ya vyanzo vya umasikini barani. Kuhusiswa huko na umasikini ni kutokana familia nyingi barani kushindwa kumudu manunuzi ya dawa za kuzuia maambukizi lakini pia mara nyingine kukosa uelewa wa namna ya kujikinga hususani vijijini na mijini kwenye familia zenye elimu na kipato cha kadri ama chini .
Chandarua chaweza kuzuia maambukizi
Ugonjwa huu unaweza kuzuiwa kwa kutumia chandarua kilichotiwa dawa ya kuua mbu na wadudu wengine, kusafisha vyema mazingira ya maeneo tunayoishi ili kuharibu mazalia ya mbu, kukausha na kuondoa maji yote yaliyotuama. na kadhalika.

Ugonjwa wa malaria unazuilika na inawezekana kufanya hivyo kama usemavyo ujumbe wa kataa Malaria. Na ukweli huu umedhihirika huko Zanzibar na Zambia ambapo katika ripoti za hivi karibuni, ugonjwa huo umedhibitiwa kwa asilimia zaidi ya hamsini.

Kwa kumbukumbu ya siku hii tujihadhari zaidi na kuhadharisha wenzetu wawe makini na ugonjwa huu unaoendelea kuuwa binadamu wengi zaidi mithiri ya vita.  

Taarifa za Malaria zaidi zinaweza kupatikana katika blogu hii pia. na katika blogu la unicef, who nk




Sunday, April 22, 2012

JE UMEANDIKA NINI?

Kipanya kikitoa huduma ya usafiri kwa umma. Picha toka blogu

















Hivi karibuni nilikuwa kwenye basi dogo la usafiri wa umma daladala; toka Mtwara kwenda Mikindani. Usafiri maarufu kwa daladala za Mtwara ni vipanya; vibasi vidogo vidogo ambavyo nadhani vingi ni mitumba toka Dar es Salaam. Vipanya vingi mjini hapa vimechoka na vinakwenda kwa mwendo wa kusuasua vinapokuwa barabarani. Hakuna mabasi makubwa mithili ya yale ya Mwenge Posta kwa Dar es Salaam, pamoja na hayo ule udaladala upo pale pale. Daladala ama vipanya hivi vinajaza kama ilivyo ada ya daladala sehemu nyingi Tanzania. Hapo juu nimegusia Mikindani; huu ni mji mkongwe, mji wa zamani ambao kwa bahati mbaya umesahaulika, hauendelezwi tena. Pengine kwa kuwa neema ya gesi mjini hapa imefunguliwa basi mambo huenda yakawa sawia  kwa mji huu wa kihistoria.Sasa nirejee kwenye mada ya makala hii.

Mikindani chakavu, picha na blobu ya wadau wa safari


















Katika kipanya nilichokuwa abiria, utakumbuka kuwa kwenye daladala huwa kuna mada nyingi, kondakta wetu alikuwa muongeaji kupindukia. Kodakta, konda ndivyo wanavyofahamika zaidi, huyu hatofautiani na wengi walio mikoa mingine; ni kijana aliyevalia sare chakavu ya kazi na ambapo kama walivyo wengi wao suruali yake ilikuwa ikining'inia zaiki kuliko kuvaliwa, namna hiyo ya kuvalia huitwa na vijana wa leo "kata k". Koda yule katika utani na abiria mmoja ndani ya daladala letu, ambaye nadhani ni shwahiba wake kwa jinsi walivyokuwa wameshibana kwa simulizi za kutosha bila shaka kwa lengo la kufupisha safari. Basi yule konda alimtupia rafiki yake swali ambalo hasa nd'o linabeba kichwa habari cha mada hii, hivi wewe toka umalize shule ya msingi umeandika chochote kweli?
Hivi wewe umeandika chochote kweli? Kwa hakika hili ni swali dogo sana na lategemea uzito ambao mtu ataamua kulitilia mkazo. Lakini ni jambo kubwa na muhimu sana pia. Mtu anayeandika kwa kawaida ni mtu anayesoma pia. Kwa hivi swali la konda lauliza pia, je, umesoma nini hivi karibuni? Sina hakika kama yeye mwenyewe ameandika ama amesoma chochote hivi karibuni. Tafiti na ripoti mbalimbali zinaonyesha kuwa moyo na tabia ya kujisomea kwa watu wengi imepotea ama inapotea kwa kasi kubwa . Hapo zamani ilikuwa ni lazima kuandika barua ili kujua nini kinaendelea nyumbani kwa wazazi wako walio mbali nawe, siku hizi inatosha kuweka salio katika simu ya mkoni, simu hizo karibu kila mmoja anayo yake; hii ni moja ya sekta ambazo Tanzania imepiga hatua kubwa sana, na kuanza kuongea. Anayejua kuandika ataongea kama asiyejua kuandika halikadhalika. Kukua kwa tekinolojia ya habari nako kwa kiasi kikubwa kinachangia kushuka kwa moyo wa kuandika na kusoma kama hapo awali. Hivi leo hata zile huduma za kibenki ambazo humlazimu mtumiaji kuandika japo sentensi mbili tatu zinafanywa kwa wepesi na urahisi kabisa kupitia simu ya mkononi hata na mtu asiyejua kusoma na kuandika ila tu masuala ya lazima hususani yahusuyo pesa. Maendeleo ya tekinolojia ya habari ni muhimu lakini tuendelee kujifunza kusoma na kuandika.

Hivi wewe umeandika chochote toka uhitimu elimu ya msingi, sekondari, chuo kikuu, toka upate udaktari wa falsafa?Swali hili la konda mhitimu wa darasa la saba lamgusa kila mmoja wetu toka wale wa shule ya msingi hadi madaktari wasiotimu watu ila falsafa. Nchini Tanzania pamoja na juhudi nyingi za wasomi wetu mahitaji ya vitabu vya mafunzo mbalimbali bado ni vichache; tunaendelea kutumia vitabu toka ng'ambo. Hili si jambo jema hata chembe.

Wito kwa kila mmoja wetu tuongeze muda wa kusoma vitabu zaidi na kufanya hivyo tutapata hamu na ujumbe wa kuandika chochote kitu kwa lengo la kuielimisha jamii, ambalo ni jukumu la kila mmoja wetu.