Monday, September 12, 2011

Tandahimba Pia


















Sekondari ya Milongodi ilikuwa na walimu wetu pia. Hapa mkuu msaidizi wa shule hiyo akitushirikisha jambo kuhusu sekondari hiyo ambayo ingali ikikuwa kabisa.

Katika shule hii kidato kimoja kina wanafunzi wa kiume tu bila binti hata mmoja, Zaidi ya hayo walimu, kama ilivyo katika shule nyingine nyingi, ni wachache mno. Kwahiyo, walimu mafunzoni ilikuwa ni ukombozi mkubwa kwa shule nyingi za wilayani Newaala na Tandahimba, mkoani Mtwara. Pengine muda wa mazoezi uongezwe, ili huduma hiyo iendelee kwa muda mrefu zaidi? Tutawauliza walimu hawa mafunzoni.

Walimu mafunzoni

Nilipata fursa ya kukutana na walimu-mafunzo
sekondari ya kutwa Newala mjini

Alaa kumbe ni NEWALA !














Hapa nikijiandaa kuanza safari asubuhi na mapema- mjini Newala! Picha na Eric Wamalwa

Nipo wilayani Newala. Hii ndo wilaya ya kwanza kuandikishwa hapa Tanzania, ni moja ya wilaya tano za mkoa wa Mtwara. Wilaya hii, kama jinsi ilivyo kwa maeneo mengine, ina mahitaji ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kuna makundi yote ya lazima katika jamii; watu wazima, vijana, na watoto.

Kijamii; maji ni shida (jamii imejenga utamaduni wa kuvuna maji ya mvua: karibu kila familia ina mikingio maji kwaajili hiyo – huu ni utamaduni wa kuigwa hasa na sehemu zenye mvua za kutosha. Maji hayo ya akiba yaweza kuwa na matumizi kedekede. Mfano kumwagilia bustani za mboga mboga, kuanzisha mabwawa ya samaki n.k )

Elimu: wilaya ina shule kadha wa kadha; karibu kila kata ina shule yake. Hili ni moja ya mambo mazuri ya serikali iliyopo madarakani. Ni vyema kuwa na shule za kuweza kuandikisha wanafunzi wengi iwezekanavyo. Vijana wengi wakiandikishwa shule za sekondari ndo hasa mwanzo mzuri na wa uhakika wa kupiga vita umasikini kwa vitendo. Hata hivyo mtaala wa elimu uzingatie mfumo wenye vitendo zaidi kuliko nadharia kama ilivyo hivi sasa. Vijana wetu wengi wakimalima masomo yao, kwa mfumo tulio nao hivi sasa, hulazimika kusubiri ajira. Mfumo unaofaa ni ule wa kumuandaa kijana ili aweze kujiajiri; hilo hasa ndo liwe lengo la elimu yetu. Tukirejea mada yetu; shule nyingi huko Newala zina watenda kazi wachache sana.

Shule kadhaa zina walimu wawili, watano, sita, nyingi zina idadi isiyozidi walimu kumi. Hii ni changamoto kuu na kubwa mno katika sekta ya elimu. Wanafunzi wanapokuwa na walimu wa kutosha ndo inawarahisishia kujifunza kwa ufanisi zaidi. Kwa walimu wakiwa na wanafunzi kiasi, kwao inakuwa ni vyema zaidi katika utendaji kazi wao.

Ukosefu nyumba za walimu; shule nyingi za kata zipo vijijini hasa, ni sawa kwani huko ndiko wanapoishi wananchi na watanzania wengi zaidi. na vijiji vyetu vingi havina huduma kwa wageni hususani nyumba za kulala wageni. Ukosefu nyumba za kulala wageni vijijini unakwamisha hata wakaguzi na wataalamu wa kada zingine kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi. Shule nyingi hizi za kata ama hazina nyumba za kutosha kwa walimu ama hazina kabisa nyumba hizo. Ni kweli walimu waliopo katika shule hizo ni wachache pengine inajieleza sawa pia kutokuwa na nyumba kwa walimu. Kuwa na nyumba za ziada kwa walimu inaweza kuwa ni fursa ya kuwavutia walimu wageni, ambao wengi wafikapo kujitambulisha na kuona mazingira ya shule hugoma kurejea shuleni huko.

Kisiasa: Newala ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa hivyo huko pia kuna mfumo wa vyama vingi vya kisiasa lakini wakazi wa huko wanaishi kwa amani na undugu. Hata hivyo hii ni tathmini yangu ya juma moja tu.

Kiuchumi: zao la korosho ni uti wa mgogo wa uchumi wa wilaya hiyo; wakazi wengi hujihusisha na kilimo cha zao hilo la msimu na lenye kuhitaji matunzo ya karibu hasa. Kwa wananchi wanaoweza kufuata vyema maelekezo ya wataalamu wa kilimo hujipatia mavuno na pesa nzuri kutokana na kilimo cha zao hilo. Hata hivyo mkulima siku zote huchukua tu bei inayopangwa sokoni na watu wengine; yeye hufanya kazi ngumu ya kutunza shamba na kufuatilia ukuazi wa korosho hadi kuwa tayari na kisha hapo watu wengine wenye “utu” zaidi ya mkulima hukaa meza na kupanga bei ya zao hilo kama ilivyo kwa mazao mengine ya wakulima wetu maskini hapa Tanzania na sehemu nyingi nyingine barani Afrika. Siku moja tufikie hatua ya kupanga bei ya mazao yetu wenye kwenye hilo soko la dunia; hii ni mantiki zaidi kwa kuwa wakulima wetu ndio wanafahamu haswa gharama za kilimo.

Ajira za vijana: Vijana kundi lenye nguvu na msukumo mkubwa wa maendeleo ya wakati uliopo na ujao katika jamii. Nikiongea na vijana kadhaa wa mjini Newala niligundua kuwa kuna idadi kubwa ya vijana wa kitanzania wanofanya shughuli za kiuchumi, hususan biashara nchini Msumbiji. Newala ni wilaya ya mpakani kabisa na Msumbiji. Upande wa kaskazini ya Msumbiji haujapiga hatua kubwa kimaendeleo na hivyo kutoa fursa nyingi kwa watafuta mali: hivyo vijana wetu hupitia huko na kufanya biashara za bidhaa anuwai. Vijana niliongea nao, wanijuza kuwa vijana hao wa kitanzania huko, hususani wale wenye bidii ya shughuli zao, ni wenye mafanikio makubwa.

Nyumba za kulala wageni chache: wilaya hii ina nyumba chache za kulala wageni. Upungufu huo hivyo unatoa fursa za kiuchumi kwa wananchi kujiimarisha kiuchumi na hivyo kujiongezea pato na pia kuongeza pato la taifa kwa ujumla.Kuna changamoto lakini pia fursa anuwi za kujiimarisha kiuchumi, kujiondoa kwenye umasikini na kuchangia kwa pato jumla la taifa.



Tuesday, August 23, 2011


Baadhi ya wadau wa Vijana tukisimama kwa picha ya pamoja

Wadu wa Vijana

Hapa ni Moro nikiwa na wadau wa vijana.
Hawa ni wadau toka mikoa mbalimbali waliokutana kujadili masuala ya afya ya uzazi na maendeleo ya vijana kwa ujumla.

Picha kwa hisani ya kiongozi wa mradi wa masuala ya vijana wa fhi









Saturday, August 20, 2011

Vijana Maji Moto

Picha kwa Hisani ya mtandao
Hivi karibuni tumeshuhudia harakati kubwa za vijana sehemu mbalimbali duniani. Harakati hizo zimekuwa na dhima na vyanzo tofauti tofauti. Harakati za vijana mashariki ya kati na Afrika kaskazini zilisababishwa na kukosa mahitaji yao muhimu hususani kukosa nafasi za kazi na kutokuwa na uhakika wa mustakabali wa maisha yao. Giza hilo kwa mustakabali wa maisha ya vijana ulisababishwa na ubinafsi wa viongozi wa nchi hizo. Kiongozi wa Tunisia, Ben Ali amekuwa madarakani kwa muda mrefu na amejikusanyia mali nyingi mno na hivyo kuharibu matumaini ya vijana na wananchi wake kwa ujumla. Hali kadhalika, Misri, Libya, Yemen na kwingineko mashariki ya kati.

Vijana wa Uingereza wao nao walisababisha fujo ama varangati (Kiswahili cha kizamani) lakini wao sababu ilikuwa tofauti. Makala ya mwandishi kutoka London Macha, inatoa sababu ambazo zinawapambanua vijana wa Uingereza na wale wa Mashariki ya kati. Wachambuzi wengine husema kuwa vijana wa dola hiyo kuu zamani, wanafundishwa tu/ ama zaidi juu ya haki zao, hawafahamu kuhusu wajibu wao kwa jamii. Hili ni tatizo kubwa. Vijana wanapokua ni vyema tukawajuza haki zao, lakini muhimu kabisa watambue pia namna ya kuwajibika kwa jamii zao. Hili ni jambo la kila mahali Tanzania na nchi nyingine zote duniani, na tena muhimu kwa wananchi na pia serikali kutoa mchango wo kwa maendeleo ya vijana.

Tanzania kuna asasi zisizo za kiserikali (AZAKI) lukuki zinazojihusisha na masuala ya vijana. AZAKI hizo zimeanzishwa na wananchi kwa malengo lukuki, ikiwa ni pamoja na kuwahudumia vijana. Hili ni jambo jema kwani vijana ni moja ya makundi yaliyo muhimu kwa maendeleo ya jamii ya wanadamu. Hata hivyo katika siku za nyuma kidogo kulizuka AZAKI nyingi ambazo hazikujali masilahi ya walengwa husika bali waanzilishi kujijaza mapesa.

Serikali yetu Tanzania, imepiga hatua kubwa hasa kwa kuwa na utashi muhimu wa kisiasa na kuazisha shule za sekondari kila kata. Bila ubishi hii ni hatua kubwa sana ya kuelekea maendeleo ya kweli. Elimu mwanzo wa ustaarabu wote duniani; elimu kwa upana wake si tu ile ya darasani. Hata hivyo changamoto kubwa kwa serikali ya Tanzania na wananchi wake kwa ujumla wao ni kuziboresha shule hizo lukuki za kata. Ni muhimu kufanya hivyo kinyume na hapo tunapata taifa la watu walioelimika nusu nusu. Hii elimu nusu ni hatari sana, pengine afadhali asiyeipata kabisa; mwenye elimu nusu hatokubalika katika kundi la wajinga kabisa kwani ana maarifa kiasi na hivyo kuwa tofauti na wasiosoma kabisa, lakini hawezi changamana pia na walioiva vilivyo kielimu kwake itakuwa ni kujinyanyapaa – “kujichora” (maarufu kwa vijana) mbele ya wasomi. Ni hatari kama nusu wasomi hawa watakuwa wengi; watadai haki kwa njia zisizokubalika kwani elimu yao yawatuma hivyo.

Hivyo AZAKI zilenge kuwasaidia vijana wapate stahili yao. Wananchi wote kwa ujumla na serikali kwa maana ya dola tujipange kuziboresha shule hizi haraka iwezekanavyo kama inavyoelezewa kwenye MKUKUTA II ili kuepukana na nusu wasomi na matatizo mengi toka kwa vijana wetu siku zijazo.

Wednesday, August 3, 2011

Familia Inafaa - Families Matter Program! FMP

Hapa nikiwa na mratibu wa Mradi wa Familia Inafaa huko mkoa wa Ruvuma. Wanakikundi ni wadau wa Familia Inafaa katika mkoa wa mashujaa wa kingoni, nyumbani kwa simba wa vita 



Hapa nikiwa na raia wa siku nyingi hapa Tanzania. Mzee huyu ananipatia somo juu ya malezi kulingana na uzoefu wake wa siku nyingi duniani hapa- asante mzee! 



      
                                                                                                                                                               Hapa nikiwa na wadau wa Familia Inafaa mkoani Mtwara; hapa ni kijiji cha Nanguruwe Mtwara Vijijini!


Familia Inafaa – Families Matter Program! (FMP)













Huu ni mradi unaongozwa na Kampuni ya T-MARC. Mradi huu unawalenga wazazi, walezi na wadau wa malezi ya watoto ambao bado hawajabalehe kwa wavulana na hawajavunja ungo kwa mabinti. Familia Inafaa! Ni mradi ambao tayari umeshaanza kutoa huduma kwa wazazi na walezi wa mikoa ya Mtwara na Ruvuma.
• Lengo la msingi kabisa la FMP ni kuwatia shime wazazi katika juhudi zao za kuwalea watoto wao ili wakue katika afya njema.

• FMP ni program mahususi kwa ajili ya wazazi. Imeandaliwa katika namna ambayo inawasaidia wazazi kutumia mbinu ambazo zinaweza kuwalinda watoto wao dhidi ya tabia hatarishi za afya ya jinsia, hivi sasa na wakati ujao pia.

• FMP inaamini kuwa wazazi wana nafasi yenye ushawishi mkubwa wa kujenga, katika namna chanya tabia za kiafya za watoto wao.

• Lakini hata hivyo ushawishi huo ni lazima ushindane na ujumbe wanaoupata watoto wao toka kwenye vyombo vya habari, vijana wenzao, na jamii yote kwa ujumla.

• Mawasiliano ya wazazi yanaweza kuwalinda watoto, kujenga uwezo wa kufanya maamuzi yafaayo, na kufikisha ujumbe sahihi.

• FMP inataka kuwasaidia wazazi “kuongeza ujuzi wao” kwa kuwapatia vifaa na mbinu mahususi kabisa ili waweze kuwa na mtindo bora wa afya katika familia zao.