Monday, December 28, 2015

MAISHA NI MALENGO




                                              Imepakuliwa hapa:https://www.youtube.com/watch?v=G23nC6i5jl8
Leo ni mwanzo wa juma jipya, mwezi mpya, mwanzo wa miezi mipya kumi na mbili ama maarufu zaidi mwaka mpya.

Mwanzoni mwa mwaka ni kipindi kizuri kufanya tathmini ya kile tulichokuwa tukikifanya kama hatukufanya hivyo mwishoni mwa mwaka. Ama yaweza kuwa fursa ya kuweka malengo mapya ama kuyapitia yaliyotangulia kwaajili ya muda mpya unaoanza mbele yetu.

Kufanya tathmini ama kujiwekea malengo katika maisha ni suala la msingi mno kama tunataka kuishi katika namna inayoeleweka na yenye tija na mchango katika dunia yetu. Lengo la maisha kwa kila binadamu awe anafahamu ama la ni kuwa na furaha maishani. Aristotle, mwanafalsafa wa kale anasema hivyo pia; ili mtu awe na furaha basi hana budi kujiwekea malengo. Malengo huwekwa na watu wa kila kada.

Mwalimu shuleni hujiwekea malengo yake, mwanafunzi, mwanasiasa, mwanamichezo, mwanasanaa, mwanauchumi, msomi, mwanazuoni, mwanasheria, mkufunzi, mfanyabiashara, mkulima, mchungaji kanisani, shehe msikitini, imamu sinagogini, na kadhalika…watu wote makini wa kada zote hujiwekea malengo maishani. Kutokuwa na malengo maishani ni mithili ya muuza duka bila daftari, ambapo twajua mali bila daftari hupotea bila habari. Maisha bila malengo hupotea bila taarifa.

Kujiwekea malengo ni utamaduni ambao inafaa watu wote tuwe nao. Kwa kusema hivyo nafahamu fika kuwa kuna ndugu wasio na mazoea ya kufanya hivyo; watu hao mara nyingine hufananishwa na bendera fuata upepo hufuata chochote kitakachokuwa mbele yao. Bila ubishi si utaratibu mzuri wa maisha. Kwa wasio na utaratibu huo ni wakati sawia kuuanzisha.

Dini nyingi hutueleza kuwa hapa duniani ni sehemu tu ya mpito - twapita tu na kwamba makao yetu halisi yapo kwa muumba wetu. Hivyo wakati tukiandika malengo yetu ya maisha ni vyema tukamshirikisha huyo muumbaji kwa kuwa sisi hatujui siku wala saa ya kuyahama makazi ya hapa duniani, japokuwa hatutakiwi kuogopa kifo.

Unapoandaa malengo fanya hivi:

Kwa wanandoa, ama watarajiwa, wawashirikishe wenzi wao. Malengo haya si yako peke yako. Kwa hiyo nafsi ya kwanza ni Mwenyezi Mungu na pili ni mwenzi wako wa maisha; mkeo, mumeo ama mchumba wako. Muombe(ni) Mungu ili awaangazie kufanya malengo ya kweli.

Hatua ya pili ni kuwa mkweli na hali yako halisi; weka malengo ambayo yana uhalisia wa maisha yako. Mfano haina maana kwako mwanafunzi wa Tanzania kuwa na lengo la kuwa rais wa Pakstani miaka mitano ijayo. Weka malengo ambayo kwa kiasi fulani una nafasi ya kuyatekeleza. Mfano kusoma kozi ya Kifaransa kwa undani mara baada ya kumaliza masomo yako mwezi wa Juni.

Weka malengo yenye kukujenga na yatakayohitaji juhudi zako kuyatimiza.

Usiogope kuwa na malengo mengi bora tu ni muhimu katika makuzi na utu wako, mwisho wa muda wa kuyatimiza utakapowadia utakuwa na wasaa wa kujitathmini na kujua wapi ulihitaji ama utahitaji juhudi zaidi. Mara nyingine tukiwa na malengo mengi na yenye kudai juhudi zetu zaidi ndipo ambapo huwa na mafanikio zaidi maishani.

Usiwe mtu wa kujihurumia; kuona kuwa malengo haya ni mengi na magumu mno siwezi kuyatimiza. Usishindwe kujaribu, jaribu kutenda na ukishindwa wakati ukitenda ni tofauti kabisa na ukishindwa kujaribu kufanya chochote.

Jiamini na usijilaumu. Fanya utakachoweza kwa juhudi zako na mambo yakienda kombo, bila shaka utapata fursa nyingine ya kutenda tena!



Kila la heri na Mungu akubariki!

Mandalu
01/01/2012

Tuesday, December 15, 2015

MAGUFULI APASUA VICHWA WASOMI


WAKATI wananchi wengi wakipongeza hatua ya Rais Dk. John Magufuli kuelekeza pesa zilizochangwa kwa hafla ya kuzindua Bunge kununua vitanda katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, wapinzani wake wanaeleza huo ni mwanzo wa kushindwa katika vita dhidi ya ufisadi.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Profesa Mwesiga Baregu amesema hatua ya Rais Magufuli kupokea pesa hizo bila kuhoji malengo na msingi wa Mhimili huo wa kutunga sheria kuchangiwa fedha ni ishara ya wazi kuwa ameingia kwenye mtego wa ufisadi wa kimfumo.

“Bunge ni taasisi nyeti sana kuruhusu kuchagiwa pesa na watu ambao linapaswa kuwasimamia, hizi taasisi za fedha zilizochangia zinaweza kujikuta zinatakiwa kuchunguzwa na Bunge, credibility yake itakuwa wapi. Angeuliza kwanza kwanini wamechangisha pesa hizo, nani anawajibika nazo?

“Kama anasimamia uadilifu hakupaswa kuchukua tu hela ambazo zimechangwa bila kujua dhamira za wachangiaji, huko tunakokwenda tunahitaji miswada ya kusimamia sekta ya fedha, sheria za kodi wanapolipia dhifa ya kwanza ya kufungua Bunge, huu ni mtego, kwani Bunge haliwezi kupewa uwezo wa kuchukua hazina kiasi kidogo hata kama ni shilingi milioni tano kufanya mambo yake, dignity (heshima) yetu iko wapi kama tuna Bunge omba omba na hatujui dhamira za wachangiaji?” alihoji Profesa Baregu.
Aliongeza kwamba huo ndiyo ufisadi wa kimfumo unaoitesa Tanzania, huku akiweka wazi kuwa anazofanya sasa Rais ni mbio za sakafuni kwa kuwa hawezi akadumu na hali hiyo.
“Mkapa (Benjamin, Rais wa awamu ya tatu) alianza na kasi kuliko hata hii, pamoja na juhudi kubwa za Mwalimu Nyerere, kumtangaza kuwa Mr. Clean, kuunda Tume ya Warioba kuhusu rushwa na kuwa na baraza aliloiita la askari wa miavuli, ameishia wapi, katika kipindi chake ndiyo kashfa nyingi za ufisadi zimeibuka. Simuoni kama atakuwa tofauti na watangulizi wake,” alisema.
Ni kama Nyerere
Wakati Profesa Baregu anayatazama mambo kwa jicho hilo mchambuzi wa masuala ya siasa nchini Dk. Charles Kitima ameliambia Raia Mwema kuwa Rais Magufuli, amejipambanua kuwa ni aina ya kiongozi anayeweza kutekeleza anayoyasema kutokana na rekodi yake ya utendaji.
Amemweleza Rais Magufuli kuwa ni kiongozi wa kipekee ambaye hotuba yake ya kuzindua Bunge imeonyesha ni jinsi gani anaweza kuunganika na wananchi masikini wa ngazi ya chini.
“Hotuba yake imegusa watu wa kawaida kabisa, kama zilivyokuwa hotuba za Mwalimu Nyerere, anasema kwa lugha inayotoka moyoni, pengine ni kwa sababu ameishi maisha ya kawaida, ndiyo maana ameweza kuwavutia wengi,” alisema Dk. Kitima.
Aliongeza kwamba ingawa hotuba za mwanzo za viongozi ni kujaribu kuwaaminisha wananchi kwamba atatekeleza ahadi zake alizoahidi wakati wa kampeni, utekelezaji wa ahadi hizo hutegemea aina ya kiongozi husika.

Katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge pamoja na mambo mengine aliwekea umuhimu suala la kubana matumizi ya serikali ili fedha zinazookolewa zielekezwe kwenye huduma za jamii.

Ili kuonyesha alivyodhamiria kulitekeleza hilo, juzi Jumatatu, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alisema Rais Magufuli ameagiza kufutwa kwa sherehe za uhuru ili watu watumie siku hiyo kufanya kazi ya usafi.
“Hatuwezi kusherehekea miaka 54 ya Uhuru huku tukiendelea kusumbuliwa na ugonjwa wa kipindupindu unaoweza kuzuilika kwa kufanya usafi tu. Hii ni kejeli kwa taifa huru kwa zaidi ya miaka 50.

“Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri wameagizwa kununua vifaa vya kufanyia usafi ili siku hiyo tuiadhimishe kwa utaratibu maalumu wa kupambana na kipindupindu,” alisema Balozi Sefue.
Akizunngumzia hotuba hiyo, aliyekuwa mtia nia ya kuwania urais kupitia CCM, Williamu Ngereja alisema hotuba hiyo ya Rais Magufuli ni mwanzo mpya kwa taifa.
“Hotuba ya Rais Magufuli ni mwongozo sahihi kwa taifa letu kufikia malengo ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Kama wananchi wanataka mabadiliko ya kweli, kama walivyoonyesha kwenye kampeni, kila mtu anapaswa kumuunga mkono,” alisema Ngeleja. - 

CHANZO CHA HABARI HII :http://www.raiamwema.co.tz/magufuli-apasua-vichwa-wasomi