Sunday, December 25, 2011

YOSEFU NA VIJANA WA LEO


Yosefu ama Yusufu alikuwa baba mlishi wa mtoto Yesu. Ndugu huyu alikuwa na mchumba aliyejulikana kwa jina la Maria ama Mariamu; wote wawili walikuwa Wayahudi. Kabla ya kuishi pamoja kama mume na mke, Mariamu alionekana kuwa mjamzito. Kwa taratibu za kiyahudi, husasani za wakati ule, Yosefu alitakiwa kutoa taarifa kwa wahusika na binti huyo angeuwawa kwa kupigwa mawe. Yosefu lakini aliadhimia kumuacha kimya kimya yule binti. Maandiko yanatuambia kuwa Mwenyezi aliingilia kati na hatimaye Yosefu akamchukua mchumba wake.

Vijana wa kiume hapa Tanzania na duniani kote wanaweza kujifunza tabia hiyo ya Yosefu. Vijana wetu wa kiume wakijifunza tabia hiyo basi matatizo mengi yanayoisibu jamii yetu yanaweza kupungua ama kuisha kabisa.

Vijana hawawezi kukataa mimba wanazowapa mabinti na kisha kuwakana. Hii itasaidia kupunguza watoto wa mitaani. Miji yetu mingi mikubwa ina watoto wengi wa mitaani; watoto hawa kwa kiasi fulani ni matokeo ya kina kaka na kina baba kuwatelekeza wake na ama wachumba wao, wao pekee na watoto. Basi sherehe hizi za Krismasi tunaweza kuzitumia kuwakumbuka watoto wa mitaani na sisi kubadilisha tabia zetu kwa mfano wa Yosefu.

Wednesday, December 21, 2011

Mvua kubwa zaleta madhara Dsm

Picha hii kwahisani ya blogu la mjengwa inaonyesha wanachi
wakijaribu kuokoa mali zao toka kwenye nyumba zilizojaa maji.
Kwa siku ya tatu mfululizo mvua zimeendelea kunyesha jijini Dar es Salaam na kusababisha maafa makubwa ikiwa ni pamoja na maisha kupotea.

Mamlaka ya hali ya hewa Tanzania wamesema kuwa mvua hizi zimezidi vipimo vyote vilivyorekodiwa toka mwaka 1954. Utaona kuwa ni mvua kubwa hasa.






Hii ni shida kubwa kwa jiji la Dar es Salaam ambalo sehemu kubwa halijapangiliwa vizuri kuwa makao ya kuishi binadamu. Kwa kuwa tumekumbwa na baa hili, tunawapa pole sana ndugu zetu wanaopitia hali hii nguvu ambayo haijawahi kutokea ndani ya Tanganyika na kisha Tanzania huru. Pole sana kwa msiba huu mkubwa; kwa hakika ni janga la taifa.

Pengine tatizo hili litupatie funzo wananchi tunaojenga maeneo ambayo si rasmi. Maeneo ya mabondeni siku zote wananchi tumekuwa tukiambiwa tusijenge lakini hatujali maelekezo rasmi na ya kitaalamu. Tatizo kama hili likitokea basi tunalazimika kuwasaidia ndugu hawa kwa kuwa ni binadamu wenzetu na hatuwezi kuwaacha katika matatizo. Hata hivyo sasa ni lazima kufuata taratibu rasmi ili kuweka mambo katika mstari mnyofu.

Mafuriko ya mara hii yamegusa hata maeneo rasmi, hii inaonyesha shida kubwa ya miundo mbinu mibovu ya jiji kuu hilo la kibiasahara hapa Tanzania. Ni lazima sasa kwa wadau wa miundo mbinu, mipango miji na wengine wote wanaohusika kwa karibu kuhakikisha kuwa mifumo muhimu na ya msingi kama vile maji taka, iwekwe vyema zaidi; tusisubiri tena kutokea kwa maafa kama haya tena.