Saturday, July 26, 2014

SOKO LA KIBEPARI NA PANDE ZAKE MBILI

Wachumi na wapiga debe wa “mfumo wa uchumi wa soko wenye ubinadamu” ( The market friendly approach ) [Tafsiri hii ni yangu binafsi ] ambao lengo lao ni kuona uchumi unakuwa, kupitia mabadiliko katika taasisi, kupunguza rushwa, na kuhakikisha maisha ya watu kupitia huduma muhimu kama afya, elimu, uhakika wa chakula na kadhalika yanakuwa bora zaidi. Njia hii ni mbadala wa njia zingine zilizotangualia (sitaki kuingia katika nadharia hii ya Neo-liberalism kwa ndani).

Nadharia hii yenye kulenga kupunguza umasikini inazishauri nchi “masikini” kushirikisha Serikali na sekta ya umma kukuza uchumi na kupambana na umasikini. Kwa hiyo wadau wakubwa wa kujenga uchumi na kupunguza umasikini katika jamii ni wadau hao wawili; serikali na sekta binafsi. Nadharia hiyo inashauri uchumi kwa kiasi kikubwa uendeshwe na sekta binafsi ilhali serikali iandae miundo mbinu na mazingira yenye kuiwezesha sekta binafsi katika shughuli za kujenga uchumi; lakini serikali inapewa jukumu na fursa ya kuirekebisha sekta hiyo binafsi yenye jukumu kubwa la kuzalisha uchumi. Kwahivi serikali kazi yeke kuu ni kusisimua, kuibua fursa, kujenga mazingira na kurekebisha wazalishaji pale wanapoelekea kupotoka.

Nadharia hii ina mashabiki na pia wapinzani wa kutosha tu: lengo la makala hii hata hivyo si kuichambua nadharia hii bali kuongelea kwa ufupi tu mfumo wa biashara nchini Afrika Kusini. Naongea kupitia uzoefu wangu wa miezi michache nchini Afrika Kusini; nitaandika kwa uhuru kama nilivyokuwa nikifanya wakati wa kuandika insha shule ya msingi hadi kidato cha kwanza. Tuliandika kwa uhuru mkubwa na kutumia vizuri zaidi hisia, kumbukumbu na uzoefu wetu. Hatukubanwa na takwimu, ambazo kwenye makala za baada ya shule ya msingi tumefundishwa kuwa ni muhimu na mara nyingine lazima. Sasa tuangalie biashara nchini Afrika kusini.

Afrika Kusini ina mfumo wa kipepari; uchumi wake kwa kiasi kikubwa unaendeshwa na soko. Natazama hapa soko la mahitaji ya kila siku ya binadamu. Moja ya sifa ya nchi za kibepari ni kuunganisha bidhaa za mashambani katika mfumo wa soko wa bidhaa za viwandani. Kwahiyo masoko yanakuwa na bidhaa za mashambani na viwandani hali kadhalika. Hivyo katika soko moja utakuta viatu, nguo na kadhalika [n.k] (bidhaa za viwandani), nyanya, maboga, mahindi mabichi, n.k (bidhaa za mashambani). Najua masoko yetu pia yanafanya hivyo ila kuna tofauti kubwa iliyopo kati ya masoko yetu Tanzania na ya Afrika Kusini [A.K].

Masoko nchini Afrika Kusini ambayo mengi ni mtandao wa wamiliki kadhaa wenye nguvu ya uchumi yamewekwa katika namna ambayo hupatikana katika miji karibu yote. Masoko hayo makubwa kwa kawaida hupatikana katika miji midogo, mikubwa na majiji. Eneo moja huweza kuwa na makampuni kadhaa ya kibiashara, kulingana na ukubwa wa mji na uchumi wa eneo husika. Kwa Tanzania mfano sahihi ni ule wa soko la Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Soko la Mlimani City, Dar es Salaam
Kama ilivyo kwa Mlimani City, Dar es Salaam, masoko ya A.K hujumuisha makampuni kadhaa ndani yake. Muhimu na kubwa zaidi ni kuwa masomo hayo, kwa kawaida, yameunganishwa na mfumo wa kibenki ambapo wateja wana uhuru wa kuingia na pesa taslimu ama kadi za benki zenye pesa ndani yake. Mteja huchagua bidhaa anazotaka na kulipia kwa njia iliyo muafaka kwake; kwa pesa taslimu ama kwa kuchanja kadi yake ya benki.

Kwa kawaida Masoko hayo huwa na umeme wa uhakika muda wote; kwa kuwa kuna bidhaa zenye kuhitaji majokofu. Nyama, Samaki, vinywaji mbalimbali n.k. Lakini pia mfumo wa malipo huhitaji umeme muda wote. Zaidi masoko haya ni chanzo kikubwa cha ajira; watu wengi hupata fursa za kufanya kazi za aina mbalimbali. Unaweza kuorodhesha nafasi chache tu hapa: wauzaji (wapokea pesa), wapanga bidhaa, wakagua bidhaa, wasukuma mikokoteni, n.k

Masoko ya A.K yana sifa nyingine muhimu ya kuwa na wateja wenye kupenda kufanya manunuzi (nadhani hii ni kutokana na uimara wa uchumi na aina ya utamaduni); wananchi wengi wana uwezo kununua bidhaa nyingi na kulipia kila bidhaa walioichagua. Utakumbuka mfumo wa soko wa aina hii unauza karibu kila kitu kinachohitajika katika matumizi ya mwanadamu. Wakati sehemu nyingi nchini Tanzania uchumi wetu unaruhusu mtu kujipatia mahitaji yake toka vyanzo vingine mbali na soko; mfano kwenye bustani yake atakula machungwa, maembe n.k, toka shambani kwake atakula viazi, mihogo n.k. Nchni A.K bidhaa nyingi kwa watu wengi hupatikana kwenye masoko hayo tu.

Ni utamaduni wenye uzuri na ubaya wake pia; si lengo langu kukugusa mada hii kwa undani hivi leo, lakini inafaa kusema chochote juu yake. Mfumo huu wa soko una faida lukuki lakini pia mapungufu hayakosekani. Nitaelezea jambo moja tu kwa kila upande uzuri na udhaifu wake.

Mfumo huu wa soko, ni njia ya uhakika ya ukusanyaji kodi. Serikali kupitia mamlaka zake husika hukusanya kodi kwa uhakika kabisa. Kodi, twafahamu ni muhimu kwa maendeleo ya taifa lolote duniani. Ni kupitia kodi ndio serikali inapata nguvu ya kuwapatia wananchi wake hudumu za msingi kama hospitali, shule, n.k

Mfumo huu wa soko, kwa maoni yangu, una shida kwenye bidhaa za vyakula. Wahitaji wa bidhaa kadhaa mara nyingine ni wengi kuliko uzalishaji wa asili unavyoweza kumudu mahitaji ya wateja hao. Ili kukidhi mahitaji hayo basi ni lazima kutafuta njia ya uzalishaji ambayo ni ya bandia, matumizi ya teknolojia yanaingia hapo. Si kila jambo linalotumia teknolojia ni jema. Chukua uzalishaji wa mayai kwa njia ya asili. Kwa kawaida kuku anapotaga yai basi kwa siku ni yai moja tu. Lakini kuna watu wanakula zaidi ya yai moja kwa siku. Hivyo basi ili kukidhi haja ya walaji lakini na ili kupata faida haraka ni lazima teknolojia iingie kati na kuzalisha mayai mengi kwa siku moja. Mfano huu unaweza kutumika kwa bidhaa nyingine za vyakula. Mfumo huu unalzimu bidhaa nyingi za vyakula kuzalishwa kwa teknolojia. Hivyo bidhaa nyingi za vyakula zinakosa virutubisho na viini asilia ambavyo sehemu nyingi nchini Tanzania bado tunaendelea kuvifurahia…

Mambo mengi ndivyo yalivyo, kama sarafu, yana pande mbili…

Baadhi ya makampuni ya kibiashara nchini Afrika Kusini, ambayo baadhi yake hupatikana pia Afrika Mashariki ni pamoja na  Picnpay, Spar,Checkers, Shoprite, Pep, mrprice, edgers, kfc, lewis, steers, jetmart