Sunday, February 5, 2017

AZIMIO LA ARUSHA LINAPOFIKISHA MIAKA 50 : NINI KILISABABISHA KUZALIWA KWAKE?


Hivi leo Azimio la Arusha (AA) limefikisha miaka 50 ama nusu karne tangu kutangazwa kwake.... Tarehe 05.02.1977 ambayo ni miaka hamsini ama nusu karne iliyopita, lilitolewa tamko ama tangazo la kihistoria katika mji wa Arusha. Azimio hilo linaendelea kujulikana kama Azimio la Arusha hata hivi leo.



Lengo la Azimio la Arusha
Kimsingi lilikuwa ni kuboresha maisha ya Watanganyika wanyonge. Azimio la Arusha lililenga kuboresha nyanja zote za maisha ya wananchi wa kawaida lakini hasa ililenga kuboresha nguvu yao kiuchumi na kisiasa. 

Tanganyika ilijipatia uhuru wake wa kisiasa 09.12.1961 bila kufahamu kuwa uhuru wa kiuchumi uliendelea kuwa mikononi mwa wakoloni. Tanganyika ilirithi uchumi wa kibepari, tena ubapari wa kikoloni. Kwa mantiki hiyo utaona kuwa "sisi" tulikuwa na uhuru kisiasa ilihali "wao" walikuwa na uhuru wa kiuchumi.

Uchumi huo wa kibepari wa kikoloni ambao ulikuwa ukiongozwa kwa sheria za soko, ulikuwa kandamizi kwa wananchi wa kawaida. Wananchi waliofanya kazi kwa matajiri wa kigeni na kupangiwa mishahara kwa matakwa ya matajiri hao kabla ya uhuru waliendelea kufanya kazi kwa namna ile ile kama walivyofanya hata kabla ya uhuru wa kisiasa. Wakulima hali kadhalika walijikuta katika mazingira yale yale wakiuza mazao yao kwa mabwana wale wale na kwa bei zile zile za kabla ya uhuru.

Kutoka na uchumi ule wa kibepari, serikali haikuwa na uwezo wa kuingilia masuala ya uchumi huo na hivyo haikuwa rahisi kuwawezesha wananchi kuonja ama kushiriki katika furaha ya matunda ya uhuru. Hivyo basi kama ilitakiwa wananchi waonje ladha ya matunda ya uhuru wao basi ilikuwa lazima kwa TANU kudai ama kuchukua pia uhuru wa kiuchumi na mabadiliko hayo yalikuwa lazima.

Ili kusikiliza kusikiliza wananchi na kuhakikisha kuwa wanahisi faida za uhuru katika nchi yao, ndipo hapo chama cha Tanganyika African National Union kilipofanya maamuzi ya kihistoria.

Chama cha TANU kilitangaza za na historia mpya kabisa katika taifa changa la Tanganyika. Mnamo tarehe tano Februari mwaka elfu moja mia tisa sitini na saba pale mjini Arusha chama kilitangaza rasmi kuwa kuanzia siku hiyo nchi ya Tanganyika ilikuwa inaanza na inaingia katika siasa za ujamaa na kujitegemea.

Siasa ya ujamaa na kujitegemea ilijengwa juu ya nguzo mbili za (i) Utaifishaji wa njia zote kuu za uzalishaji mali na (ii) Vijiji vya ujamaa na kujitegemea kama nguzo muhimu kufikisha maendeleo kwa wananchi wengi.

Nini kilifanyika ndani ya siasa za ujamaa na kujitegemea? Hii ni mada ya wakati mwingine; kwa leo itoshe tu kuona kilichofanyika.

No comments:

Post a Comment